DAR ES SALAAM: BENKI ya Maendeleo TIB imesaini hati ya makubaliano (MoU) ya miaka minne na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa, kwa lengo la kuimarisha mifumo ya ufadhili wa maendeleo itakayochochea ukuaji wa uchumi jumuishi na endelevu nchini.

Hafla ya utiaji saini imefanyika Machi 17, 2026, jijini Dar es Salaam katika ofisi za Benki ya Maendeleo TIB. Ushirikiano huo unatarajiwa kufungua fursa mpya za kuibua na kuendeleza miradi bunifu yenye tija, pamoja na kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo TIB, Deogratius Kwiyukwa, amesema maeneo yatakayopewa kipaumbele ni pamoja na nishati jadidifu, maendeleo ya biashara ndogo na za kati (SMEs), uchumi wa buluu, pamoja na miradi inayoongozwa na vijana, huku akisisitiza kuwa ushirikiano huo unaakisi dhamira ya pamoja ya kuharakisha maendeleo endelevu nchini, huku benki hiyo ikiendelea kutoa mitaji ya muda mrefu na suluhisho bunifu za kifedha kwa ajili ya kuchochea uwekezaji katika sekta muhimu za uchumi.

Kwiyukwa ameongeza kuwa makubaliano hayo yanaonesha kuimarika kwa imani ya washirika wa maendeleo wa kimataifa kwa uwezo wa Benki ya Maendeleo TIB katika kubuni, kuandaa na kutekeleza miradi yenye athari chanya kwa uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa UNDP, Shigeki Komatsubara, amesema ushirikiano huo unaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na juhudi za serikali za kuleta mageuzi ya kiuchumi endelevu, kuimarisha uwekezaji, na kulinda rasilimali za mazingira.

Ameeleza kuwa hatua hizo zinaendelezwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ambapo serikali imeendelea kusukuma mbele mageuzi ya kiuchumi, kukuza maendeleo endelevu, na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati unaoongeza ushindani wa Tanzania katika uchumi wa kimataifa, hata hivyo Tanzania imeendelea kuonesha mwelekeo chanya katika kuimarisha ustahimilivu wa uchumi, kukuza maendeleo endelevu, na kudumisha amani na utulivu wa kikanda.

Aidha, Komatsubara amesisitiza kuwa ushirikiano na taasisi za kifedha za kitaifa kama Benki ya Maendeleo TIB ni muhimu katika kuongeza athari za miradi ya maendeleo, huku alibainisha kuwa UNDP inatambua dhamira ya Tanzania katika kuendeleza maendeleo endelevu, kulinda mazingira, na kuimarisha uthabiti wa uchumi.

Kupitia makubaliano hayo, pande zote zinalenga kuanzisha mifumo bunifu ya ufadhili itakayochochea ukuaji jumuishi, kuongeza ustahimilivu wa kiuchumi, na kupanua fursa za maendeleo kwa jamii.

Kwa ujumla, hati hiyo ya makubaliano imeweka msingi wa utekelezaji wa miradi ya pamoja, ushirikiano wa kitaalamu, pamoja na uhamasishaji wa rasilimali kwa lengo la kuharakisha miradi yenye athari kubwa za maendeleo, kuimarisha uwezo wa jamii, kuunda ajira kwa vijana, na kuchangia mustakabali endelevu wa uchumi wa Tanzania.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *