
Arusha. Vijana wabunifu wameanza kutumia mabaki ya nywele za binadamu kutoka saluni mbalimbali kuzalisha mbolea hai, hatua inayosaidia kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi na uchafuzi wa mazingira.
Nywele hizo, ambazo mara nyingi hutupwa bila matumizi, sasa zimekuwa chanzo cha mbolea asilia inayosaidia wakulima kuboresha rutuba ya udongo bila kutumia kemikali zenye madhara kwa muda mrefu.
Hayo yamesemwa jana Jumamosi, Mei 9, 2026, na Ojung’u Laizer, mwanzilishi mwenza wa Kampuni ya Cutoff Recycle, wakati wa ugawaji wa ruzuku kwa kampuni za vijana wabunifu wanaotekeleza miradi ya kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi.
Laizer amesema kampuni yake inakusanya taka za nywele kutoka saluni na kuzibadilisha kuwa mbolea hai.
Ameongeza kuwa lengo lao ni kusaidia wakulima wadogo kupitia maduka ya pembejeo huku wakipunguza matumizi ya mbolea za kemikali zinazoweza kuathiri afya ya binadamu na udongo.
Laizer amesema fedha walizopata Sh12.5 milioni zitasaidia kukamilisha ujenzi wa kiwanda chao kilichopo Arusha, hatua itakayowawezesha kuongeza uzalishaji na kufikia masoko ya ndani na nje ya nchi.
“Tunatarajia kuongeza uwezo wa uzalishaji ili kuhudumia soko la Tanzania na pia masoko ya kimataifa kama India, China na Japan,” amesema.
Kampuni hiyo ilianza mwaka 2024 na sasa inakusanya nywele kutoka Arusha, Dar es Salaam na Kilimanjaro. Wanatarajia kuzalisha tani 40 za mbolea kavu na lita 7,500 za mbolea ya kioevu kwa kila mzunguko wa uzalishaji, huku na kuwa na vituo viwili vya ukusanyaji.
Aneth Mutembei, mwanzilishi wa Kampuni ya Nishati Eco Solutions ya Dar es Salaam, anazalisha mkaa mbadala kutokana na taka za kilimo kama vifuu vya nazi na maganda ya miwa.
Mkaa huo unalenga kupunguza ukataji miti na kuchangia nishati safi ya kupikia kwa kaya, shule na taasisi mbalimbali.
“Mkaa wetu unasaidia kupunguza ukataji miti na pia gharama za nishati kwa jamii. Tunabadilisha taka kuwa bidhaa yenye thamani,” amesema Mutembei.
Aidha, majivu yanayotokana na mkaa huo amesema hutumika kurutubisha udongo, hivyo kuchangia kilimo endelevu.
Mutembei amesema ruzuku walizopata zitasaidia kupanua eneo la uzalishaji, ambalo kwa sasa lina uwezo wa kuzalisha tani tano kwa wiki, na wanapanga kufikia tani 100 kwa wiki.
“Tumejifunza jinsi ya kuboresha ubora wa bidhaa zetu na kuongeza uwezo wa soko, jambo lililosaidia ukuaji wa biashara yetu,” amesema.
Joshua Silayo, Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi isiyo ya kiserikali ya Anza Entrepreneurs, amesema inawalenga vijana wajasiriamali katika sekta ya mazingira.
Silayo amesema mradi wa Regenerative Economy Accelerator Tanzania, ulioanza Agosti 2025, ulianza na washiriki 135 na kubaki 20, kati yao, wamo watano waliopata ruzuku ya Sh62.5 milioni na kila mmoja amepewa Sh12.5 milioni.
“Tunataka kuona vijana wanageuza changamoto za mazingira kuwa fursa za kiuchumi zinazowezesha ajira na kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi,” amesema Silayo.
Mosses Pesha, Katibu Tawala Msaidizi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Mkoa wa Arusha, amesema Serikali inaunga mkono jitihada za taasisi zinazosaidia vijana kuanzisha biashara rafiki kwa mazingira.
“Programu kama hizi zinasaidia kupunguza ukosefu wa ajira na kuongeza uelewa wa utunzaji wa mazingira. Tunaishukuru taasisi hii na wadau wake kwa kuwawezesha vijana kubadili changamoto za mazingira kuwa fursa za maendeleo,” amesema Pesha.
Ameongeza kuwa wadau wengine wanapaswa kuendelea kuwekeza katika miradi ya vijana ili kusaidia Taifa kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi na kukuza uchumi.