Maadhimisho ya Siku ya Afya Duniani 2026 yamekuja na wito mzito kwa Watanzania kusimama na sayansi ili kulinda afya na kujenga mustakabali bora, huku Shirika la Afya Duniani (WHO) likisisitiza kuwa ushahidi wa kisayansi ndio nguzo ya maendeleo ya sekta ya afya.
Kaulimbiu ya mwaka huu, “Pamoja kwa Afya; Simama na Sayansi,” inalenga kuhamasisha matumizi ya ushahidi katika kufanya maamuzi, kuimarisha mifumo ya afya na kukabiliana na changamoto zinazoibuka ikiwemo magonjwa ya mlipuko na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Kwa mujibu wa WHO, sayansi imekuwa na mchango mkubwa katika kuokoa maisha nchini Tanzania kupitia huduma kama chanjo, uchunguzi wa magonjwa, pamoja na mifumo ya ufuatiliaji wa magonjwa. Hatua hizi zimewezesha kuboreshwa kwa huduma za afya na kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika.
Taasisi za utafiti nchini zimetajwa kuwa nguzo muhimu katika mafanikio hayo. Taasisi kama Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Taasisi ya Afya ya Ifakara (IHI), Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA) zimekuwa mstari wa mbele kuzalisha ushahidi unaosaidia kuboresha sera na huduma za afya.
Matokeo ya matumizi ya sayansi yanaonekana wazi, ikiwemo kupungua kwa vifo vya watoto chini ya miaka mitano, pamoja na kuboreshwa kwa huduma za uzazi salama na upasuaji.
Tafiti zinaonyesha kuwa matumizi ya mbinu za kisayansi katika huduma za afya yamechangia kupunguza maambukizi baada ya upasuaji na vifo vya mama wakati wa kujifungua.
Aidha, WHO imeeleza umuhimu wa mbinu ya “Afya Moja” (One Health) inayounganisha afya ya binadamu, wanyama na mazingira, hususan katika kukabiliana na magonjwa yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na changamoto za mazingira.
Hata hivyo, changamoto kama upotoshaji wa taarifa za afya mitandaoni bado zinaathiri juhudi hizi. WHO imetoa wito kwa wananchi, wataalamu wa afya na waandishi wa habari kusambaza taarifa sahihi na zinazotegemea ushahidi.
Mratibu wa Kuimarisha Mifumo ya Afya (HSS), Dk Thomas Fedjo Tefoyet akizungumza kwa niaba ya Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania, Dk Alex Gasasira wakati wa maadhimisho ya Siku ya Afya Duniani yaliyokuwa na kaulimbiu: “Kwa pamoja, tutumie sayansi kwa manufaa ya wote.”
Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu ya Afya kwa Umma kutoka Wizara ya Afya, Dk Rahma Hingora anasema Serikali kwa kushirikiana na WHO inaendelea kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa kuibeba sayansi katika kulinda afya, akihusisha juhudi hizo na kaulimbiu ya mwaka ya “One Health” inayounganisha afya ya binadamu, wanyama na mazingira.
Kwa mujibu wake, magonjwa ya mlipuko kama Marburg Virus Disease na Mpox yanaonesha umuhimu wa ushirikiano huo, kwani mengi hutokana na mwingiliano kati ya binadamu, wanyama na mazingira.
Mkurugenzi wa Kukuza na Kuratibu Tafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu Tanzania, Dk Nyanda Ntinginya, anasema taasisi hiyo imeendelea kuzalisha ushahidi wa kisayansi kwa zaidi ya miongo minne na nusu ili kusaidia kuboresha sera na mifumo ya afya nchini.
Anasema NIMR inashirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi katika kufanya tafiti na kutafsiri matokeo yake ili yaweze kutumika katika kufanya maamuzi sahihi ya kiafya.
Naye Mkurugenzi wa Kiufundi wa Mradi wa Usalama wa Afya Duniani kutoka CIHEB Tanzania, Dk Siril Kullaya, anasema takribani asilimia 60 hadi 70 ya magonjwa ya mlipuko yanatokana na wanyama na mazingira.
Anasisitiza kuwa matumizi ya mkakati wa “Afya Moja” yanawezesha kugundua na kudhibiti magonjwa mapema kabla hayajaenea kwa binadamu, huku akibainisha kuwa ushirikiano kati ya sekta za afya ya binadamu, mifugo na mazingira ni muhimu katika kukabiliana na changamoto hizo.
“Afya na uchumi vinaenda pamoja. Tukishirikiana vizuri kama Taifa, tutaimarisha usalama wa afya na kuchochea maendeleo ya kiuchumi,” anasema Dk Kullaya.
Akizungumza kupitia ujumbe wake rasmi, Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Dk Mohamed Janabi anasema kaulimbiu ya mwaka huu, inaakisi mchango mkubwa wa tafiti za kisayansi katika kuokoa maisha na kuboresha huduma za afya duniani.
Anasema maendeleo ya kisayansi yamewezesha kupatikana kwa kinga bora, matibabu madhubuti na kuongeza umri wa kuishi kwa wananchi, huku Afrika ikiwa mstari wa mbele katika baadhi ya mafanikio hayo.
“Wanasayansi wa Afrika, taasisi na jamii zimekuwa na mchango mkubwa katika kukabiliana na changamoto za kiafya. Mfano ni maendeleo ya haraka ya chanjo za Ebola wakati wa milipuko ya magonjwa Afrika Magharibi na Kati,” anasema.
Anaongeza kuwa uwezo wa uchunguzi wa vinasaba (genomic sequencing) nchini Afrika Kusini uliwezesha kubainika mapema kwa aina mpya za virusi vya UVIKO-19, hatua iliyosaidia dunia kuchukua tahadhari mapema.
Anasema jitihada za afya ya umma zinazotegemea ushahidi wa kisayansi zimeleta mafanikio makubwa, hata hivyo, amebainisha kuwa bado Afrika inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo magonjwa sugu, milipuko mipya ya magonjwa na mifumo dhaifu ya afya.
Anaeleza kuwa mkakati wa Afya Moja unaohamasisha ushirikiano kati ya sekta mbalimbali umesaidia nchi nyingi za Afrika kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa, tathmini ya hatari na mwitikio wa dharura za kiafya.
Pamoja na mafanikio hayo, bado kuna upungufu wa fedha za utafiti, mifumo ya ufuatiliaji isiyo imara na udhaifu katika mifumo ya tahadhari za mapema.
Kwa sasa, nchi 46 za Afrika zimeandaa mipango ya kitaifa ya usalama wa afya, huku nchi zote wanachama zikiwa na mikakati ya kukabiliana na usugu wa dawa dhidi ya vimelea.
Pamoja na mafanikio hayo, bado kuna upungufu wa fedha za utafiti, mifumo ya ufuatiliaji isiyo imara na udhaifu katika mifumo ya tahadhari za mapema.
WHO imezitaka Serikali za Afrika kuongeza uwekezaji wa ndani katika sayansi na ubunifu, huku ikiwahimiza washirika wa kimataifa kuunga mkono juhudi zinazoongozwa na Afrika kwa usawa na kuongeza upatikanaji wa teknolojia na maarifa.
“Ubunifu wa kisayansi unapaswa kuwafikia wote. Ugunduzi ambao hauwafikii wanaouhitaji zaidi bado ni kazi ambayo haijakamilika,” anasisitiza Dk Janabi.
Kwa ujumla, ujumbe wa mwaka huu unasisitiza kuwa kila mmoja ana nafasi ya kuchangia kwa kuamini sayansi, kutumia ushahidi na kushiriki katika kujenga jamii yenye afya bora.
WHO imezitaka taasisi za afya na watafiti nchini kuimarisha matumizi ya sayansi ya utekelezaji ili kuboresha huduma za afya na kuleta matokeo chanya kwa wananchi.
Akizungumza kwa niaba ya Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania, Dk Alex Gasasira, Dk Thomas Fedjo Tefoyet, Mratibu wa Kuimarisha Mifumo ya Afya (HSS) anasema mafanikio ya afya yanategemea si tu kugundua suluhisho, bali jinsi yanavyotekelezwa katika mazingira halisi ya jamii.
Anasema taaluma za utafiti wa utekelezaji, utafiti wa uendeshaji na utafiti wa vitendo zina mchango mkubwa kwa kuwa zinajibu maswali muhimu kama “nini kinafanya kazi, wapi, kwa nani na kwa namna gani.”
“Hata kama utafiti wa msingi ni muhimu, haukidhi mahitaji yote. Tanzania ina nafasi kubwa ya kufanya vizuri zaidi kwa kuingiza ushahidi moja kwa moja kwenye mifumo ya huduma za afya,” anasema.
Anaeleza kuwa matumizi sahihi ya takwimu katika kupanga huduma, tathmini za ubora na uwezo wa wataalamu kubadilisha afua kulingana na mazingira yao ni miongoni mwa mambo yatakayosaidia kuongeza ufanisi wa sekta ya afya.
Hata hivyo, anasema bado kuna changamoto kadhaa zikiwemo usambazaji hafifu wa matokeo ya tafiti, upungufu wa rasilimali, pamoja na mifumo isiyoratibiwa vizuri ya takwimu.
Anataja pia hitaji la taasisi kama SUA na NIMR kuongeza juhudi katika tafiti za magonjwa yanayojitokeza na kurejea, pamoja na magonjwa yaliyopuuzwa na afya ya akili kwa vijana.
WHO inaendelea kuwahimiza watafiti vijana na wahudumu wa afya walioko mafunzoni kutambua kuwa nchi yao inahitaji utaalamu wao wa kisayansi na ubunifu wao. WHO itasimama bega kwa bega na Serikali ya Tanzania na inathibitisha upya dhamira yake ya kushirikiana ili kuhakikisha kuwa sayansi inanufaisha wananchi wote.