DAKTARI Bingwa Bobezi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Frank Muhamba amejiwekea utaratibu wa kutumia muda wake wa likizo kutoa huduma za kibingwa bobezi katika Hospitali ya Rufaa ya Bukoba kama sehemu ya kurudisha kwa jamii.
Akizungumza na Azam TV juzi, Dk Mhamba amesema kuwa ana miaka mitatu tangu aanzishe utaratibu huo ambao kusudi lake ni kuisaidia jamii iliyomlea ambayo wakati mwingine hukosa fedha za kugharamikia matibabu katika hospitali kubwa.
“Lengo langu ni kurudisha kwa jamii, nimezaliwa katika mkoa huu, nimesomea katika mkoa huu kwa hiyo sina namna nyingine ya kurudisha katika jamii yangu zaidi ya kuja kubadilishana uzoefu na wataalamu wa hospitalini hapa. Ni katika hali ya kuboresha na kutoa huduma kwa wagonjwa katika ngazi ya udaktari bingwa bobezi,” alisema.
Ameeleza kuwa hugawa siku 28 za likizo yake ambapo hutumia wiki mbili kuwa na familia yake, wiki moja kwa ajili ya kutoa huduma hospitalini hapo na wiki nyingine moja kwa ajili ya kwenda kuiona familia ya kijijini kwao. SOMA: Serikali kuimarisha tiba bobezi – Mhagama
Ameongeza kuwa matamanio yake kwa siku za mbele ni kupata watu wa kuunga mkono mpango huo na kuwa wakiunganisha nguvu huduma hizo zitapatikana kikamilifu. “Najua kuna wazaliwa wengi wa mkoa huu, marafiki wa mkoa huu kila mtu kwa nafsi yake kuna kitu anachoweza kusaidia, tutaunganisha nguvu ili hizi huduma ambazo tunakuja kutoa hapa za kibobezi basi ziweze kupatikana hapa kikamilifu na kusiwe na kikwazo cha vifaa au kikwazo cha wataalamu kama tukiwa na moyo huu wa kuja kusaidia,” alifafanua.
Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Bukoba, Dk Theomon Theophil amesema hospitali hiyo ndio hospitali kubwa zaidi mkoani humo ambayo ina huduma za kibingwa lakini haina huduma za kibingwa bobezi hivyo, uwepo wa madaktari kama Dk Mhamba husaidia wananchi kupata huduma hizo na kusaidia madaktari waliopo kupata ujuzi mpya.
Daktari wa Upasuaji katika Hospitali ya Rufaa ya Bukoba, Dk John Richard amesema,“Tumenufaika kwa kupata ujuzi kutoka kwake kwa kufanya operesheni ambazo ni adimu.” Aliongeza: “Amejitolea kuja kufanya hizi huduma ambazo sisi madaktari ambao ni wa jumla hatuwezi kuzifanya, ujio wake umetusaidia tumefanya naye tumeona baadhi ya operesheni ambazo zinaweza zikafanyika, tunaweza hata sisi kuzifanya.”
