
Siku moja baada ya shambulio katika eneo la Lusinga katika Hifadhi ya Taifa ya Upemba, kaskazini mwa Katanga nchini DRC, lililohusishwa na wanamgambo wa Mai-Mai, hali imerejea kuwa shwari. Jeshi limechukua udhibiti wa eneo hilo, ambalo linahifadhi huduma zote za hifadhi hiyo, na baadhi ya wafanyakazi wamerejea.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Na mwandishi wetu huko Lubumbashi, Denise Maheho
Kulingana na Taasisi ya Uhifadhi wa Mazingira ya Kongo, walinzi watano wa hifadhi hiyo waliuawa na vitu kadhaa viliibiwa na washambuliaji. Hifadhi ya Taifa ya Upemba imejaa wanyamapori wengi, wakiwemo pundamilia wa porini, nyati wa mwisho wa Katanga, na tembo.
Shambulio hilo lilianza yapata saa 10:00 alfajiri siku ya Jumanne na liliwashangaza walinzi waliokuwepo katika eneo hilo. Hasara ni kubwa: watu watano walifariki, kulingana na taarifa kutoka Taasisi ya Uhifadhi wa Mazingira ya Kongo (ICCN). Vyanzo vilivyo karibu na ICCN vinahusisha shambulio hilo na kundi la wanamgambo wa Mai-Mai kutoka vijiji jirani, haswa Kinja na Ngonga. Hili linaonekana kuwa kundi jipya ambalo kiongozi wake hajatambuliwa.
Vifaa kadhaa viliporwa na baadhi ya miundombinu ikaharibiwa, kulingana na ICCN. Vyanzo vingine vinaonyesha kwamba washambuliaji pia walishambulia ghala la silaha na risasi la walinzi wa mbuga, ambalo walilichoma moto baada ya kulipora.
Utulivu umerejea
Leo, utulivu umerejea katika eneo la Lusinga. Wafanyakazi wa kigeni wa mbuga hiyo, pamoja na mkurugenzi wake, Tina Lain, wako salama, ofisi ya mawasiliano ya mbuga hiyo inabainisha. Vyanzo vingine pia vinasema kwamba jeshi lilipata gari lililotelekezwa msituni lenye sehemu ya shehena ya silaha na risasi zilizoibwa.
Eneo linalozunguka Hifadhi ya Kitaifa ya Upemba limeshuhudia shughuli za wanamgambo kwa muongo mmoja. Mnamo mwaka 2004, eneo la Lusinga lilikumwa na shambulio baya. Mlinzi wa mbuga hiyo na wafanyakazi wengine wawili waliuawa na wanamgambo wa Mai-Mai walio wa Chifu Kyungu Mutanga Gédéon.