• Safari ya shule iligeuka kuwa janga lisilofikirika baada ya basi lililokuwa limewabeba wanafunzi wa King David Junior School kupata ajali lilipokuwa likirejea kutoka ziara ya kielimu, na kuwaua watoto 20 pamoja na mtu mzima mmoja
  • Polisi wanasema basi hilo lilipoteza mwelekeo kabla ya kutoka barabarani, kugonga mwamba mkubwa uliokuwa kando ya barabara na kupinduka
  • Miili ya waliofariki imehifadhiwa katika Mochari ya Kapchorwa huku uchunguzi ukiendelea kubaini chanzo cha mojawapo ya ajali mbaya zaidi za mabasi ya shule nchini Uganda katika miaka ya hivi karibuni

Kilichoanza kama siku ya kujifunza na burudani kiligeuka kuwa simanzi baada ya basi lililokuwa limewabeba wanafunzi wadogo kupata ajali na kugharimu maisha ya watu wengi wasio na hatia.

Wanafunzi 20 wafariki katika ajali ya basi la shule Uganda
Mabaki ya basi la shule iliyoanguka na kusababisha vifo vya wanafunzi 20 na mtu mzima 1. Picha: Uganda Police Force.
Source: Facebook

Jeshi la Polisi la Uganda limethibitisha kuwa watu 21, wakiwemo wanafunzi 20 na mtu mzima mmoja, walifariki dunia kufuatia ajali mbaya ya barabarani katika Wilaya ya Kapchorwa Alhamisi jioni, Julai 16.

Ajali hiyo ilihusisha basi aina ya Isuzu lenye nambari ya usajili UA 108BQ, linalomilikiwa na King David Junior School iliyoko Ndejje, Kitengo cha Makindye, Kampala.

Pia soma

“Usalama kwanza”: Wizara ya Elimu nchini Uganda yafuta safari zote za shule baada ya ajali kuua 21

Ajali ya basi la shule Uganda ilitokeaje?

Kwa mujibu wa polisi, ajali hiyo ilitokea katika Kijiji cha Chekwatit, Parokia ya Kimawa, Kaunti Ndogo ya Kawowo, majira ya saa mbili usiku (takriban saa 8:00 pm), na kusababisha polisi pamoja na vikosi vya uokoaji kufika eneo la tukio mara moja.

Awali, mamlaka zilisema bado zilikuwa zikitathmini ukubwa wa janga hilo huku shughuli za uokoaji zikiendelea.

Hata hivyo, katika taarifa iliyotolewa baadaye, Polisi wa Uganda walithibitisha kuwa idadi ya waliofariki imefikia 21, wakiwemo wanafunzi 20 na mwanaume mmoja mtu mzima.

Walionusurika kadhaa ambao utambulisho wao ulikuwa bado haujafahamika walikimbizwa katika Kituo cha Afya cha Kaserem Level IV, Hospitali Kuu ya Kapchorwa, na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mbale kwa matibabu.

Ni nini kilisababisha ajali hiyo?

Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa wanafunzi hao walikuwa wamesafiri kwenda Maporomoko ya Maji ya Sipi (Sipi Falls) katika Wilaya ya Kapchorwa kwa ziara ya kielimu.

Polisi walisema mkasa huo ulitokea wakati kundi hilo lilipokuwa likirejea Kampala.

Pia soma

Ajali ya basi la shule yaua wanafunzi wasiopungua 20 nchini Uganda

“Walipokuwa wakirejea kutoka kwenye ziara hiyo, dereva aliripotiwa kupoteza mwelekeo wa gari, ambalo lilitoka barabarani, likagonga jiwe kubwa lililokuwa kando ya barabara na kisha kupinduka,” Polisi wa Uganda walisema.

Mbali na waliofariki, wanaume watatu watu wazima pamoja na watoto kadhaa walijeruhiwa katika ajali hiyo.

Miili ya waliofariki imepelekwa katika Mochari ya Kapchorwa, ambako inasubiri kutambuliwa na ndugu pamoja na kufanyiwa uchunguzi wa maiti.

Mamlaka zilisema uchunguzi kuhusu chanzo halisi cha ajali hiyo bado unaendelea, zikiongeza kuwa taarifa zaidi zitatolewa zitakapopatikana.

“Jeshi la Polisi la Uganda linatoa pole za dhati kwa familia zilizopoteza wapendwa wao, uongozi wa King David Junior School na wote walioathiriwa na tukio hili la kusikitisha. Pia tunawatakia majeruhi kupona haraka na kikamilifu,” polisi walisema.

Jinsi basi la AIC Lomut lilivyopata ajali likiwa na wanafunzi 56

Takribani wiki moja iliyopita, TUKO.co.ke iliripoti kuwa basi la shule lililokuwa limewabeba wanafunzi 56 na walimu wanne kutoka AIC Lomut Secondary School lilihusika katika ajali ya barabarani kwenye Barabara ya Kabarnet-Marigat likielekea Eldoret.

Vikosi vya dharura vilihamisha wanafunzi na walimu waliojeruhiwa hadi Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Baringo, ambako walipatiwa matibabu pamoja na huduma za usaidizi wa kisaikolojia.

Pia soma

Magazeti ya Kenya, Julai 15: Kundi la Edwin Sifuna latikisa serikali na muungano wa upinzani

Kwa bahati nzuri, hakuna kifo wala majeraha ya kutishia maisha yaliyoripotiwa.

Read: ENGLISH VERSION

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.

Chanzo: TUKO.co.ke

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *