
ARUSHA: Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Arusha na Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Cecilia Paresso, ametoa mchango wa mbao zenye thamani ya Sh milioni 2.5 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Karatu mkoani hapa.
Mbao hizo zimekabidhiwa rasmi leo mbele ya viongozi mbalimbali wa chama na Serikali wilayani Karatu ikiwa ni sehemu ya mchango wake wa awali katika kuunga mkono juhudi za chama za kuboresha mazingira ya kazi na makazi ya watumishi wake kama alivyoahidi katika kampeni.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Paresso alisisitiza umuhimu wa mshikamano na ushirikiano katika kujenga na kuimarisha miundombinu ya Chama itakayowawezesha watumishi wa chama kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi wakiwa kazini.

Viongozi wa CCM Karatu walimshukuru Mbunge huyo kwa mchango wake, wakieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu muhimu ya kuharakisha ujenzi wa nyumba hizo na kuwahamasisha wadau wengine kujitokeza kuchangia mradi huo