Akizungumza jijini Nairobi jioni ya Jumapili, Türk amesema Sudan “imeangukia katika shimo la mateso makubwa yasiyoelezeka” kutokana na takribani miaka mitatu ya mapigano kati ya Jeshi la Sudan (SAF) na Rapid Support Forces (RSF). Ziara yake ilimfikisha Port Sudan, Dongola, pamoja na maeneo ya Ad Dabba na Merowe katika Jimbo la Kaskazini, ambako alikutana na wakimbizi wa ndani, viongozi wa jamii, wafanyakazi wa misaada, na maafisa wa serikali.

Türk amesema alishuhudia “ukatili usioelezeka” unaowakumba raia, lakini pia aliona uimara na mnepo wa jamii za Wasudan zinazojitahidi kuishi katikati ya vurugu, njaa na uhamaji wa lazima wa watu wengi.

Katika kambi ya Al Afad huko Ad Dabba, ambayo sasa inahifadhi takribani watu 20,000 waliokimbia kutoka El Fasher, Kaskazini mwa Darfur, Türk alikutana na watoto waliopata mshtuko wa kisaikolojia kutokana na mashambulizi ya mabomu. 

Alimtaja mtoto wa miaka minne aliyepoteza uwezo wa kusikia kwa sababu ya mashambulizi, na mtoto wa miaka mitatu ambaye “hakuweza kutabasamu.”

Pia amesimulia ushuhuda wa wanawake waliopitia ukatili wa kingono, vipigo na utekaji nyara walipokuwa wakikimbia kutoka El Fasher. Mwanamke mmoja kijana alieleza jinsi wanaume wenye silaha walivyomuua kaka yake, wakamteka nyara na kumbaka, na kumwacha akiwa na majeraha ya kisaikolojia na hofu ya kuwa mjamzito.

“Miili ya wanawake na wasichana imegeuzwa silaha ya vita,” amesema Türk, akisisitiza kuwa ukatili wa kingono unatumika kama silaha ya kivita. Ofisi yake imebaini visa vingi vya ukatili wa kingono unaohusiana na migogoro huko Darfur, hasa wakati wa mashambulizi ya RSF.

Alaani mashambulizi ya droni

Türk pia amelaani mashambulizi ya ndege zisizo na rubani kwenye Bwawa la Merowe na kituo cha kuzalisha umeme wa maji, ambacho hapo awali kilikuwa kikisambaza asilimia 70 ya umeme wa Sudan. Mashambulizi hayo yamesababisha kukatika kwa umeme katika hospitali, kusimamisha umwagiliaji wa mazao, na kuathiri upatikanaji wa maji safi, hali inayochochea magonjwa na njaa.

“Mashambulizi dhidi ya miundombinu muhimu ya kiraia ni ukiukwaji mkubwa wa sheria za kimataifa na yanaweza kuhesabiwa kama uhalifu wa kivita,” amesema, akizitaka RSF na SAF kusitisha mara moja mashambulizi dhidi ya masoko, hospitali, shule na makazi ya raia.

Kamishna Mkuu huyo ameonya kuwa ukatili kama ule uliofanyika wakati wa kuanguka kwa El Fasher unaweza kujirudia katika eneo la Kordofan, ambako mapigano yameongezeka. Ametaja mashambulizi makali ya mizinga, ndege zisizo na rubani na mashambulizi ya angani yanayosababisha uharibifu mkubwa, uhamaji wa watu, na kusambaratika kwa huduma muhimu katika maeneo kama Kadugli na Dilling, ambako tayari kuna hali ya njaa.

Watoto wanaingizwa vitani

Türk ameeleza wasiwasi mkubwa kuhusu kuongezeka kwa ulinzi wa kijeshi katika jamii ya Wasudan, ikiwa ni pamoja na kuajiri watoto na kuwapa raia silaha. Pia amekosoa kukamatwa kwa waandishi wa habari, wanasheria na wanaharakati wa kiraia kwa tuhuma za “kushirikiana” na pande pinzani, akisema vikwazo kwa vyombo vya habari vinachochea chuki na kuendeleza vita.

“Hakuna mtu mwenye akili timamu anayeweza kufikiri kuwa kuendelea na mapigano ndiyo suluhisho,” amesema Türk. “Fedha nyingi zinatumika kununua silaha badala ya kupunguza mateso ya wananchi.”

Amewataka wahusika wa kikanda na wa kimataifa, hasa wale wanaotoa silaha au kunufaika kiuchumi na vita, kutumia ushawishi wao kusaidia kumaliza mgogoro huo.

Kama hatua ya haraka, Türk ametoa wito wa kulindwa kwa raia, kuruhusiwa kwa njia salama kwa watu wanaokimbia maeneo ya vita, kuruhusu misaada ya kibinadamu kufika bila vikwazo, kutendewa kwa kibinadamu kwa waliokamatwa, na kuachiliwa kwa raia wanaozuiliwa bila sababu za kisheria.

Akikumbuka ziara yake ya mwisho ya Sudan mwaka 2022, Türk amesema matumaini ya mpito wa kidemokrasia yalivunjwa na vita. Amewataka wahusika wote kuweka mbele maslahi ya wananchi wa Sudan na kufanya haki za binadamu kuwa msingi wa mchakato wowote wa amani.

“Roho ya mapambano ya amani, haki na uhuru haijavunjika,” amesema. “Kwa ustahimilivu wa wananchi wa Sudan, amani ya kudumu ni ngumu lakini siyo haiwezekani.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *