Mji wa Kipumbwi katika Wilaya ya Pangani, Mkoa wa Tanga, unazidi kukua, hii ni kutokana na mabadiliko ya kiuchumi na kijamii kupitia mradi wa kisasa wa viwanja vya biashara na makazi unaoratibiwa na Kampuni ya Makazi Solution.
Mradi huu unaendelea kuvutia sekta mbalimbali za uwekezaji, biashara, uvuvi, huduma za kijamii na utalii na kuibua matumaini makubwa kwa wakazi wa Pangani na mikoa jirani.
Kama inavyofahamika kuwa Tanga ni lango la uchumi Afrika Mashariki na Kipumbwi ndiyo kitovu muhimu cha lango hilo hii ni kutokana na uwepo wa Bandari ya Kipumbwi ambayo ni kitovu cha biashara kinachounganisha kisiwa cha Zanzibar na kupitia Bandari ya Mkokotoni kwa takribani kilometa 60 tu.
Viwanja vya Kipumbwi vina sifa nyingi zinazowafanya wawekezaji na wanunuzi kuviona kama fursa adhimu. Kwanza, eneo hili liko kando ya Bahari ya Hindi, likitoa mtazamo wa kuvutia na mandhari ya bahari kwa makazi ya kisasa.
Wavuvi wakiendelea na shughuli zao katika Mji wa Kipumbwi ambao upo kilomita 60 kutoka Bandari ya Mkokotoni, Zanzibar. Serikali inajenga soko kubwa la samaki na dagaa katika eneo hilo ili kuwasaidia wavuvi hao kuongeza thamani na kuboresha shughuli zao.
Pia, vina miundombinu ya msingi kama barabara zilizoimarishwa, umeme, maji na upatikanaji wa huduma za mawasiliano ya kisasa.
Huduma za kijamii zilizopo katika eneo hilo
Kipumbwi imejengwa kwa uzingatia mahitaji ya jamii. Huduma muhimu kama vituo vya afya, shule za msingi na sekondari zinapatikana ndani ya eneo hilo na kuwepo kwa vituo vya huduma za kijamii kunatoa urahisi kwa wananchi.
Miundombinu ya maji safi na usafi wa mazingira pia inaendelea kuboreshwa kwa kushirikiana na mamlaka za Serikali na sekta binafsi.
Ujenzi wa Barabara Mpya ya Lami ya Tanga-Pangani_Kipumbwi-Bagamoyo mpaka Dar es Salaam itaiunganisha Kipumbwi na kufungua fursa lukuki za kiuchumi kutokana na magari mengi kutumia njia hiyo inayofupisha safari ya Tanga- Dar es salaam kwa takribani kilometa 90.
Fursa za biashara na uchumi
Kipumbwi kuna fursa nyingi za kiuchumi. Kwanza ni uwepo soko la kimataifa la samaki na dagaa ambalo Serikali imeanza utekelezaji wake kwa gharama ya Sh 1.3 bilioni jambo ambalo litaongeza ufanisi kwa wavuvi na wafanyabiashara wa ndani pamoja na nchi jirani za Congo na Burundi wanaofuata samaki na dagaa katika mji wa Kipumbwi
Pia, kuna mpango wa ujenzi wa bandari ya kisasa ya Kipumbwi itakayosaidia kukuza shughuli za uvuvi na usafirishaji wa bidhaa baharini, kuvutia meli ndogo na kati za usafirishaji wa mizigo na abiria. Bandari hii itaifanya Kipumbwi kuwa daraja la biashara kati ya Tanzania Bara na visiwa vya Pemba na Zanzibar na eneo la Afrika Mashariki kwa ujumla.
Kwa kuwa Pangani ni kitovu cha biashara ya uvuvi, kilimo na usafirishaji, uwekezaji katika maeneo ya kuhifadhi na kusindika mazao ya baharini utaibua fursa za ajira kwa vijana na kuongeza mapato kwa wakazi wa eneo hilo.
Utalii na biashara: Fursa nyingine adhimu Kipumbwi
Kipumbwi ipo takribani kilometa 30 tu kutoka katika mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Saadan na Kilometa 60 mpaka wa Zanzibar. Kimkakati mji wa Kipumbwi unaweza kutumika kama malazi kwa watalii kutoka maeneo hayo. Aidha kupitia barabara mpya ya lami inayojengwa itaweza kusafirisha watalii kwenda Mlima Kilimanjaro, Dar es Salaam na maeneo mengine.
Aidha, Kipumbwi ina mandhari ya kuvutia ya Pwani, fukwe zenye mchanga mweupe, maji ya bahari yenye rangi ya buluu na utajiri wa utamaduni wa ukanda wa Pwani. Hii inalifanya kuwa kivutio kikubwa kwa watalii wa ndani na nje ya nchi.
Kwa kuwa Pangani ni mji wenye historia ndefu ya utamaduni wa Waswahili, huongeza mvuto wa utalii kwa watalii wanaopenda historia na urithi wa tamaduni mbalimbali za Pwani.
Aidha, uwekezaji katika utalii wa vijijini kama safari za mashambani, utembezi kwa miguu katika misitu ya pembezoni na ziara za kihistoria kunachochea shughuli za kibiashara kwa wakazi wa eneo hilo.
Fursa hizo za utalii zinapunguza utegemezi kwa sekta moja tu ya uvuvi na kuchochea uchumi wa mkoa mzima kwa kuleta wageni wengi wanaotumia huduma za hoteli, migahawa, maduka na safari za baharini.
Kauli ya Serikali
Serikali imeonyesha msimamo thabiti wa kuunga mkono miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Pangani na Mkoa wa Tanga kwa ujumla. Kwa mfano, ujenzi wa soko la kimataifa umekisiwa kuwa moja ya mikakati ya Serikali kuboresha kipato cha wakazi na kukuza sekta ya samaki nchini.
Serikali imesema soko hili litakuwa na manufaa makubwa kwa familia zaidi ya 10,000 zinazojihusisha na uvuvi na usindikaji wa samaki.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Pangani, Wakili Agape Fue anasema halmashauri hiyo kwa kushirikiana na kampuni Makazi Solution imefanya kazi kubwa ya kupima viwanja kwa ajili ya uwekezaji, makazi na biashara ambapo pia alielezea fursa nyingi zilizopo kwenye wilaya hiyo.
“Pangani ni wilaya yenye fursa nyingi za uwekezaji na biashara, ikiwemo soko la kisasa la samaki, hoteli na maeneo mengi ya utalii kama Kisiwa cha Maziwe, miundombinu bora ya kuingia na kutoka pamoja na boti za kisasa za utalii,” amesema Wakili Fue.
Fue ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kutoka ndani na nje ya Tanzania kwenda Pangani na kuahidi kuwa Serikali ipo tayari kushirikiana nao bega kwa bega.