Dar es Salaam. Shahidi wa 14 katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, ameieleza Mahakama kuwa alitishiwa maisha na wafuasi wa Chadema kuwa akienda kutoa ushahidi katika kesi hiyo lolote baya litampata.

Shahidi huyo ambaye ni miongoni mwa mashahidi fiche wa Jamhuri (waliopewa ulinzi, yaani wasiotakiwa kuonekana wala kutambulika), wanaotoa ushahidi wakiwa ndani ya kizimba maalumu ambamo hawawezi kuonekana kwa wasikilizaji wala mshtakiwa isipokuwa kwa majaji tu ametambulishwa kwa jina la P9 (38).

Alitoa madai hayo wakati akihojiwa na mshtakiwa Lissu maswali ya dodoso kuhusiana na ushahidi wake wa msingi, alioutoa wakati akiongozwa na mwendesha mashtaka, Wakili wa Serikali Cuthbert Mbilingi.

Hata hivyo, Lissu kutokana na maswali aliyombana amemwambia anaamini kuwa atakwenda kuwaeleza askari aliodai kuwa ndio waliomtengeneza na kumtuma kutoa ushahidi kwenye kesi yake kuwa huko hakufai.

Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini kinyume na kifungu cha 39(2) (d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, linalotokana na maneno aliyoyatamka kuhusiana na kusudio la kuzuia kufanyika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Anadaiwa kuwa Aprili 3, 2025, jijini Dar es Salaam, akiwa raia wa Tanzania, kwa nia ya uchochezi alishawishi umma kuzuia kufanyia kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, huku akitamka na kuandika maneno ya kumshinikiza kiongozi Mkuu wa Serikali ya Tanzania kuwa:-

“Wakisema msimamo huu unaashiria uasi, ni kweli…, kwa sababu tunasema tutazuia uchaguzi, tutahamasisha uasi, hivyo ndivyo namna ya kupata mabadiliko…, kwa hiyo tunaenda kukinukisha…, sana sana huu uchaguzi tutaenda kuuvuruga kwelikweli…, tunaenda kukinukisha vibaya sana…”

Kesi hiyo inayosikilizwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam na jopo la majaji watatu linaloongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Iringa, Dunstan Ndunguru akishirikiana na majaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.

Shahidi huyo wa 14, P9 ni mkazi wa Mbeya, fundi umeme na pia ni mfuasi wa Chadema.

Kwa mujibu wa ushahidi wake mwaka 2024, alivutiwa na sera na kuwa mfuasi wa Chadema.

Aprili 3, 2025 usiku akiwa nyumbani kwake, akiwa anapitiapitia mitandao ya kijamii kupitia simu yake ya mkononi aina ya Sumsung, Pro 8, katika mtandao wa Instagram, aliona video ya Lissu.

Katika video hiyo, Lissu alitamka maneno ya kuzuia uchaguzi wa mwaka 2025 usifanyike kwa kukichafua na kwa kuwa yeye alikuwa mfuasi wa chama hicho, alihamasika kwa kauli hizo za Lissu.

Aprili 4, 2025 asubuhi, akiwa nyumbani na jamaa zake anaoishi nao, wakati wakiendelea kujadili suala la Lissu kuhusu kufanya vurugu katika uchaguzi, alitokea mtu ambaye alimuomba namba ya simu na akamwambia kuwa watakaa kwa ajili ya kujadiliana zaidi suala hilo.

Aprili 5, 2025 asubuhi, alipigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kuwa ni mteja na anataka huduma ya kufungiwa umeme akamueleza mahli alikokuwa akaenda kukutana naye.

Alipofika yule mtu aliyempigia simu alijitambulisha kuwa yeye ni ofisa wa polisi kutoka kituo cha Polisi Mwanjelwa huku akimuonesha kitambulisho cha kazi.

Askari huyo alimuweka chini ya ulinzi na akamtaka waongozane hadi kituo cha polisi Mwanjelwa ambako alihojiwa na akaachiwa kwa dhamana.

Aprili 22, 2025 alipigiwa simu akiitwa kituo cha Polisi Mwanjelwa ambako alihojiwa na kuandikwa maelezo kuhusiana na kuhamasisha kuzuia uchaguzi namna alivyoanza.

Alieleza kuwa ailiona video kwenye mtandao wa kijamii ikimuonesha Tundu Lissu akizungumzia kuzuia uchaguzi.

Baada ya maelezo hayo ndipo Lissu akaanza kumhoji maswali mbalimbalj ya dodoso ikiwa ni pamoja na kama aliwahi kutishiwa, kama ifuatavyo;

Lissu: Shahidi kuna viongozi ama wafuasi wowote wanaojua kuwa umekuja kutoa ushahidi wake hapa?

Shahidi: Nahisi baadhi wanajua,

Lissu: Ulishawahi kutishiwa na wafuasi wa Chadema?

Shahidi: Ndio walishanitishia kwa maneno.

Lissu:- Walikutishaje?

Shahidi:- Kama unaenda kutoa ushahidi, lolote baya linaweza kukuta.

Lissu:- Hao wafuasi ni kina nani?

Shahidi:- Siwezi kuwataja

Lissu:- Waeleze majaji kama uliwahi kutoa taarifa kituo chochote cha Polisi?

Shahidi:- Ndio nilishatoa taarifa kituo cha Polisi

Lissu:- Kituo gani?

Shahid:- Siwezi kukitaja

Jaji:- Jibu hilo swali, ndugu shahidi

Shahidi:- Kituo cha Polisi Ilonga.

Lissu:- Ulipewa RB?

Shahidi:- Ndio

Lissu:- Hiyo RB umeiwasilisha mahakamani hapa?

Shahidi: Sijaiwasilisha

Lissu:- Waeleze majaji Polisi walichukua hatua gani?

Shahidi:- Walinieleza kuwa wanafuatilia.

Lissu: Hao watu walishakamatwa na kufikishwa mahakamani?

Shahidi: Hawajawahi kukamatwa.

Lissu:- Hadi sasa hao watu wamekamatwa na kupelekwa mahakamani?

Shahidi:-Hawajakamatwa na hawajapelekwa mahakamani.

Lissu: Bado sijamalizana na wewe, nataka tukimalizana hapa uende uwaeleze hao mapolisi waliokutuma kuwa kule hakufai.

Shahidi: Hayo ni yako.

Lissu: Nina uhakika utawaambia huko hakufai.

Lissu: Waeleze majaji kama una fahamu au hufahamu kuwa kuzuia uchaguzi siyo kosa.

Shahidi: Najua kuzuia uchaguzi ni kosa kwa mujibu wa sheria.

Lissu: Waeleze majaji ni sheria gani iliyozungumza kuzuia uchaguzi ni kosa.

Shahidi: Mimi siyo mwanasheria, ila najua kuzuia uchaguzi ni kosa.

Lissu: Wewe mbumbumbu tu unajuaje?

Shahidi: Najua tu, kwani kufanya vurugu si ni kosa?

Lissu:- Kwani mimi nimeshtakiwa kwa kufanya vurugu?

Shahidi: Kwa uhaini ambapo ndani yake ndio kuna vurugu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *