Wakati dunia inaadhimisha Siku ya Maji Duniani chini ya kaulimbiu “Maji na Jinsia,” bado inakabiliwa na changamoto ya uhaba wa maji unaothiri kwa kiasi kikubwa wanawake na wasichana na hilo limeonekana katika maeneo mengi ya Afrika Mashariki, hususan Tanzania vijijini.
Wanawake na wasichana hulazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji, mara nyingi kabla ya mapambazuko au baada ya jua kuzama.
Kwa kufanya hivyo, hujikuta wanalazimika kukosa masomo, kushindwa kushiriki katika shughuli za kiuchumi, na wakati mwingine hujiweka katika hatari ya kiafya na kiusalama.
Hivyo basi, upatikanaji wa maji si suala la uhai pekee, ni suala la usawa, fursa, usalama na utu wa binadamu. Mifumo ya maji inaposhindwa kufanya kazi, muda wa wanawake hupotea, elimu ya wasichana huathirika, na ustawi wa familia hudorora.
Lakini mifumo ya maji inapofanikiwa, wanawake hupata muda wa kushiriki katika shughuli za kiuchumi, uongozi na maendeleo ya jamii. Miundombinu ya maji inayozingatia jinsia ni hitaji la msingi la maendeleo.
Wanawake na upatikanaji wa maji
Nchini Tanzania, Waterforce Africa Ltd inaonyesha namna uhandisi wa maji unavyoweza kukabili changamoto hizi kwa makusudi.
Kampuni hii inayoongozwa na wazawa inaona upatikanaji wa maji si suala miundombinu tu, bali ni uwajibikaji wa kijamii, ujumuishi na uwezeshaji wa jamii.
Kwa kuzingatia uendelevu, matumizi ya wazawa kwenye miradi ya maji na mifumo jumuishi inayotambua jinsia, kampuni hii inaleta mageuzi namna jamii, taasisi na viwanda vinavyopata na kusimamia maji.
“Tukibuni mifumo ya maji na usafi wa mazingira, tunajiuliza swali rahisi tu! Nani anafaidika zaidi?” anasema Mkurugenzi Mtendaji wa Waterforce Africa Ltd, Shivanand Poojari.
“Ninaamini ukimwezesha mwanamke, umeiinua jamii nzima. Wanawake wanapowezeshwa kwenye eneo la usimamizi na upatikanaji wa maji, jamii nzima inanufaika kwa kuwa na afya, elimu na uzalishaji bora,” anasema Mkurugenzi huyo.
Kampuni imekuwa ikizingatia makundi ya aina yote, ikiendelea kukuza ujumuishi miongoni mwa wafanyakazi wao na usimamizi wa miradi mbalimbali, anaeleza Mkurugenzi.
Miradi ya Waterforce Africa Ltd imejengwa juu ya uhalisia wa mahitaji ya jamii. Visima virefu, pampu za maji zinazotumia nishati ya jua, matenki ya kuhifadhia maji na mitandao ya usambazaji hutengenezwa kimkakati karibu na makazi, shule na vituo vya afya ili kupunguza umbali wa kutafuta maji, anafafanua.
Vilevile, kulingana na Mkurugenzi huyo, miundombinu ya usafi wa mazingira imeundwa kwa kuzingatia faragha na heshima, hususan kwa wasichana balehe.
Hatua hizi hupunguza adha za kila siku za kutafuta maji, huboresha usafi na afya, na kuwapa muda zaidi kwa ajili ya masomo, biashara ndogondogo na malezi ya familia, anaongeza.
Zaidi ya miundombinu, anasema Waterforce Africa Ltd huziwezesha jamii kusimamia mifumo yao ya maji. Ushiriki wa wanawake katika kamati za maji huhamasishwa, na wanajamii hupatiwa mafunzo ya uendeshaji na matengenezo ya msingi.
“Wanawake wanaposhirikishwa katika maamuzi, mifumo hufanya kazi vizuri zaidi, jamii hustawi, na wasichana hubaki shuleni,” anaeleza Mkurugenzi Mtendaji.
Mtambo wa kutibu maji wenye uwezo wa kutibu lita 10,000 kwa saa, unaotumia teknolojia ya hali ya juu ya kuchuja maji (Nano Filtration), uliofungwa katika kampuni ya Irvine’s jijini Arusha.
Usambazaji maji kwenye viwanda na taasisi
Mbali na kuziwezesha kaya maskini kupata maji safi, anasema WaterForce imejipambanua katika kuimarisha sekta ya viwanda na taasisi nchini.
Kwenye Kiwanda cha Mtibwa Sugar Limited, kampuni ilibuni na kusanifu mfumo jumuishi wa kutibu maji wenye kifaa cha kusafisha maji (clarifier) chenye uwezo wa mita za ujazo 150 kwa saa, mfumo wa uchujaji maji (ultrafiltration) wa mita za ujazo 40 kwa saa, pamoja na mtambo wa usafishaji wa maji (Reverse Osmosis) wa mita za ujazo 30 kwa saa.
Mfumo huu ulidhibiti changamoto ya tope nyingi (turbidity) na kukidhi viwango vya juu vya uchemshaji maji, na hivyo kuboresha ufanisi wa utoaji mvuke, ubora wa kiutendaji na uzalishaji wa kiwandani kwa ujumla.
Pale Zanzibar, mtambo wa usafishaji maji (Reverse Osmosis) wenye uwezo wa mita za ujazo 20 kwa saa uliofungwa katika Kiwanda cha Ikraam Bottlers and Creamery Limited unahakikisha upatikanaji wa maji salama ya kunywa kwa matumizi ya umma na kusaidia sekta ya utalii, anabainisha Poojari.
Aidha, anasema Kule Kwala Industrial Park, Eneo la Hifadhi ya Viwanda la Sino–Tanzania, WaterForce Africa Ltd inaendelea na ufungaji wa mtambo wa kutibu majitaka wenye uwezo wa KLD 500, kuhakikisha usimamizi bora wa maji taka katika eneo hilo la viwanda, usafirishaji na biashara linalokua kwa kasi zaidi.
Anasema kuwa hatua hiyo inadhihirisha umuhimu wa kujumuisha miundombinu ya mazingira katika mipango ya ukuzaji wa sekta ya viwanda nchini.
Kujenga uhimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi
Mabadiliko ya tabianchi yanakwamisha dhamira ya dhati iliyonayo WaterForce kuwa uhalisia. Ukame, mvua zisizotabirika na changamoto za umeme vinatishia usalama wa maji Afrika Mashariki, anasema na kuongeza.
Hivyo, hivi sasa masuluhisho ya kampuni yamebuniwa kwa kuzingatia uimara na hii ni pamoja na uendelezaji wa maji ya chini ya ardhi kwa tafiti za kitaalamu za kijiolojia, matumizi ya pampu za nishati ya jua, teknolojia za urudishaji maji katika matumizi mapya na uchakati maji upya, pamoja na mifumo ya matibabu inayoweza kushughulikia ubora tofauti wa maji.
“Uhimilivu unamaanisha miundombinu inayofanya kazi hata katika miezi mikavu zaidi au wakati umeme unapokatika,” anasema Poojari. “Jamii na viwanda vinahitaji maji ya uhakika bila kujali hali ya hewa.”
Ahadi ya uendelevu na matumizi ya wazawa
Waterforce Africa Ltd, kulingana na Poojari, inajitofautisha kwa kutumia vipaji vinavyopatikana nchini, uwezo wa uzalishaji vifaa vyake yenyewe, utaalamu wa kihandisi, na uendelevu wa muda mrefu wa miradi ya maji.
Miradi haitekelezwi tu na kuachwa; huanzishwa rasmi, hufuatiliwa na kutunzwa. Waendeshaji wazawa hufundishwa namna sahihi ya kuisimamia ili kuhakikisha mifumo inaendelea kutoa huduma kwa muda mrefu baada ya kukamilika, anaeleza.
Ushirikiano na taasisi za serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali, waendelezaji wa viwanda na washirika wa kimataifa wa teknolojia ni chachu ya mafanikio ya miradi ya kampuni hiyo, hatua inayohakikisha inabakia kuwa imara kiufundi, ina thamani sawa ya fedha ya uwekezaji wake na jumuishi kwa jamii yote.
“Usalama wa maji ni usalama wa taifa,” anaongeza Mkurugenzi Mtendaji. “Tanzania ina vipaji vingi, teknolojia na uwezo wa sekta binafsi wa kutatua changamoto za maji, kinachohitajika ni ushirikiano na dhamira ya pamoja.”
Athari halisi, mabadiliko ya kudumu
Matokeo yanaonekana wazi. Jamii zilizokuwa zikitumia muda mwingi kutafuta maji sasa zinapata maji salama na ya uhakika karibu na makazi yao. Mahudhurio shuleni yanaongezeka, hususan kwa wasichana.
Wanawake sasa wanapata muda wa kushiriki katika shughuli za kiuchumi na uongozi. Afya za jamii zinaimarika, na viwanda vinafanya kazi kwa ufanisi zaidi bila kuharibu mazingira.
Katika Siku hii ya Maji Duniani, simulizi ya Waterforce Africa Ltd inaonesha uhusiano wa kina kati ya upatikanaji wa maji, usawa wa kijinsia na maendeleo ya kiuchumi.
Ikiwa kama mzalishaji halisi wa vifaa, kampuni hiyo inaamini kuwa Tanzania lazima iendelee kujenga uwezo wake wenyewe wa uhandisi wa miundombinu ya maji.
Lakini miundombinu pekee haitoshi, mifumo lazima iwe jumuishi, imara na isimamiwe kwa uendelevu.