Msemaji wa harakati ya Muqawama ya Jihad Islami ya Palestina amesisitiza kuhusu “matamanio matukufu” ya Kiongozi Shahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Seyyed Ali Khamenei, akisema kuwa nguvu ya Mhimili wa Muqawama inatokana na kujitolea kwake maishani.

Mohammad al-Hajj Musa ameyasema hayo akiwa mjini Tehran, na kuongeza kuwa kuchanganyika kwa damu ya viongozi wa Mhimili wa Muqawama na damu ya wapiganaji wa Palestina ni dhihirisho la umoja wa vita na hatima ya pamoja katika kukabiliana na adui mmoja.

Amesisitiza kuwa: “Damu ya hayati Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Seyyed Ali Khamenei, imechanganyika na damu ya wapiganaji wa Palestina katika vita moja” dhidi ya utawala haramu wa Israel.”

Hajj Musa amebainisha kuwa Ayatullah Khamenei alikuwa na ahadi thabiti katika mapambano yaliyolenga ukombozi wa Palestina, na alikuwa nguzo ya msingi katika kuunga mkono taifa la Palestina kwa miongo kadhaa, akitoa msaada mkubwa wa kijeshi, kilojistiki, na kisiasa katika mwelekeo huo.

Ofisa huyo mwandamizi wa Jihad Islami amesema “Kiongozi Shahidi alionyesha uongozi wa maono na wa kipekee, na alikuwa mtetezi thabiti wa mamlaka ya Ummah wa Kiislamu dhidi ya mipango ya kidhalimu na ya kibeberu.”

Hajj Musa amesisitiza kuwa kushikamana na kuunga mkono kwa dhati kadhia ya Palestina kunawakilisha kanuni ya msingi na njia pekee ya kuunganisha safu mbalimbali za mataifa ya Kiislamu na Kiarabu.

“Iran imesimama kidete kutetea mamlaka yake na hadhi yake, pamoja na masuala nyeti ya Ummah mzima wa Kiislamu,” amesema kiongozi huyo wa kupigania ukombozi wa Palestina. Aidha amesisitiza kuwa Jamhuri ya Kiislamu “iliweza kuvunja haiba ya Marekani wakati ikiwa katika kilele cha ubeberu wake wa kimataifa.”

Msemaji huyo wa Jihad Islami amesistiza kuwa: “Yeyote anayefikiri kuwa roho ya Ayatullah Khamenei Shahidi haipo tena, amekosea sana, kwani makundi ya Muqawama yanayopambana huko  Lebanon na katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu yanazidi kupata nguvu kila uchao. Mapambano yanaendelea, na fungamano letu kwa haki ya ardhi yetu na maeneo matakatifu ni imara na haliwezi kutikisika.”

Hajj Musa amemalizia kwa kusema, “Damu takatifu na ya thamani ya Shahidi Ayatullah Khamenei, licha ya maumivu makali inayoacha katika nyoyo zetu, inatupa azma zaidi na uthabiti wa kumuumiza adui Mzayuni, na inabariki njia ya Muqawama.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *