Maadhimisho hayo mapya yanaangazia urithi wa pamoja wa lugha na utamaduni wa jamii zinazozungumza lugha za Kituruki, na kuimarisha dhamira pana ya UNESCO ya kukuza matumizi ya lugha nyingi na utofauti wa kitamaduni.

Tarehe ya kihistoria

Uchaguzi wa tarehe 15 Desemba unatokana na tukio muhimu katika taaluma ya isimu. Siku hiyo mwaka 1893, mwanaisimu kutoka Denmark, Vilhelm Thomsen, alitangaza kuwa alikuwa ametafsiri herufi za Maandishi ya Orkhon moja ya rekodi za kale zaidi zilizoandikwa za familia ya lugha za Kituruki.

Ugunduzi huo uliweka msingi wa kuelewa kwa kina zaidi mapokeo ya lugha ambayo leo yanaunganisha jumuiya nyingi kote Eurasia.

Familia ya lugha ya kimataifa

Lugha za Kituruki zikiwemo Kiazerbaijani, Kikazakh, Kikyrgyz, Kituruki, Kiturkmen na Kiuzbek zinazungumzwa kama lugha mama na zaidi ya watu milioni 200 katika eneo linalokadiriwa kufikia takribani kilomita za mraba milioni 12.

UNESCO inabainisha kuwa lugha hizi zinabeba urithi mkubwa wa maandishi, mapokeo imara ya simulizi za mdomo na desturi mbalimbali za kitamaduni zinazoshirikiwa katika nchi nyingi wanachama.

Kutangazwa kwa siku hii mpya kumefuatia ombi la pamoja kutoka Azerbaijan, Kazakhstan, Kyrgyzstan, Uturuki na Uzbekistan, na kuungwa mkono na Nchi Wanachama 21, hatua inayoonesha kutambuliwa kwa mapana kwa thamani ya utofauti wa lugha.

Kuimarisha ushirikiano

UNESCO inasema maadhimisho ya kila mwaka yanaendana na ajenda pana ya Umoja wa Mataifa ya kukuza matumizi ya lugha nyingi, kama ilivyoainishwa katika azimio la Baraza Kuu 71/328.

Kwa kutenga siku maalum kwa familia ya lugha za Kituruki, shirika hilo linalenga kuhimiza ushirikiano wa lugha, kubadilishana tamaduni na mazungumzo kati ya ustaarabu.

Shughuli zilizopangwa ni pamoja na kampeni za uhamasishaji, utafiti wa kitaaluma na programu za kulinda lugha za Kituruki pamoja na mapokeo yao ya simulizi za mdomo.

Maadhimisho ya kila mwaka

Siku hiyo itaadhimishwa kupitia maonesho, mihadhara, matukio ya fasihi na maonesho ya kisanaa yanayolenga kuonesha kina cha kihistoria na uhai wa sasa wa lugha za Kituruki.

UNESCO inasema maadhimisho hayo ni fursa ya kuheshimu utofauti wa lugha kama sehemu ya urithi wa pamoja wa binadamu na kuimarisha juhudi za kimataifa za kulinda lugha kama vyombo muhimu vya utambulisho, maarifa na maelezo ya kitamaduni.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *