Viongozi wa Afrika, wataalamu wa afya, watafiti na wawakilishi wa vijana wametoa wito wa hatua za haraka za kuingiza tiba asili katika mifumo ya kitaifa ya afya barani humo.

Wakizungumza katika Mkutano wa Kikanda wa Afya Duniani uliofanyika Nairobi Kenya kuanzia tarehe 29 Aprili mwaka huu washiriki wamesema tiba asili lazima iwe sehemu muhimu ya huduma za msingi za afya na utekelezaji wa huduma za afya kwa wote barani Afrika.

Kikao hicho cha ngazi ya juu kilichoitwa “Tiba Asilia kama Sehemu ya Suluhu: Kutafakari Upya Huduma za Msingi za Afya na Huduma za Afya kwa Wote Afrika” kiliungwa mkono na Kituo cha Kimataifa cha Tiba Asilia cha Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa Duniani WHO pamoja na Charité Competence Center kwa ajili ya Tiba Asili na Dawa Jumuishi cha Chuo Kikuu cha Charité Universitätsmedizin cha Berlin Ujerumani.

Wito wa kuhamia utekelezaji wa vitendo

Washiriki wamesisitiza umuhimu wa kuondoka katika majadiliano ya sera pekee na kuelekea katika utekelezaji wa hatua madhubuti zinazolingana na Mkakati wa Kimataifa wa Tiba Asili 2025–2034.

Wamesema tiba asili haipaswi kupewa tu utambuzi wa kisiasa, bali pia kuungwa mkono kwa fedha, mifumo ya udhibiti na kuingizwa rasmi katika mifumo ya afya ya serikali.

Akitoa hotuba kuu, Profesa Martins Emeje mjumbe wa kamati ya WHO amezitaka nchi za Afrika kuweka mkazo katika utekelezaji na uwajibikaji. Ameeleza kuwa mkakati huo mpya wa kimataifa unaweza kuwa mwongozo wa vitendo kwa muongo ujao.

“Mkakati wa Kimataifa wa Tiba Asili 2025–2034 unaweza kuwa kipimo cha utekelezaji na uwajibikaji,” amesema Profesa Emeje. “Juhudi za kuingiza tiba asili katika mifumo ya afya zitashindwa iwapo jamii za asili na makabila ya jadi hazitahusishwa kikamilifu katika kubuni suluhisho zinazozingatia hali halisi na lugha za jamii zao.”

Kulinda maarifa ya jadi na kuimarisha udhibiti

Washiriki pia wamesisitiza umuhimu wa kulinda mifumo ya maarifa ya jadi ya Afrika kupitia haki za umiliki wa kiakili, tafiti za kisayansi na mifumo madhubuti ya udhibiti. Wamesema mbinu zinazotegemea ushahidi wa kisayansi pamoja na ushirikiano kati ya serikali, watafiti na jamii zitakuwa muhimu katika kujenga imani na kuhakikisha usalama wa matumizi ya tiba asili.

Wawakilishi kutoka Shirika la Dawa Afrika (AMA) na taasisi za kitaaluma wameeleza kuwa tiba asili inaweza kusaidia kupanua upatikanaji wa huduma za afya, hasa katika maeneo ambayo huduma za kawaida za hospitali bado ni ghali au hazifiki kwa urahisi.

Wameongeza kuwa huduma za afya zinazotokana na jamii na kuzingatia tamaduni za wananchi zinaweza kusaidia kujenga mifumo imara ya afya na kupunguza gharama kwa mamilioni ya Waafrika.

Msukumo mpya baada ya ahadi za kimataifa

Majadiliano hayo mjini Nairobi yamejengwa juu ya msukumo uliotokana na Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa WHO kuhusu Tiba Asili, ambapo nchi mbalimbali zilitoa ahadi za kuimarisha ushirikiano, udhibiti na tafiti katika sekta hiyo. Washiriki wamesema Afrika sasa ina nafasi ya kuwa kinara duniani katika matumizi salama ya tiba asili yanayotegemea ushahidi wa kisayansi.

“Tiba asili, inapodhibitiwa kwa usalama na kuongozwa na jamii, inaweza kuwa njia muhimu ya kupanua huduma za afya na kujenga mifumo imara ya afya,” washiriki wamehitimisha, huku wakizitaka serikali kubadili ahadi kuwa mipango ya kitaifa yenye fedha na utekelezaji wa moja kwa moja kwa wananchi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *