
Maadhimisho ya kila mwaka yanaangazia fursa muhimu, saratani ya shingo ya kizazi husababisha zaidi ya vifo 350,000 kila mwaka, ilhali ni ugonjwa ambao tuna zana za kuutokomeza.
Siku hii inaunga mkono nguzo kuu za mkakati wa kimataifa wa WHO wa kutokomeza ugonjwa huo: chanjo ya 90% ya wasichana dhidi ya virusi vya papilloma (HPV), uchunguzi wa 70% ya wanawake, na matibabu ya 90% ya wale walio na vidonda vya kabla ya saratani na saratani iliyoendelea. Pia hutumika kama jukwaa muhimu kuimarisha utetezi, kuharakisha utoaji huduma, na kuhamasisha rasilimali ili kuhakikisha kila mwanamke na msichana anapata huduma za kuokoa maisha.
“Mnamo 2018, nilijivunia kuzindua wito wa kimataifa wa kutokomeza saratani ya shingo ya kizazi, na sasa ninajivunia hata zaidi kuona kile ambacho zamani kilionekana kama ndoto ya mbali kikigeuka kuwa ukweli, nchi nyingi zaidi zinapanua utoaji wa chanjo ya HPV, kuboresha uchunguzi, na kupanua matibabu, kutuleta karibu na siku zijazo zisizo na saratani ya shingo ya kizazi.” amesema Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa WHO.
Msukumo wa kimataifa wa kutokomeza saratani ya shingo ya kizazi unaongezeka, ukiungwa mkono na taarifa ya Gavi kwamba wamefikia lengo la kuwafikia wasichana milioni 86 kwa chanjo kufikia mwisho wa 2025. Hili linaonyesha hatua kubwa za nchi katika kupanua mipango ya chanjo, uchunguzi na matibabu.
Nchi mbalimbali zinaadhimisha siku hii kwa kuchukua hatua nyingi kwa pamoja. Sierra Leone na Liberia zinaendesha kampeni za chanjo kwa zaidi ya wasichana milioni 1.5, huku Sierra Leone pia ikifanya kampeni ya uchunguzi katika wilaya zake zote 16 na matembezi ya uhamasishaji. Nchini Malaysia, manusura wa saratani wanaongoza kampeni ya wiki moja ya kuhamasisha uchukuaji sampuli binafsi za HPV, mbinu muhimu inayopanua upatikanaji wa uchunguzi.
Hatua muhimu katika ngazi ya nchi ambazo zimeweka msingi madhubuti kwa maadhimisho haya mapya ya kila mwaka.
· Angola: Ilizindua kampeni ya chanjo ya HPV mwezi Oktoba kwa wasichana wenye umri wa miaka 9–12.
· China: Iliongeza chanjo ya HPV katika mpango wa taifa wa chanjo, ikiwawezesha wasichana wote wenye umri wa miaka 13 kupata chanjo.
· Cuba: Ilizindua chanjo ya HPV Oktoba 2025 kwa wasichana wote wa Darasa la 4.
· Ghana: Iliendesha kampeni ya kitaifa Oktoba 2025 kwa wasichana wa miaka 9–14, ikilenga kufikia wasichana milioni 2.4.
· Indonesia: Iliandaa mkutano wa pili wa kimataifa wa kutokomeza saratani ya shingo ya kizazi na kurudia kujitolea kwake kutokomeza ugonjwa huo kufikia 2030 kupitia malengo makubwa (90-75-90), ubia imara, na uwekezaji mkubwa katika chanjo, uchunguzi, na matibabu.
· Nepal: Iliendesha kampeni ya kitaifa Februari 2025 kwa wasichana wa miaka 10–14, ikianza rasmi kuingiza chanjo ya HPV katika ratiba ya kitaifa.
· Nigeria: Ilizindua jitihada za kitaifa za kutokomeza saratani ya shingo ya kizazi, huku Mke wa Rais, Seneta Oluremi Tinubu, akitoa dola 700,000 kupitia mpango wa “Renewed Hope Initiative”.
· Pakistan: Ilizindua chanjo ya kitaifa ya HPV kupitia kampeni iliyolenga wasichana milioni 9, kampeni kubwa zaidi kuwahi kufanywa na nchi yoyote.
· Rwanda: Kupitia “Mission 2027”, nchi inapanua upimaji na matibabu ili kufikia malengo ya 90-70-90 kufikia 2027—miaka mitatu kabla ya lengo la dunia.
· Spain: Kupitia AECID, inaunga mkono mpango wa WHO wa kutokomeza saratani ya shingo ya kizazi katika Afrika na Mediterania Mashariki.
· South Africa: Iliweka suala la kutokomeza saratani ya shingo ya kizazi katika ajenda ya G20, ikiendeleza uongozi wake na ikimalizia mfumo wa kitaifa wa mkakati wa kutokomeza ugonjwa huo.
· Tajikistan: Ilianza chanjo ya HPV kwa wasichana wa miaka 10–14 katika chanjo za kawaida kuanzia Oktoba 2025.
· Tunisia: Ilianzisha chanjo ya HPV Aprili 2025 kwa wasichana wa miaka 12.
Katika Kanda ya WHO ya Pasifiki ya Magharibi, Unitaid na WHO zimepanua ushirikiano kuimarisha upatikanaji wa uchunguzi na matibabu ya vidonda kabla ya saratani.
Nchi duniani kote zinaongeza kasi ya upatikanaji wa chanjo ya HPV, uchunguzi, na matibabu, zikisonga kuelekea malengo ya kimataifa ya 90-70-90.