MOROGORO: KAMISHNA Jenerali wa Uhamiaji, Dk Anna Makakala amesema mafanikio ya idara hiyo yanatengemea kwa kiasi kikubwa nidhamu, uadilifu na uweledi wa watumishi wake

Dk Makakala amesema hayo leo Machi 24, 2026 katika hotuba ya ufunguzi wa mkutano mkuu wa siku mbili wa Tawi la Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania ( TUGHE ) la idara hiyo unaoambatana na uchaguzi wa viongozi wa wapya wa tawi hilo uliofayika mjini Morogoro.

Hotuba hiyo ilisomwa kwa niaba yake na Naibu Kamishna wa Uhamiaji ambaye pia ni  Mkuu wa Uhamiaji wa Mkoa wa Morogoro, Elizabeth Gabriel Lukuwi.

Dk Makakala amesema serikali kupitia mamlaka husika inaendelea kutambua na kufanyiwa kazi changamoto inayohusu ajira mpya kwa kuzingatia taratibu mahitaji halisi ya taasisi na upatikanaji wa rasilimali fedha.

Kamishna Jenerali wa Idara hiyo pia amehimiza kutumia rasilimali zilizopo kwa ufanisi mkubwa kwa kuzingatia nidhamu, uwajibikaji na ubunifu katika utendaji wa kazi za kila siku .

Dk Makakala amesema kila mmoja ana nafasi ya kuchangia maendeleo ya taasisi hiyo pamoja na taifa kwa ujumla kupitia utekelezaji makini katika majukumu yake.

Amesema kumekuwa na mchango mkubwa unaotokana na kuwepo TUGHE Tawi la Idara ya Uhamiaji katika kulinda na kutetea maslahi ya wafanyakazi.

Dk Makakala amesema vyama vya wafanyakazi ni nguzo muhimu katika kuimarisha ustawi wa watumishi na kuleta uwiano mzuri kati ya wafanyakazi na mwajiri.

Akijibu risala ya Tawi la Tughe la Idara hiyo kuhusu upungufu wa  watumishi katika kada mbalimbali  za kiraia amesema kuwa anatambua  changamoto hiyo ipo na inaathiri ufanisi wa utendaji wa kazi.

“Menejimeti nzima ya Idara ya Uhamiaji tunaendelea kuthamini mchango wa kila mtumishi na tunaendelea kushirikiana katika kuboresha mazingira ya kazi kadri ya uwezo uliopo,“ amesema Dk Makakala.

Kwa upande wake Katibu wa Tawi la  Tughe Idara ya Uhamiaji, Francis Katawa ameeleza kwenye hotuba yake kuwa kumekuwepo na ushirikiano na mwajiri katika masuala mbalimbali yakiwemo ya uboreshaji wa maslahi ya watumishi na kimaendeleo.

Katawa amesema licha ya mafanikio yaliyopo, Idara ya Uhamiaji kwa sasa inakabiliwa na upungufu mkubwa wa watumishi raia katika kada mbalimbali muhimu.

Katibu huyo amesema kuwa upungufu huo umetokana na sababu mbalimbali ikiwemo watumishi kustaafu, kuhama kwenda taasisi nyinine na baadhi yao kufariki dunia.

Hivyo ameomba,Serikali kupitia mamlaka yake awasaidie kuidhinisha ajira mpya ili kujaza pengo ililipo hususani katika kada ya wahasibu na wakaguzi wa hesabu  za ndani , watumishi sekta ya afya  wauguzi na madaktari kwa ajili ya kituo cha afya kilichoanzishwa Raphael Kubaga mkoani Tanga .

Katawa ametaja  eneo lingine ni Watunza kumbukumbu na nyaraka , waandishi waendesha ofisi kwa ajili ya utendaji wa kazi za kila siku  pamoja na madereva .

“Upatikanaji wa watumishi hao kutasaidia kwa kiasi kikubwa  utendaji wa kazi kuwa ni kuingo kikubwa cha kuongeza ufanisi , kuimarisha uwajibikaji na kuboresha uhai wa chama “ amesema Katawa.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *