Akizungumza mjini Bunia, mji mkuu wa Jimbo la Ituri na kitovu cha mlipuko huo, mashariki mwa nchi, Tedros amesema jamii za wenyeji lazima ziwe kiini cha mwitikio dhidi ya aina ya Ebola ya Bundibugyo, ambayo kwa sasa haina chanjo wala tiba iliyoidhinishwa.

“Hatujaja kuwaambia watu cha kufanya. Tupo hapa kusikiliza,” amesema katika mkutano na waandishi wa habari. “Jamii zinaelewa changamoto zao na suluhisho zao. Jukumu letu ni kuwaunga mkono katika kutekeleza suluhisho hizo kwa pamoja.”

© WHO/Joël Lumbala WHO linafanya kazi kukamilisha kituo cha afya ya umma ambacho kitashughulikia wagonjwa wanaoshukiwa au wamekubaliwa kuwa na ugonjwa wa virusi vya Ebola nchini DR Congo.

Mlipuko huo unaendelea kubadilika kwa kasi

Kufikia tarehe 27 Mei 2026, jumla ya wagonjwa 906 wanaoshukiwa kuwa wa Ebola na vifo 223 vinavyoshukiwa kuhusiana na ugonjwa huo vilikuwa vimeripotiwa nchini DRC. Katika DRC na Uganda kwa pamoja, visa 134 vilivyothibitishwa na vifo 18 vilivyothibitishwa vilikuwa vimeripotiwa kufikia tarehe 29 Mei. Aidha, raia mmoja wa Marekani ambaye alikuwa akiwatibu wagonjwa nchini DRC kwa sasa anapatiwa matibabu nchini Ujerumani.

Kujenga imani ya jamii

Tedros ametumia ziara yake kukutana na maafisa wa serikali, viongozi wa jamii, mashirika ya kibinadamu na washirika wa afya, akisisitiza kuwa imani ya wananchi na ushiriki wa jamii vitakuwa muhimu katika kukomesha maambukizi.

“Umiliki wa jamii ndiyo utakaokomesha mlipuko huu,” amesema.

Ameeleza matumaini ya kukutana na vikundi vya wanawake, viongozi wa dini, wawakilishi wa wafanyabiashara na vijana wakati wa ziara yake, akieleza kuwa kujenga imani ni mchakato unaoanza kwa kusikiliza.

WHO imeongeza juhudi za kushirikiana na mitandao ya kijamii ya ndani, ikiwemo viongozi wa jamii, vituo vya redio na watu wenye ushawishi katika mitandao ya kijamii, ili kupambana na taarifa potofu na kuhamasisha utambuzi wa mapema pamoja na matibabu.

Matibabu ya haraka ni muhimu

Mlipuko huu unasababishwa na virusi vya Bundibugyo, aina nadra ya Ebola iliyogunduliwa kwa mara ya kwanza nchini Uganda mwaka 2007.

Ingawa kwa sasa hakuna chanjo au tiba iliyoidhinishwa kwa aina hii ya virusi, Tedros amesisitiza kuwa wagonjwa wanaweza kupona iwapo watapata huduma bora za afya kwa wakati.

“Ebola inayosababishwa na virusi vya Bundibugyo inaweza kutibika kwa huduma nzuri za afya, na baadhi ya watu hapa Ituri tayari wamepona,” amesema. “Kutafuta matibabu mapema kunaleta tofauti kubwa.”

WHO na washirika wake pia wanaendelea na majaribio ya kitabibu yanayolenga kutengeneza chanjo na matibabu kwa aina hiyo ya virusi.

Kulinda huduma muhimu za afya

Wakati huo huo, juhudi za kukabiliana na mlipuko zinaendelea kuimarishwa.

WHO imewasilisha zaidi ya vifaa 2,000 vya uchunguzi wa maabara na kusaidia kuimarisha uwezo wa uchunguzi katika vituo muhimu vya usafiri. Shirika hilo pia linaimarisha mifumo ya maji katika vituo vya matibabu ya Ebola ili kusaidia kuzuia na kudhibiti maambukizi.

Hata hivyo, kuna wasiwasi mkubwa kuwa mlipuko huo unaweza kuvuruga huduma nyingine muhimu za afya katika maeneo yaliyoathirika.

Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ya Uzazi, UNFPA, limesema vituo vya afya vinaendelea kuelekeza wafanyakazi, vifaa na miundombinu katika shughuli za kukabiliana na Ebola, jambo ambalo limepunguza upatikanaji wa huduma kama upasuaji wa dharura wa kujifungua, huduma za watoto wachanga, uzazi wa mpango na huduma za baada ya kujifungua.

Ili kusaidia kuendelea kwa huduma hizo, UNFPA inapeleka wakunga, vifaa vya afya ya uzazi na vifaa tiba huku ikiunga mkono mpango wa kikanda wa mwitikio unaozihusisha DRC, Uganda na South Sudan.

‘Tupo hapa pamoja nanyi’

Tedros amesema mwitikio huo lazima uende zaidi ya kukabiliana na mlipuko wa sasa pekee.

“Tunapopambana na mlipuko huu pamoja nanyi, tumejizatiti kuhakikisha kuwa huduma nyingine muhimu za afya na misaada ya kibinadamu zinaendelea kutolewa kwa jamii za Ituri na maeneo mengine,” amesema.

Pia Ameeleza imani yake kuwa mlipuko huo unaweza kudhibitiwa.

“DRC imekabiliwa na Ebola mara 16 hapo awali na imefanikiwa kukomesha kila mlipuko,” amesema. “Huu ni wa 17. Historia hiyo inanipa matumaini makubwa.”

Akihitimisha hotuba yake, Tedros alitaka kuwapa matumaini wananchi walioathirika.

“Hamko peke yenu katika hili,” amesema. “Tupo hapa, tuko pamoja nanyi, na tutalivuka jambo hili kwa pamoja.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *