Rais William Ruto ametangaza uteuzi na mapendekezo mapya katika Idara ya Utendaji, akimteua Msemaji mpya wa Serikali huku akiwasilisha majina ya wateuliwa katika Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC), Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) na taasisi nyingine za serikali.

Katika mabadiliko yaliyotangazwa siku ya Jumanne, Julai 21, aliyekuwa msemaji wa polisi Charles Owino Wahong’o amehamishwa kutoka Wizara ya Habari, Mawasiliano na Uchumi wa Kidijitali (ICT) na kuteuliwa kuwa Msemaji mpya wa Serikali.

Mabadiliko hayo pia yamemshuhudia aliyekuwa Katibu Mkuu wa Kenya National Union of Teachers (KNUT), Wilson Sossion, akiteuliwa kuwa mjumbe wa Bodi ya Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC).

Antonina Lentoijoni pia amependekezwa kuwa mjumbe wa TSC, huku majina yao yakipelekwa bungeni kwa ajili ya kuidhinishwa kwa mujibu wa Katiba.

Charles Owino

Rais Ruto pia amempendekeza Dkt. Duncan Ojwang Oburu kuhudumu kama Mwenyekiti wa IPOA, uteuzi ambao unasubiri kuidhinishwa na Bunge.

Pia soma

Mbunge wa EALA Kanini Kega Asema Amenyang’anywa Walinzi Mara Baada ya Uchaguzi Mdogo wa Ol Kalou

Nafasi ya Mwenyekiti wa IPOA ilibaki wazi baada ya Issack Hassan kujiuzulu kufuatia kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufaa.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Felix Koskei, Ruto alifanya mabadiliko hayo baada ya Tume ya Utumishi wa Umma (PSC) kuidhinisha kupandishwa vyeo na kuhamishwa kwa maafisa wa ngazi za juu katika Idara ya Utendaji.

“Mheshimiwa Rais leo amefanya mapendekezo ya uteuzi katika Tume mbalimbali za Kikatiba na Taasisi za Kisheria na Mahusiano ya Kiserikali kujaza nafasi zilizokuwa wazi mapema mwaka huu. Aidha, Tume ya Utumishi wa Umma imeidhinisha kupandishwa vyeo na kuhamishwa kwa maafisa wa ngazi za juu katika Idara ya Utendaji,” Koskei alisema katika taarifa hiyo.

Kufuatia uteuzi wa Owino, Isaac Mwaura, ambaye amehudumu kama Msemaji wa Serikali tangu mwaka 2022, amepandishwa cheo na kuteuliwa kuwa Mkuu wa Ofisi ya Uanuwai, Ushirikishwaji na Haki za Watu Wenye Ulemavu katika Ofisi ya Rais.

Wakati huohuo, Rais amempendekeza Flora Mutua kuwa mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Umma (PSC), taasisi inayosimamia masuala ya usimamizi wa rasilimali watu na utawala katika utumishi wa umma.

Pia soma

Kenya yaomboleza: Aliyekuwa Kamishna wa IEBC Mohamed Sharawe afariki dunia

Uteuzi mwingine

Rais Ruto pia amewapendekeza watu saba kuhudumu katika Kamati ya Kiufundi ya Mahusiano kati ya Serikali (IGRTC), uteuzi ambao unasubiri kuridhiwa na Mkutano wa Kuratibu Serikali za Kitaifa na Kaunti.

Miongoni mwa waliopendekezwa ni Mary Nanjala Kilobi (mke wa Katibu Mkuu wa COTU, Francis Atwoli), ambaye atawakilisha Kaunti ya Nairobi.

Wengine ni Wilson Kuria Thuita (Murang’a), Silvya C. Apaa (Busia), Ahmed Kanyara Bishar (Wajir), Pascalyne Ntang’enoi Kimiriri (Laikipia), Ken Riaga (Migori) na Evalyn Chepkirui Aruasa (Nakuru).

Read ENGLISH VERSION

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.

Chanzo: TUKO.co.ke

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *