- Mtoto wa kiume mwenye umri wa siku sita aitwaye Levi Baraka alipatikana ametekelezwa katika Eden Village, eneo la Kiamunyi, Nakuru, tarehe 28 Juni 2026
- Mama wa mtoto huyo aliacha barua iliyoandikwa kwa mkono akieleza kuwa hakuwa na makazi, alikuwa yatima, na baba wa mtoto alimfukuza baada ya kukataa mimba hiyo
- Msamaria mwema kutoka Nakuru alishiriki kisa hicho mtandaoni na kuthibitisha kuwa mtoto huyo yuko salama, jambo lililowagusa hisia Wakenya wengi
Mtoto mchanga wa kiume alipatikana ametekelezwa katika Kaunti ya Nakuru tarehe 28 Juni 2026, akiwa amewekewa pembeni barua iliyoandikwa kwa mkono iliyofichua hali ya kukata tamaa ya mama yake pamoja na ombi la kuhakikisha mwanawe anakuwa salama.

Source: Facebook
Mtoto huyo, aliyepewa jina la Levi Baraka na kukadiriwa kuwa na umri wa siku sita wakati alipopatikana, alipatikana akiwa hai katika Eden Village, Kitengo cha Ngata, Eneo la Kiamunyi, Kitongoji cha Mercy Njeri, ndani ya Kaunti Ndogo ya Rongai. Alizaliwa tarehe 22 Juni 2026.
Barua ya mama wa Nakuru iliyowagusa Wakenya
Barua ambayo mama huyo aliacha iliandikwa kwa Kiingereza fasaha na kwa utulivu, ikielezea maisha ya taabu aliyokuwa akipitia.
Alijieleza kuwa ni yatima asiye na ndugu wala jamaa wa kumtegemea, hana makazi na alitelekezwa na baba wa mtoto ambaye, kwa mujibu wake, alikataa mimba hiyo na kuwafukuza wote wawili.
“Samahani kwa kile nilichofanya kama mama, lakini sikuwa na chaguo, kwa kuwa sina makazi na ninahangaika kuimarisha maisha yangu. Ningependa kumbaki naye, lakini sina njia yoyote ya kujikimu.”
Aliendelea kueleza kuwa anatamani Levi apate makazi yenye upendo ya watoto au familia ya kumlea, na akamwomba yeyote atakayempata amsamehe.
Jambo lililogusa zaidi ni pale alipofichua kuwa alianza kuwa na mawazo ya kujiua, ingawa alisisitiza kuwa hakutaka mwanawe apatwe na madhara yoyote.
“Afadhali nisiwe na makazi peke yangu kuliko kuwa naye. Mawazo ya kujiua yalinizidia, lakini afadhali nife peke yangu kuliko kufa pamoja naye.”
Msamaria mwema wa Kenya aingilia kati
Nkatha, mwanzilishi wa shirika lisilo la kiserikali la Frolics of Hope Africa, alishiriki kisa hicho kupitia Facebook tarehe 2 Julai, akitoa wito kwa umma kusaidia kumpata mama huyo na kuhakikisha ustawi wa mtoto.
Baadaye alithibitisha kuwa mtoto Baraka alikuwa amepatikana na yuko salama.
Shirika la Frolics of Hope Africa linaweza kupatikana kupitia nambari 0707 825 250 kwa yeyote mwenye taarifa kuhusu mama huyo au anayependa kutoa msaada.
Wakenya walivyoitikia
Chapisho hilo lilizua hisia kali, huku wengi wakitaka mama huyo naye apewe msaada.
@Star Maweu:
“Laiti mchakato wa kuasili watoto ungekuwa rahisi; ningemchukua mtoto huyu.”
@Waithera Ratemo:
“Hapa ndipo uchunguzi wa kitaalamu wa kisayansi (forensic analysis) unapohitajika, ingawa utachukua muda. Unaweza kujua kuhusu mwanamke huyo kupitia mwandiko wake, lakini pia alikuwa na sababu zake za kumwacha mtoto. Angalau mtoto yuko hai na salama.”
@Nita Si:
“Mama huyu anampenda mtoto wake, ndiyo maana alibeba ujauzito hadi mwisho. Mungu amsaidie popote alipo….”
@Lilian Motanya:
“Yeye ni mama mzuri, tena anaandika vizuri sana. Ninaomba maisha yamtendee vyema. Naomba apate kazi au kitu kitakachomwezesha kupata chakula.”
@Waithaka Mfalme:
“Kiingereza chake kimeandikwa vizuri sana. Nina uhakika ameelimika kiasi. Ajitokeze.”
Mtoto wa Tharaka Nithi aokolewa
Katika habari nyingine, TUKO ilichapisha maelezo kuhusu uokoaji wa kusikitisha wa mtoto mwenye umri wa wiki moja aliyepatikana ametekelezwa katika shamba la mahindi katika Kaunti ya Tharaka Nithi.

Pia soma
Davis Lichuma: Familia yazungumza kwa uchungu baada ya mwanaharakati kupatikana lakini hajitambui
Tukio hilo la kuhuzunisha limezua mjadala wa kitaifa kuhusu changamoto zinazowakabili akina mama, hasa hali ya huzuni ya baada ya kujifungua (postpartum depression), huku wengi wakitaka jamii kuwaonyesha huruma mama huyo pamoja na kutoa wito wa haki kutendeka.
Read ENGLISH VERSION
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.
Chanzo: TUKO.co.ke

