MAMLAKA ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ipo katika hatua za mwisho za kuandaa na kupeleka muswada wa sheria bungeni mwaka huu itakayowawezesha kuanza kuwasajili watoto kuanzia umri wa mwaka 0 hadi 17.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Hadija Kombo alikiambia Kituo cha Televisheni cha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuwa muswada huo utakapopitishwa wataanza majaribio ya kuwasajili watoto katika wilaya tatu za Kilolo mkoani Iringa, Songwe mkoani Songwe na Kusini Unguja, Zanzibar.
Aliongeza kuwa kwa sasa sheria inayotumika ni ya mwaka 1986 iliyofanyiwa mapitio mwaka 2012 na kanuni zake zikarejewa mwaka 2014.
“Kwa sasa hivi sheria inayotumika katika usajili ni ile Sheria Namba 11 ya Mwaka 1986 ambayo ilifanyiwa mapitio mwaka 2012 na kanuni zake zikarejewa mwaka 2014. Kwa sasa tupo kwenye mchakato wa kubadilisha hiyo sheria kutoka kuruhusu usajili wa kuanzia miaka 18 na kuendelea ije iruhusu usajili wa watoto kuanzia mwaka 0 hadi 17,” aliongeza Hadija.
Aidha, alisema kwa ngazi ya NIDA imeshakamilisha taratibu zote za muswada huo na kuuwasilisha Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ambayo nayo imeshakamilisha sehemu yake na kuiwasilisha kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa hatua za mwisho na kuiwasilisha bungeni ili ipitishwe.
Alifafanua kuwa vitambulisho hivyo vitakuwa na umuhimu kwa watoto kwa sababu vitawasaidia kupata haki zao za msingi. Kwa sasa sheria ya vitambulisho vya taifa inasema Mtanzania anayestahili kusajiliwa na kupata kitambulisho cha taifa ni yule mwenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea.
