Makabiliano makali ya kijeshi yameendelea kushuhudiwa kati ya nchi jirani za Afghanistan na Pakistan, kuanzia usiku wa kuamkia Ijumaa, na kuzua wasiwasi wa nchi hizo kuingia kwenye vita vya muda mrefu kwa sababu ya mzozo wa mpaka.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Waziri wa Ulinzi wa Pakistan Khawaja Asif, amesema nchi yake ipo kwenye vita vya wazi dhidi ya Afghanistan inayoongozwa na Taliban na uvumilivu wan chi yake umekwisha.
Aidha, Asif amesema operesheni ya kijeshi inaendelea nchini Afganistan, baada ya saa kadhaa ya makabiliano makali kati ya mipaka ya nchi hizo mbili.
Kabla ya kauli hii ya Pakistan, msemaji wa serikali ya Taliban Zabihullah Mujahid alisema, Afghanistan ilikuwa inatekeleza mashambulio makubwa dhidi ya jeshi la Pakistan.
Pakistan inasema, imewauwa wapiganaji 274 wa Taliban, huku ikipoteza wanajeshi wake wawili. Hata hivyo, Afganistan kwa upande wake inasema, imewauwa wanajeshi 55 wa Pakistan na kupoteza wapiganaji wake wanane.
Makabiliano haya yametangulia na vita vya mpakani ambavyo vimekuwa vikiendelea kwa wiki kadhaa sasa na kusababisha mauaji ya raia wa nchi hizo mbili.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, amesema anafuatilia kwa karibu kinachoendelea na kutoa wito kwa pande zote kuheshimu sheria za Kimataifa na kuhakikisha kuwa, raia wa kawaida wanalindwa.
Iran nayo kupitia Waziri wake wa Mambo ya nje Abbas Araghchi, ametoa wito kwa nchi hizo jirani kutatua tofauti zao kwa njia ya mazungumzo, wito ambao pia umetolewa na Qatar.