KATIBU Mkuu Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji anayeshughulikia Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dk. Tausi Kida amewataka watafiti nchini kuelekeza tafiti zao katika kutatua changamoto halisi za kiuchumi na kijamii ili kuchochea maendeleo jumuishi na endelevu.
Akizungumza jijini Dodoma wakati akifungua kikao kazi cha wadau wa utafiti, Kida amesema Serikali inalenga kuhakikisha maamuzi ya sera na mipango ya maendeleo yanajengwa juu ya ushahidi wa kitaalamu unaotokana na tafiti zenye ubora na tija kwa taifa.
Amesema kupitia Tume ya Taifa ya Mipango, Serikali inaandaa mwongozo maalum wa tafiti utakaosaidia kuimarisha uratibu, kuongeza ubora na kuhakikisha matokeo ya tafiti yanatumika moja kwa moja katika kuboresha sera, kuongeza tija ya uchumi na kuvutia uwekezaji.

Kida amesema agenda ya utafiti wa taifa imejikita katika maeneo muhimu ikiwemo utawala bora, mageuzi ya uchumi, maendeleo ya rasilimali watu, mazingira na mabadiliko ya tabianchi pamoja na mienendo ya idadi ya watu. Ameeleza kuwa lengo ni kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinatoa majibu ya changamoto za maendeleo ya taifa. SOMA: Kihenzile akoshwa uwekezaji bandari ya Durban
Aidha, amesisitiza umuhimu wa tafiti kuwa na matokeo yanayoonekana kwa wananchi kwa kuongeza ajira, tija na ustawi wa jamii. Pia amehimiza ushirikiano kati ya Serikali, vyuo vikuu, taasisi za utafiti na sekta binafsi ili kuhakikisha tafiti zinachangia kikamilifu katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya taifa.