
ILIPOISHIA
Mganga alikuwa kwenye chumba cha mke mkuu. Aliposikia sauti yangu akatoka na kuniuliza.
“Umesharudi?”
“Nimerudi, nilikuwa nimekwenda msalani”
“Huyo uliyekwenda kumsalimia hajambo?” Mganga aliniuliza hivyo kwa kuzuga ili wake zake wasijue kama nilikwenda madukani.
“Hajambo, anawasalimia”
Mganga huyo akajifanya kama anakwenda msalani. Nilijua kwamba alikuwa anavunga tu ili mke wake asijue kuwa alitoka chumbani baada ya kusikia sauti yangu. Alitaka mke wake ajue kuwa alitoka chumbani ili aende msalani..
SASA ENDELEA…
NIKAINGIA chumbani mwangu. Baada ya muda kidogo mganga akaingia na kukaa kitandani.
“Umenunua vitu ulivyotaka?” akaniuliza kwa sauti ya chini chini iliisisikike.
“Nimenunua. Hivyo humo kwenye mfuko”
Mgannga akauchukua mfuko huona kuvitoa vitu nilivyokuwa nimenunua zikiwemo nguo za ndani. Akazitazama kisha akazirudisha mle mle.
“Usije ukawambia wenzako kuwa ulikwenda madukani. Ukiwambia wataona wivu, wataona nakupenda wewe zaidi. Umesikia?”
“Nimesikia mumewangu”
“Hawa ni washamba, waache hivyo hivyo na ushamba wao. Watavaa kaniki na shuka ninazoagulia watu hapa hapa. Sidiria zao pia ni za kushonesha”
Nilitaka kucheka aliponiambia hivyo lakini nikajizuia na kumuitikia.
“Sawa, nimekeuelwa.’’
Siku iliyofuata saa nne asubuhi nilikuwa chumbani mwangu nimekaa kitandani kwangu, ghafla nikasikia sauti ya mwanamke akibisha hodi huko uani. Nilitaka nitoke nimuitikie lakini mke mwenzangu aliyekuwa akitoka msalani akawahi kumuitikia.
“Karibu”
“Habari za hapa?” mwanamke huyo akauliza.
“Nzuri, karibu”
Nikapata shauku ya kutoka ili nimuone. Wakati nachungulia kwenye mlango kabla sijatoka nikamuona lakini yeye hakuniona.
Nikashituka! Unajua alikuwa nani?
Alikuwa wifi yangu, mdogo wake mume wangu niliyemtoroka! Nikahisi kwamba huenda amesikia kuwa ninaishi pale na amekuja kuniulizia.
Nikarudi ndani haraka ili asinione.
“Nilikuwa namuhitaji mganga, sijui yupo?” wifi yangu akauliza.
“Mganga yupo, chumba chake ni hiki” mke mwenzangu akamwambia.
Nikamsikia wifi yangu akibisha katika kile chumba kisha akakaribishwa ndani.
Hicho chumba kinapakana na kile chumba nilichokuwemo. Kwa vile nyumba haikuwa na dari, sauti za chumba kimoja zilikuwa zikisikika katika chumba kingine.
Nikamsikia akiulizana hali na yule mganga na kisha akaulizwa alikuwa akihitaji nini.
“Nina tatizo lililonileta” wifi yangu akamwambia mganga.
“tatizo gani?”
“Hilo tatizo halinihusu mimi, linamhusu kaka yangu”
Moyo wangu ukashituka kidogo niliposikia akisema kuwa tatizo lililomleta linamhusu kaka yake ambaye ni mume wangu niliyemtoroka.
“Nieleze ni tatizo gani?”
“Mke wa kaka yangu ametoroka nyumbani na hajulikani yuko wapi. Tumehangaika kumtafuta mpaka imebidi twende kwa waganga kumtazamia. Kila mganga tunayemwendea anatuambia eti amefungwa na mganga na hawezi kurudi mpaka huyo mganga ategue dawa zake. Ukiangalia haya maneno ni kweli?”
Hapo nikaanzakupata hofu kwamba mganga huyo ameshagundua kuwa mke anayetafutwa ni mimi. Lakini pakapita ukimya kidogo. Baadaye nikasikia sauti ya mganga akiniita.
Nikaguna na kunyamza kimya.
“Ananiita ili iweje?” nikajiuliza.
Akaniita mara ya pili. Nikaendelea kubaki kimya. Mke mkubwa akaingia chumbani mwangu nakuniambia.
“Unaitwa”
“Siendi, nenda wewe. Huyo msichana niliwahi kugombana naye. Sitaki anione hapa” nikamdanganya kwa kumnong’oneza.
Yule mwanamke akanielewa akatoka na kwenda yeye chumbani kwa mganga.
Nikamsikia akimwambia mganga.
“Huyo unayemuita kaenda dukani, nimekuja mimi”
“Nilikuwa nahitaji moto”
“Ngoja nikakuletee”
Yule mwanamke baada ya kupeleka moto hakurudi tena mle chumbani.
Sasa nikawa najiuliza huyu mganga hakugundua kuwa huyo msichana anayeelezwa kuwa amemtoroka mume wake ni mimi? Kama amegundua ni kwanini aniite mbele yake nimletee moto?
Nikahisi kwamba kwa vyovyote vile yule mganga hakugundua. Kama angejua asingeniita mbele ya yule msichana ambaye ni wifi yangu.
Nikajiuliza tena, hivi uganga wake au majini wake wameshindwa kutambua kuwa msichana aliyekusudiwa ni mimi au ndio kama wanavyosema waswahili mganga hajigangi! Na wengine wanasema jicho halijioni!
Baadaye kidogo nikasikia sauti ya mganga huyo akimwambia wifi yangu.
“Ramli yangu inaonesha ni kweli huyo msichana amefungwa na mganga na ni mimi peke yangu niinayeweza kumfungua ili aweze kurudi kwa mume wake. Nataka mniletee kuku mweusi na upande mmoja wa kaniki”
“Hivyo vitu vikipatikana, wifi yangu ataweza kurudi kwa kaka?”
“Atarudi bila wasiwasi wowote. Kinachowaponza hawa wasichana sikuhizi ni tamaa tu ya maisha”
“Ni kweli kwa sababu kaka amenieleza kuwa hawakugombana. Alioondoka ghafla tu”
“Ndiyo hivyo. Kapata mtu kamdanganya, kaamua kubaki huko huko”
“Sasa nije lini?”
“Siku yoyote ukiwa tayari njoo tu”
“Basi nitakuja kesho pamoja na hivyo vitu”
“Hakuna tatizo. Mimi nipo”
“Hii ramli yako ni shilingi ngapi?”
“Nipe elfu tano”
Baada ya wifi yangu kutoa hiyo pesa nikamsikia akiagana na yue mganga kisha akatoka.
Ghafla yakanijia mawazo kwamba huenda mganga huyo alikuwa amemdanganya wifi yangu kumwambia alete kuku na upande wa kaniki ili amshughulikie. Niliamini kwamba alishajua kuwa msichana aliyekusudiwa nilikuwa mimi na kwa hivyo asingependa nirudi kwa mume wangu.
Baada ya wifi yangu kuondoka, nilibaki pale kitandani nilipokuwa nimeketi. Mwisho nijilaza na kupitiwa na usingizi hapo hapo.
Nililala kwa kafibu saa mbili. Aliyekuja kuniamsha alikuwa mke mdogo wa mganga.
“Vipi mwenzangu, mbona umelala sana leo?” akaniuliza.
“Ah! Ni uchovu tu” nikamjibu huku nikiinuka kitandani.
Nikakaa kwenye kitanda na kumuuliza.
“Unasemaje?”
“Kama umechoka pumzika tu. Huo ugali nitakwenda kusonga mimi”
“Ngoja niende nikasonge tu” nikamwambia.
Nikainuka kwenye kitanda. Siku ile ilikuwa ni zamu yangu ya kupika.
Kwanza nilikwenda msalani. Nilipotoka ndio nikaanza kushughulika na upishi
Siku ile mume wetu hakuniambia chochote kuhusu yule msichana aliyekuja. Nikajua hakugundua kuwa mimi ndiye niliyekuwa ninatafutwa. Na mimi sikutaka kumueleza chochote.
Asubuhi ya siku iliyofuata mimi na wake wenzangu tulichukua ndoo zetu na kwenda kuchota maji. Tulipofika huko tulikuta foleni ndefu. Maji yalikuwa yakitoka kidogo dogo. Tukaziweka ndoo zetu kwenye msururu wa ndoo zilizokuwa zimepangwa.
Mpaka inafika zamu yetu ilikuwa karibu saa tatu asubuhi, tukapeleka maji nyumbani kisha tukarudi tena na kupanga foleni. Hii foleni ya mara ya pili, maji yalikuwa yakitoka kidogo dogo zaidi. Ikabidi tusubiri kwa muda mrefu zaidi. Mke mkuu alitangulia kuchota maji akarudi nyumbani.
Baadaye ikafuatia zamu ya mke wa pili. Mimi nilikuwa wa tatu. Ndoo ya mke wa pili ilipojaa ndipo ikafuatia ndoo yangu.
Niliondoka saa sita pale kwenye maji. Nilikuwa sijaoga wala kunywa chai. Wakati narudi nikapishana na wake wenzangu. Walikuwa wanakwenda tena kuchota maji.
Nilipokuwa nakaribia kufika nyumbani nikamuona yule wifi yangu anatoka pale nyumbani.Kwanza niilishituka nilipomuona kisha nikasimama na kugeuka upande mwingine ili asinione. Akapita nyuma yangu bila kunitambua. Bila shaka alikuwa ameshafanyiwa uganga wake.
Baada ya kunipita nikaendelea na safari yangu. Nikaingiala nyumbani kwetu na kukuta kuku amechinjwa kando ya mlango.Nikajua ni kuku wa uganga wa wifi yangu.
Mume wetu alikuwa akitoka kwenye chumba chake cha uganga akanikuta ninaingia.
“Leo maji yamekuwa na taabu sana”akaniambia.
“Mmh…! Kuna foleni ndefu. Maji yanatoka kigdogo kidogo sana”
“Naona mmechelewa sana, mpaka saa hizi bado mnachota!”
“Tutafanyaje? Hatujaoga wala hatujakunywa chai”
“Sasa itabidi uwaachie wenzako waendelele, wewe shughulikia huyo kuku. Tutamlia ugali mchana”
“Ni kuku wa uganga?” nikajidai kumuuliza.
“Riziki imekuja sasa hivi. Kuna msichana nilimshughulikia shida yake. Ameshaenda”
“Sawa. Ngoja nimimine haya maji nimshughulikie huyo kuku”
Huyu ni mganga gani ambaye ameshindwa kujua kuwa mtu aliyemfanyia uganga huo ni mke wake? Nikajiuliza moyoni mwangu.