DAR ES SALAAM: Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Mwenda amesema TRA itaendelea kuwezesha biashara kwa kampuni kutoka nchini China na kushirikiana nayo katika masuala ya kodi huku akionya kampuni na wafanyabiashara wanaojihusisha na ukwepaji wa kodi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Machi 23.2026 wakati wa Mkutano wa Kikodi kwa wafanyabiashara wa China wanaoendesha shughuli zao nchini, Kamishna Mkuu Mwenda amesema TRA inatambua na kuthamini mchango wa wafanyabiashara hao pamoja na Kampuni kutoka China katika suala zima la ulipaji kodi na kuwaonya wachache wanaofanyaa udanganyifu.

Katika mkutano huo ambao pia ulihudhuriwa na Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian Kamishna Mkuu Mwenda amesema TRA itaendelea kuwasaidia wafanyabiashara hao ili waendelee kufanya biashara kwa haki na utulivu kwa kufuata sera na sheria za kodi zilizopo chini ya Mamlaka hiyo.

“TRA haina ugomvi na wafanyabiashara wa China waliopo nchini, ila ina ugomvi na wafanyabiashara wanaokwepa kodi, yeyote yule anayekwepa kodi ndani ya nchi yetu iwe kutoka China au taifa lolote lile huyo ana ugomvi na sisi,” amesema Mwenda.

Aidha, amesema ili kujenga mfumo wa kodi tabilifu, unaotenda haki, wa kisasa na unaoondoa usumbufu TRA imeanza kutekeleza baadhi ya mapendekezo 284 ya Kamati ya mapitio ya kodi ya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ambayo hayahitaji mabadiliko ya sheria yanayohusiana na usimamizi ili kuendelea kurahisisha zaidi mazingira ya ulipaji wa kodi nchini.

Pia amesema TRA itaendelea kutoa elimu ya kodi kwa wafanyabiashara hao na kuwasajili ambao bado hawajasajiliwa kwenye mifumo ya kodi kwa lengo la kuongeza wigo huku ikichukua hatua kwa wile wanaokwepa kodi.

Kwa Upande wake Balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian mbali na kupongeza ushirikiano wa muda mrefu uliopo baina ya Tanzania na China, amesema wataendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara pamoja na wawekezaji wa China waliopo nchini kuhusu umuhimu wa ulipaji Kodi kwa maslahi ya pande zote mbili.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *