
Nchini Mali, vijiji vitano katika mkoa wa Bandiagara, katikati mwa nchi, vimeshambuliwa siku ya Alhamisi alasiri, Mei 21, 2026. Kundi linalodai kuunga mkono Uislamu na Waislamu (JNIM), linalohusishwa na Al Qaeda, limedai kuhusika na mashambulio haya, lakini halikutoa hesabu ya majeruhi. Vyanzo vilivyowasiliana na RFI vimeripoti vifo vya watu zaidi ya ishirini. Wakazi wengi wametoroka vijiji vyao.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Na timu ya wahariri ya RFI ya Mandinka na Fulfulde huko Dakar
JNIM ilishambulia kwa wakati mmoja, kati ya saa 11 na 12 jioni, vijiji vya Logo, Soulakanda, na Dimbal, katika wilaya ya Dimbal, na vile vijiji vya Ogossagou na Kouroundé, katika wilaya ya Bankass. Mapigano yalihusisha wapiganaji wa kijihadi dhidi ya wawindaji wa jadi wa Dozo, ambao hupigana katika safu ya jeshi, au hata hutoa ulinzi katika baadhi ya maeneo ambapo hakuna wanajeshi wa serikali.
Vyanzo vilivyowasiliana na RFI—maafisa waliochaguliwa wa eneo hilo, wanachama wa mashirika ya kiraia, na viongozi wa Dozo—vinaripoti takriban waathiriwa ishirini, wakiwemo wawindaji wa kitamaduni pamoja na raia. Kiongozi wa Dozo aliyewasiliana na RFI alilaani ukosefu wa jeshi kujibu mashambulizi haya, ambapo hakuna taarifa yoyote rasmi ambayo imetolewa. Jeshi halijazungumzi chochote kuhusiana na mashambulizi haya.
Hofu ya kutokea mashambulizi mapya
Wakazi wengi, wakihofia kutokea kwa mashambulizi zaidi, wamekimbilia maeneo ya jirani, hasa Bankass, ambapo idadi ya watu waliokimbia makazi yao tayari ni kubwa sana. Baadhi ya waliohojiwa walionyesha wasiwasi kuhusu mwitikio wa kibinadamu kwa wimbi hili jipya. Mashambulizi ya awali mapema mwezi huu katika eneo hilo tayari yaligharimu maisha ya watu zaidi ya hamsini.
Kufuatia mashambulizi haya, msemaji wa JNIM ametishia kushambulia vijiji vyenye vituo vya wawindaji wa Dozo na amekataa kuheshimu makubaliano ya ndani na wanajihadi.
