Afrika Kusini imetangaza siku ya Ijumaa, Januari 30, 2026, afisa mmoja wa ubalozi wa Israel kuwa mtu asiyestahili. “Hatua hii inafuatia mfululizo wa ukiukwaji usiokubalika wa kanuni na desturi za kidiplomasia,” imesema Idara ya Uhusiano wa Kimataifa. Kwa miezi kadhaa, maelezo rasmi ya ubalozi kwenye mtandao wa kijamii wa X yamekuwa maarufu kwa ukosoaji wake mkali dhidi ya serikali ya Afrika Kusini. Saa chache baadaye, Israel, nayo ilimfukuza mwanadiplomasia wa Afrika Kusini.

Imechapishwa:

Dakika 1 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Katika taarifa yake, Pretoria ilibainisha kwamba Israel inakiuka kanuni za kidiplomasia, haswa kupitia mitandao ya kijamii, bila kufafanua zaidi. Chapisho kwenye mtandao wa kijamii wa X lilizua utata mnamo mwezi Novemba 2025, anakumbusha mwandishi wetu huko Johannesburg, Valentin Hugues: kujibu taarifa ya mkuu wa nchi wa Afrika Kusini, ubalozi wa Israel uliandika: “Wakati nadra wa hekima na uwazi wa kidiplomasia kutoka kwa rais Cyril Ramaphosa.” 

Hivi majuzi zaidi, ubalozi wa Israel ulimtakia balozi mpya wa Marekani nchini Afrika Kusini, kiongozi mwenye msimamo mkali na mwenye utata mkubwa huko, “bahati nzuri.”

Wizara ya Mambo ya Nje ya Afrika Kusini ilitangaza kwamba Ariel Seidman, mwanadiplomasia mkuu wa Israeli aliyeko Pretoria, lazima aondoke nchini humo ndani ya saa 72. Afrika Kusini pia iliitaka serikali ya Israel kuhakikisha kwamba diplomasia yake katika siku zijazo “inaonyesha heshima inayostahili kwa Afrika Kusini.”

Serikali mbili zinazokinana, haswa kuhusu vita huko Gaza

Israel inaona uamuzi wa Pretoria kuwa “hauna msingi” na inapuuza hoja za Afrika Kusini kama “habari potovu.” Tangu Afrika Kusini ifunge ubalozi wake huko Tel Aviv miaka miwili iliyopita, Israel ilichagua kujibu kwa kumfukuza Shaun Byneveldt, mwakilishi wa Afrika Kusini kwa Palestina, aliyeko Ramallah, katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa. Yeye pia, ataondoka katika eneo hilo ndani ya saa 72.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Israel pia ilionya kwamba “hatua zaidi zitazingatiwa kwa wakati unaofaa.” Mazungumzo haya ni kielelezo kingine cha mvutano mkubwa kati ya serikali hizo mbili. Mzozo huu umeongezeka zaidi tangu mwaka 2023 na malalamiko yaliyowasilishwa na Afrika Kusini kwa Mahakama ya Kimataifa ya Haki dhidi ya Israel kwa mauaji ya kimbari huko Gaza.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *