Tanzania yaweka alama mpaka wa KenyaTanzania yaweka alama mpaka wa Kenya

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeeleza kuridhishwa na maendeleo ya kazi ya uimarishaji wa mpaka wa kimataifa kati ya Tanzania na Kenya. Mwenyekiti wa kamati hiyo, Timotheo Mzava, amesema kuwa hadi sasa jumla ya kilometa 564 sawa na asilimia 75 ya mpaka wa nchi kavu tayari zimewekewa alama kati ya kilometa 758 za mpaka mzima.

Mzava alitoa kauli hiyo wakati kamati hiyo ilipofanya ziara ya ukaguzi katika eneo la Holili, wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro mwishoni mwa wiki. Amesema  kazi iliyofanyika ni kubwa na ya kupongezwa, huku akitambua juhudi zinazofanywa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

“Hapa ukisimama unaweza kuona alama za mpaka zimewekwa hadi mbali. Ni kazi kubwa imefanyika na tunawapongeza wizara kwa juhudi hizo,” alisema. SOMA: Kamati ya Bunge yaridhishwa kasi ujenzi jengo jipya CBE

Hata hivyo, kamati hiyo imeitaka serikali kuhakikisha inakamilisha uimarishaji wa mpaka huo uliosalia. Imeeleza kuwa inatarajia kuona mipango ya kifedha pamoja na bajeti itakayosaidia kukamilisha kazi hiyo ikiwekwa wazi katika bajeti ya sasa na ile ya mwaka wa fedha 2026/2027.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Kaspar Mmuya, amesisitiza umuhimu wa wataalamu wa wizara kuendelea kutoa elimu kwa wananchi wanaoishi katika maeneo ya mipakani ili waweze kuelewa wajibu wao katika kulinda mipaka ya nchi. Amesema hata Katiba ya nchi inaeleza kuwa wananchi wana wajibu wa kushiriki katika ulinzi wa mipaka ya taifa lao, hivyo ushirikishwaji wao kupitia elimu ni muhimu ili wawe sehemu ya juhudi hizo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Rombo, Raymond Mwangwala, alisema mpaka kati ya Tanzania na Kenya upo salama na wananchi wa maeneo ya mpakani wanaendelea na shughuli zao za kiuchumi huku wakidumisha uhusiano mzuri kati yao.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *