
Asilimia 50 ya wanaoambukizwa Ebola hufariki dunia
Ebola ni mojawapo ya magonjwa hatari zaidi duniani, ambapo takriban nusu ya watu wanaoambukizwa hufariki dunia. Ebola aina ya Bundibugyo iliyosababisha mlipuko wa 17 Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, (DRC) halikadhalika nchini Uganda haina chanjo wala matibabu yaliyoidhinishwa. Wanawake na wasichana wanaunda sehemu kubwa ya wagonjwa waliothibitishwa mtindo ambao umekuwa ukijirudia tangu mlipuko wa kwanza wa Ebola mwaka 1976. Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni za shirika la Umoja wa Mataifa la Afya duniani, WHO, katika mlipuko wa sasa wanawake ni zaidi ya asilimia 53 ya wagonjwa waliothibitishwa kwa vipimo vya maabara.
Hii haitokani na sababu za kibaiolojia, bali inahusiana na majukumu ya ulezi, ukaribu wa kijamii, na athari zinazotokea pale mifumo ya afya inapoporomoka. Maelezo haya yanaangazia upande uliofichika wa hadithi hiyo—kile kinachowakumba wanawake wakati Ebola inapoathiri jamii, kuanzia ujauzito hadi hatua za uokoaji.
Ebola ni nini?
Ebola ni ugonjwa unaobebwa na virusi vinavyosababisha maradhi makali — na mara nyingi husababisha vifo. Takriban nusu ya watu wanaoambukizwa ugonjwa huu hupoteza maisha.
Ingawa wanawake hawako katika hatari kubwa zaidi kibayolojia, wana uwezekano mkubwa zaidi kuliko wanaume wa kuambukizwa Ebola.
Kwa nini wanawake na si wanaume walio hatarini zaidi?
Sababu kuu ni kwamba wanawake duniani kote hubeba sehemu kubwa ya majukumu ya utunzaji ndani ya familia na jamii. Ugonjwa huenea kupitia misururu ya huduma za malezi, kazi za nyumbani, majukumu ya afya ya mstari wa mbele, na mila za mazishi.
Kwa kifupi, watu wanapokuwa wagonjwa nyumbani, mara nyingi ni wanawake wanaowahudumia kama mama, dada, wenza, shangazi na binti, au kama wauguzi na wafanyakazi wa usafi katika wodi za hospitali, pamoja na wakunga wanaowasaidia wanawake kujifungua.
Wanawake pia ndio wanaowahudumia wapendwa wao baada ya kifo, wakiandaa miili kwa ajili ya mazishi. Majukumu haya huwaweka wanawake katika mgusano wa karibu wa kimwili wakati wa hatua za kuambukiza za ugonjwa.
Takwimu zimeweka bayana
Historia inaonesha jinsi Ebola ilivyoathiri zaidi wanawake na wasichana katika milipuko ya awali. Wakati wa mlipuko wa Ebola wa 2018–2019 katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), wanawake na wasichana walikuwa takriban theluthi mbili ya wagonjwa walioripotiwa.
Nchini Liberia mwaka 2014, katika baadhi ya jamii, wanawake walihusisha hadi robo tatu ya vifo vya Ebola. Na takriban miaka 50 iliyopita katika DRC, wanawake walihusisha asilimia 56 ya vifo vilivyoripotiwa.
Takwimu za awali zinaonesha kwamba katika mlipuko wa sasa nchini DRC na Uganda, wanawake na wasichana wanachangia asilimia 53.4 ya visa vilivyothibitishwa maabara ambapo taarifa za kijinsia zinapatikana. Miongoni mwa vijana balehe, wasichana wanachangia zaidi ya asilimia 61 ya visa.
Nini hutokea kwa wanawake wajawazito wanaopata Ebola?
Mwanamke mjamzito akiambukizwa ebola ana nafasi ya karibu asilimia 100 ya kupoteza mtoto wake ambaye hajazaliwa. Mama pia yuko katika hatari kubwa zaidi ya kifo iwapo atapata ugonjwa huo kutokana na hatari ya kuvuja damu kwa kiasi kikubwa.
Lakini kuna upande mwingine wa hatari ambazo wanawake wajawazito wanakabiliana nazo hatari iliyoongezeka ya kupatwa na ugonjwa na hofu inayohusiana nayo. Wanawake wajawazito wana mguso wa mara kwa mara zaidi na huduma za afya.
Kwa hofu, wanawake wanaweza kukosa uchunguzi wa kawaida, au wanaweza kubaki nyumbani kujifungua badala ya katika kituo cha afya, jambo ambalo linamaanisha wanaweza kukosa matatizo yanayoweza kutibiwa ambayo yanaweza kutokea wakati wa ujauzito au wakati wa kujifungua.
Je, wanawake na wasichana wako katika hatari kubwa ya kukumbwa na vurugu wakati wa mlipuko wa Ebola?
Dharura za afya ya umma, kuanzia milipuko ya Ebola hadi janga la coronavirus“>COVID-19, zimehusishwa na ongezeko la matukio ya ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.
Hatua za karantini na vizuizi vya kusalia nyumbani zinaweza kuwanasa wanawake katika mazingira ya nyumbani pamoja na wanyanyasaji wao, huku zikikatiza uwezo wao wa kufikia marafiki, huduma muhimu, na mitandao ya msaada ambayo wangetegemea katika hali ya kawaida.
Milipuko mikubwa ya magonjwa pia huharibu upatikanaji wa huduma za afya ambazo mara nyingi tayari zimeelemewa. Hali hii inaweza kuwafanya waathirika wa ukatili kushindwa kupata huduma za matibabu wanazohitaji au hata kuripoti matukio ya unyanyasaji.
Aidha, dharura hizi huongeza changamoto za kiuchumi, ukosefu wa uhakika wa chakula, na viwango vya msongo wa mawazo ndani ya kaya. Mchanganyiko huu huweza kuzidisha migogoro ya madaraka na kuongeza uwezekano wa tabia za ukatili.
Hatari ya kuongezeka kwa ukatili dhidi ya wanawake na wasichana wakati wa milipuko ya magonjwa mara nyingi hubaki fiche kwa umma. Kwa sababu hiyo, mipango yote ya kukabiliana na dharura inapaswa kutambua wazi hatari hii na kuijumuisha katika hatua za mwitikio na ulinzi.
Je, kuna hatari nyingine zozote ambazo wanawake na wasichana wanakabiliana nazo wakati wa milipuko ya magonjwa?
Tunajua kwamba dharura za afya ya umma zinazidisha kutokuwepo kwa usawa kuliko kuwepo kwa wanawake na wasichana iwapo tayari walikuwa wakithaminiwa kidogo, walikuwa na madaraka yasiyo sawa katika kufanya maamuzi na uhuru mdogo, kwa mfano, mienendo hii ya madaraka isiyo sawa mara nyingi inazidishwa wakati wa majanga.
Mbali na hatari iliyoongezeka ya vurugu, wanawake wana uwezekano mkubwa zaidi wa kuhangaika kifedha kutokana na vizuizi vinavyopunguza uwezo wao wa kuzalisha mapato wakati wa mlipuko wa ugonjwa kama Ebola. Hili ni hatari hasa kwa wafanyabiashara wa sokoni ambao wanaweza kutegemea biashara ya mipakani na wanawake wanaoendesha biashara ndogo.
Wanawake na wasichana pia wana ugumu zaidi wa kufikia huduma muhimu. Hofu, unyanyapaa, vizuizi vya kuhama, na huduma zilizopungua zinaweza kuwazuia wanawake na wasichana kutafuta huduma wanayohitaji. Zaidi ya hili, mifumo ya afya mara nyingi imeelemewa au kuvurugwa, jambo linalofanya kuwa vigumu zaidi kupata huduma ya afya ya uzazi.
Mlipuko wa sasa nchini DRC unatokea ndani ya janga kubwa la kibinadamu. Katika maeneo yaliyoathiriwa na Ebola, takriban watu milioni 1.87 wanakabiliwa na viwango vikali vya njaa. Wanawake ndio walezi wakuu na watoaji wakuu wa chakula katika kaya nyingi. Wako chini ya shinikizo kubwa zaidi kutokana na vizuizi vya kuhama ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa, kuvurugika kwa masoko, na majukumu ya utunzaji huku wanafamilia wakiugua.
UN Women inafanya nini kudhibiti kuenea kwa Ebola?
UN Women inafanya kazi nchini DRC, ambako tayari kulikuwapo na janga kubwa la kibinadamu kabla ya mlipuko huo, na pia nchini Uganda, kwa kushirikiana na serikali za kitaifa na za mitaa, mfumo wa Umoja wa Mataifa, na mashirika ya wanawake ili kusaidia kudhibiti kuenea kwa Ebola.
Programu za kibinadamu huhakikisha kuwa taarifa za afya ya umma, vifaa vya elimu, na kampeni za uhamasishaji wa jamii zinalenga na kuwafikia wanawake na wasichana katika jamii zilizoathirika zaidi.
Pia hutoa ufadhili kwa mashirika ya kiraia yanayoongozwa na wanawake ambayo yana ufikiaji wa moja kwa moja na wa kuaminika kwa wanawake, wasichana, na jamii kwa ujumla. Katika kipindi ambacho takriban asilimia 90 ya mashirika yanayoongozwa na wanawake yanaripoti kuvurugika kwa shughuli zao kutokana na upungufu wa ufadhili wa kimataifa, msaada huu huwa wa kuokoa maisha.
Zaidi ya hayo, UN Women hukusanya na kutetea matumizi ya takwimu zilizochambuliwa kijinsia, ili kuhakikisha kuwa mwitikio wa Ebola unaongozwa na kuzingatia mahitaji mahususi ya wanawake na wasichana. Bila data kuhusu uzoefu na mahitaji ya wanawake, sera na huduma huwa na ufanisi mdogo katika kudhibiti au kuzuia ugonjwa.
UN Women pia inafanya kazi ndani ya mfumo wa Umoja wa Mataifa kuendeleza “mwitikio unaozingatia jinsia,” yaani kuhakikisha kuwa programu na mipango ya Umoja wa Mataifa katika kukabiliana na mlipuko inazingatia mahitaji na uwezo wa wanawake na wasichana. Hii inahakikisha wanawake wanaonekana, wanahusishwa, na wanasikilizwa katika vikao vya uratibu na maamuzi, ikiwemo kuongoza kwa pamoja Kundi la Jinsia katika Hatua za Kibinadamu.