ARUSHA: Serikali imewataka wakurugenzi wa bodi za kampuni ambazo ina umiliki wa hisa chache kuhakikisha uwekezaji huo unaleta matokeo yanayopimika kwa taifa na wananchi.
Wito huo umetolewa na Naibu Waziri katika Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Dk. Pius Chaya, wakati akifunga mkutano wa siku tatu wa wakurugenzi wa kampuni zenye hisa chache za Serikali (MIF 2026), uliohitimishwa Machi 18, 2026 jijini Arusha.
Chaya alisema uongozi wa kampuni hizo unapaswa kuzingatia utendaji unaopimika, akisisitiza kuwa uwekezaji wa Serikali lazima utoe thamani inayoonekana na yenye tija.
“Matarajio ni wazi kila kampuni ambayo Serikali ina hisa chache lazima izalishe thamani inayopimika kwa Serikali na wananchi,” alisema.
Aliongeza kuwa wakurugenzi wanapaswa kwenda zaidi ya usimamizi wa kawaida na kuhakikisha kampuni hizo zinachangia kikamilifu katika maendeleo ya taifa, huku akionya dhidi ya utendaji usiofikia matarajio katika kipindi ambacho nchi inalenga ukuaji wa uchumi.
Serikali pia imezitaka bodi kulinda na kukuza thamani ya hisa zake ili kuhakikisha uwekezaji wa umma unaendelea kuimarika.
Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, alisema mkutano huo umeimarisha majadiliano kuhusu uwajibikaji na nidhamu ya kimkakati katika usimamizi wa uwekezaji wa Serikali.
Alisema Ofisi ya Msajili wa Hazina itaendelea kusimamia kampuni hizo ili kuhakikisha zinatoa faida endelevu na kuchangia ajenda ya maendeleo ya muda mrefu ya Tanzania.
Mkutano huo uliwaleta pamoja wakurugenzi na watendaji wa kampuni mbalimbali kujadili mbinu za kuboresha utawala bora, kuongeza ufanisi na kuoanisha mikakati yao na vipaumbele vya taifa.
