Wachezaji wa Senegal

Chanzo cha picha, Getty Images

Iliyochapishwa

Muda wa kusoma: Dakika 6

Haikupaswa kutokea hivi.

Senegal iliingia katika Kombe lao la Dunia la nne ikiwa na dhamira ya kufika mbali zaidi kuliko mwaka 2002, walipofika hatua ya robo fainali katika ushiriki wao wa kwanza kwenye mashindano hayo.

Hata hivyo, bado hawajapata hata alama moja baada ya mechi mbili na kuna uwezekano mkubwa wa kuondolewa katika hatua ya kwanza. Wanalazimika kabisa kuifunga Iraq siku ya Ijumaa ili kubaki na matumaini yoyote ya kufuzu kwenda hatua ya timu 32 bora.

Mwanzo wa Senegal katika Kombe la Dunia umefunikwa na msururu wa matatizo ndani ya timu.

Migogoro kuhusu marupurupu na malipo, mabadiliko ya mpishi yaliyofanywa dakika za mwisho, pamoja na malalamiko kuhusu chakula, vilitawala kipindi cha maandalizi kabla ya mechi za kwanza.

Zaidi ya hayo, utata unaohusu mkataba wa kocha Pape Thiaw pia umeibua wasiwasi kuhusu athari ambazo matatizo ya nje ya uwanja yanaweza kuathiri timu uwanjani.

Hivyo basi, nini hasa kinaendelea?

“Kuna dosari kadhaa”

Wachezaji na benchi la ufundi wanaishi katika hoteli ya nyota nne ya Hyatt Regency iliyoko New Brunswick, New Jersey, tofauti na hoteli ya kifahari ya nyota tano ya Fairmont Palace mjini Tangier, ambayo ilitumika wakati wa Kombe la Mataifa ya Afrika 2025 nchini Morocco.

Hata hivyo, hili si tatizo kubwa sana, hasa kwa kuwa hoteli hiyo iko karibu na kituo cha mazoezi cha Senegal katika Chuo Kikuu cha Rutgers.

Kumekuwa na uvumi kuhusu ubora wa chakula, huku baadhi wakidai kwamba hakikukidhi matarajio ya wachezaji.

Timu ilisafiri ikiwa na mpishi wake mkuu, yuleyule aliyeshiriki katika mashindano yaliyopita na ambaye alikuwa akiandaa chakula miezi kadhaa mapema kwa ajili ya kambi za mazoezi na mashindano.

Alibaki na timu hadi baada ya mechi ya pili ya kirafiki ya maandalizi ya Kombe la Dunia, Senegal ilicheza mechi za kirafiki dhidi ya Marekani mjini Charlotte na Saudi Arabia mjini San Antonio, kabla ya kuondoka kutokana na sababu binafsi.

Nafasi yake ilichukuliwa na mpishi mwingine, na wachezaji hawana malalamiko yoyote kuhusu huduma ya chakula.

Hata hivyo, malalamiko yanatoka kwa baadhi ya wajumbe wengine wa msafara, si kutoka kwa wachezaji wala benchi la ufundi.

Hawa walikuwa watu ambao hawakuwa sehemu ya kikosi kikuu lakini walikuwa wakikaa katika hoteli hiyo. Wakati mwingine walikwenda kuagiza chakula sehemu nyingine kwa sababu walikatishwa tamaa kutokukuta vyakula vya Kisenegal kwenye orodha ya vyakula.

Baadhi ya viongozi wa Shirikisho la Soka la Senegal (FSF) waliwasafirisha baadhi ya wanafamilia wao kwa gharama zao wenyewe, lakini waliwapangia malazi karibu na hoteli rasmi ya timu.

Wakati mwingine walijikuta wakiwa karibu sana na timu, jambo ambalo halikupokelewa vizuri na kila mtu.

Familia za wachezaji zimehifadhiwa katika hoteli nyingine iliyo karibu, huku gharama za malazi na kifungua kinywa zikilipiwa na shirikisho.

Wachezaji na benchi la ufundi pia hawakuridhishwa na kuchelewa kulipwa marupurupu yao.

Hata hivyo, fedha hizo hatimaye zililipwa na serikali siku chache zilizopita.

“Ni kweli kwamba kumekuwa na kasoro kadhaa, lakini kwa upande wa wachezaji, benchi la ufundi na Shirikisho, sote tumeelekeza nguvu zetu kwenye mechi ya kesho, na hilo ndilo jambo muhimu zaidi,” alisema Thiaw Jumapili.

Senegal, inayoshika nafasi ya 17 duniani, iliingia kwenye mashindano haya ikiwa moja ya matumaini makubwa ya Afrika, licha ya kupoteza ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika 2025, ubingwa ambao bado inaweza kuurejesha kupitia rufaa.

Badala yake, sasa inalazimika kufidia mwanzo mbaya baada ya kufungwa mabao 3-1 na Ufaransa na 3-2 na Norway.

“Wachezaji hawahitaji msukosuko wote huu,” alisema mshambuliaji wa zamani wa Senegal, El Hadji Diouf, katika mahojiano na RTS Senegal.

Mazungumzo kuhusu mkataba “yamechukua muda mrefu sana”

“Nikikosa hata kwa sekunde moja imani kwamba ninaweza kushinda Kombe la Dunia pamoja na Senegal, nitajiuzulu,” alisema Pape Thiaw katika mkesha wa kuanza kwa mashindano.

Thiaw, ambaye aliichezea Senegal katika Kombe la Dunia la 2002, aliiongoza timu kufika fainali ile yenye utata ya Kombe la Mataifa ya Afrika 2025 (AFCON) mwezi Januari.

Hata hivyo, uhusiano kati ya Thiaw na Shirikisho la Soka la Senegal haukuwa mzuri kama ulivyoonekana kwa nje.

Alipoanza kazi yake mwaka 2024, Thiaw alikubali mshahara aliotolewa, ambao ulikuwa takriban pauni 210,000 kwa mwaka.

Lakini baada ya mafanikio yake katika AFCON 2025, hadhi yake iliongezeka, jambo lililompa nguvu zaidi katika mazungumzo ya kuongeza muda wa mkataba wake, hasa kwa kuwa mkataba wake wa awali ulikuwa umeisha mara tu baada ya mashindano hayo.

Mazungumzo kuhusu kuongeza muda wa mkataba wake yaliendelea kwa muda mrefu kuliko ilivyotarajiwa.

Nchini Senegal, kocha hufanya mazungumzo ya mkataba na shirikisho ambalo ndiye mwajiri wake wa moja kwa moja. Hata hivyo, kutiwa saini kwa mkataba huo na malipo yake lazima yaidhinishwe na Serikali kupitia wizara zinazohusika na michezo na fedha.

Baada ya miezi kadhaa ya kuchelewa, Thiaw alilazimika kusafiri kwenda Marekani bila kuwa amesaini mkataba wake mpya.

Hali hiyo ilitokea katika mazingira ya kisiasa yaliyokuwa na misukosuko, ambapo Senegal ilipitia kipindi kirefu cha mabadiliko baada ya serikali kuvunjwa na Waziri Mkuu kuondolewa madarakani.

Kwa kawaida, hali hiyo ya kisiasa iliathiri pia sekta nyingine.

Baada ya watu wa karibu na Thiaw kuongeza shinikizo kupitia vyombo vya habari na kuweka wazi kwamba huenda angekataa kupanda ndege kuelekea Marekani, Rais wa Senegal, Bassirou Diomaye Faye, aliingilia kati binafsi.

Alizungumza moja kwa moja na Thiaw na kumhakikishia kuwa suala hilo litatatuliwa haraka iwezekanavyo.

Baada ya kuapishwa, Waziri mpya wa Michezo, Djireye Clotilde Coly, alisafiri kwenda Marekani kuhudhuria mechi ya kwanza dhidi ya Ufaransa, kukutana na timu na kuthibitisha ahadi zilizokuwa zimetolewa kwa Thiaw.

Baadaye mazungumzo yalipiga hatua, na hatimaye pande zote zikafikia makubaliano ya mkataba mpya wenye thamani ya pauni 480,000 kwa mwaka, pamoja na bonasi ya kila mwaka ya pauni 80,000.

Siku ya Jumapili, Thiaw alisema:

“Ni kweli kwamba ilichukua muda mrefu sana, lakini haikuwa suala la fedha. Lilikuwa zaidi suala la misingi na heshima, lakini sasa limekwisha kutatuliwa.”

“Kama Msenegal, uzalendo unatangulia kila kitu. Masuala yanayohusu mkataba sasa ni historia. Mkataba umesainiwa.”

Thiaw

Chanzo cha picha, Getty Images

“Tulihitaji kurekebisha kasoro chache”

Alipoulizwa Jumapili kuhusu matatizo yaliyokuwapo ndani ya kambi ya timu, Pape Thiaw alisema:

“Ni kweli kwamba kumekuwa na misuguano kadhaa ambayo inahitaji kutatuliwa.”

Alipoulizwa kuhusu kile kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia, mlinda lango Mory Diaw, ambaye alihudhuria mkutano na waandishi wa habari pamoja na Thiaw, alisema:

“Haya yote ni masuala yanayoshughulikiwa ndani ya timu.”

“Sidhani kama ni lazima mjue kila tunachozungumza ndani ya timu. Tuna kundi la wachezaji wenye weledi.”

“Tuko hapa kuiwakilisha nchi yetu. Hakuna kitakachotuvuruga katika kufanikisha lengo letu la pamoja.”

Babacar Diarra, mwandishi wa habari wa Canal+ ambaye ameifuatilia timu hiyo kwa zaidi ya miaka kumi, aliiambia BBC Sport:

“Senegal haijapitia hali ya aina hii kwa muda mrefu.”

“Inawezekana tulishawahi kuwa katika hali kama hii hapo awali, lakini haikuripotiwa kwenye vyombo vya habari.”

“Sidhani kwamba hali hii itawaathiri wachezaji au timu. Wataendelea kuwa makini na mashindano.”

“Hainishangazi kabisa. Ingawa walifika fainali ya AFCON na kila kitu kilionekana kwenda vizuri, hali halisi haikuwa nzuri kama ilivyoonekana.”

BBC Sport imeliwasiliana na Shirikisho la Soka la Senegal (FSF) ili kupata maoni yao kuhusu suala hilo.

Idadi ndogo ya tiketi

Nchini Senegal, kuna utamaduni ambapo katika kila mashindano makubwa, Serikali hulipia gharama za usafiri, malazi na tiketi za mechi kwa makundi makuu ya mashabiki.

Hata hivyo, katika Kombe hili la Dunia, Senegal inakabiliwa na vikwazo vinavyowazuia mashabiki hao kusafiri kwenda mashindano hayo.

Wasenegal hasa wanaoishi Marekani na Canada, walitarajia kunufaika na hali hiyo.

Hata hivyo, walipata tiketi 400 pekee, na ugawaji huo haukupokelewa vizuri na wengi, ambao walilalamikia ukosefu wa uwazi na idadi ndogo ya tiketi zilizotolewa.

Wajumbe wa vyama vya kitaifa vya Senegal walikusanyika Jumapili mbele ya hoteli ya timu kueleza malalamiko yao.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *