DAR ES SALAAM: Wataalamu wa afya kutoka vituo mbalimbali nchini wanatarajiwa kunufaika na mafunzo maalumu yatakayofanyika kwa wiki moja jijini Dar es Salaam, yakilenga kuboresha uwezo wa kufanya maoteo sahihi ya dawa na hivyo kupunguza changamoto ya upungufu wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Hatua hiyo imekuja kufuatia utafiti wa utekelezaji wa ugawaji wa dawa ulioonesha kuwepo kwa mapungufu katika mchakato wa maoteo, hali inayochangia kukosekana kwa dawa muhimu kwa wakati katika baadhi ya maeneo.

Akizungumza leo Aprili 20, katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Elimu Endelevu na Mafunzo ya Kitaaluma kutoka Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), Profesa Raphael Sangeda amesema lengo kuwawezesha wataalamu hao kuongeza ufanisi na usahihi katika kupanga mahitaji ya dawa kulingana na matumizi halisi.

Amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapatiwa mbinu bora za kitaalamu zitakazosaidia kuboresha mifumo ya ugavi wa dawa, kupunguza upotevu na kuhakikisha huduma bora za afya zinapatikana kwa wananchi bila kukwama kutokana na ukosefu wa dawa.

“Mwisho wa mafunzo haya wataalamu wataondoka wakiwa wamesheheni elimu ambayo itaenda kuwasaidia kuboresha huduma katika sehemu mbalimbali wanazofanyia kazi,” amesema Prof Sangeda.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *