Wizara ya Sheria ya Marekani imetoa mamilioni ya nyaraka mpya zinazohusiana na kesi ya Jeffrey Epstein, mtendajinai aliyepatikana na hatia ya makosa ya kingono dhidi ya watoto, kabla ya kuondoa baadhi ya kurasa zilizokuwa na malalamiko yaliyomtaja Rais Donald Trump.

Naibu Mwanasheria Mkuu Todd Blanche alisema Ijumaa kuwa takriban faili milioni 3.5 zilichapishwa kwa lengo la kutekeleza Sheria ya Uwazi wa Epstein, kufuatia ukosoaji kwamba serikali ilikosa kutimiza muda wa mwisho uliowekwa na Bunge tarehe 19 Desemba.

Nyaraka hizo zinajumuisha mawasiliano ya FBI na malalamiko yaliyowasilishwa kama taarifa, baadhi yake yakimtaja Trump pamoja na watu wengine waliokuwa na uhusiano wa kijamii au kikazi na Epstein.

Trump amekanusha mara kwa mara madai yoyote ya kosa kuhusiana na mahusiano yake ya zamani na Epstein.

Baada ya kuchapishwa, kurasa zilizokuwa na malalamiko yaliyomtaja Trump ziliondolewa kwenye tovuti ya Wizara ya Sheria ya Marekani (DOJ) na sasa zinaonyesha ujumbe wa “ukurasa haupatikani.” Hata hivyo, nakala za nyaraka hizo zimesambaa kwa upana kupitia mitandao ya kijamii. Mtangazaji wa CNN Jake Tapper alikuwa miongoni mwa waliobainisha hadharani kuwa kurasa hizo zilikuwa zimeondolewa.

Moja ya malalamiko, yaliyowasilishwa na rafiki wa anayedaiwa kuwa mhanga, yanasema kuwa Trump alimlazimisha msichana mwenye umri wa miaka 13–14 kufanya tendo la ngono ya mdomo takriban miaka 35 iliyopita huko New Jersey. Hati hiyo inaeleza kuwa mpelelezi alitumwa Washington kufanya mahojiano.

Malalamiko mengine yanasema kuwa Trump alikuwa akimlipa mtu fulani mara kwa mara kufanya vitendo vya kingono, na yanaongeza kuwa alikuwepo wakati mtoto mchanga wa mtu huyo alipouawa.

Malalamiko mengine tofauti yanasema kuwa sherehe zilizojulikana kama “calendar girls” katika jumba la Mar-a-Lago la Trump zilihusisha watoto na unyanyasaji wa kingono. Hati hiyo pia inataja majina ya watu kadhaa maarufu kuwa walihudhuria matukio hayo.

Katika taarifa nyingine, mlalamikaji alisema alishuhudia  “mtandao wa biashara haramu ya ngono” katika Klabu ya Gofu ya Trump National huko Rancho Palos Verdes, California, katikati ya miaka ya 1990. Mhusika huyo amesema kuwa alipokea “vitisho” kutoka kwa mkuu wa ulinzi wa Trump iwapo angezungumza hadharani kuhusu aliyoyaona.

Utoaji wa hivi karibuni wa nyaraka pia unajumuisha rasimu ya barua pepe ambayo Jeffrey Epstein aliandika  mwaka 2013, akimtaja mwanzilishi mwenza wa Microsoft, Bill Gates. 

Wizara ya Sheria ya Marekani (DOJ) haijatoa maelezo ya kina kuhusu sababu ya kuondolewa kwa baadhi ya kurasa baada ya kuchapishwa. Idara hiyo imesema kuwa mchakato wa kutoa nyaraka bado unaendelea.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *