Vigogo wa zamani wa Temesa, CWT kortini kwa uhujumu uchumiVigogo wa zamani wa Temesa, CWT kortini kwa uhujumu uchumi

Dodoma. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) imewafikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma waliokuwa viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) pamoja na watendaji wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (Temesa).

Viongozi na watendaji hao wanatuhumiwa kwa makosa ya kuunda genge la uhalifu, uhujumu uchumi, utakatishaji fedha kwa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu Sh3.5 bilioni.

Miongoni mwa waliofikishwa mahakamani ni pamoja na aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa Temesa, Lazaro Kilahala ambaye Desemba 24, 2025, Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba aliagiza kufutwa kazi na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kutokana na tuhuma za ubadhirifu wa zaidi ya Sh2.5 bilioni.

Pia waliofikishwa mahakamani ni aliyekuwa rais wa CWT, Leah Ulaya, makamu wake, Suleimani Ikomba, aliyekuwa katibu mkuu, Maganga Japhet pamoja na Joseph Misalaba, Nashon Kidudu, Baraka Mbonalibha, Wambura Kihengu, Angelina Wambura na Kampuni ya Pyrate and Industries Company Limited.

Washtakiwa hao wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 14 ya uhujumu uchumi, ikiwemo kujipatia zaidi ya Sh2.2 bilioni kinyume cha sheria kati ya mwaka 2023 na 2024.

Akisoma mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Zabibu Mpangule, leo Jumatatu Mei 25, 2026 Jijini Dodoma Mwendesha Mashtaka Mwandamizi wa Serikali, Patrick Mwita amesema washtakiwa hao waliidhinisha matumizi ya fedha hizo kwa ajili ya ununuzi wa fulana na kofia kinyume na katiba ya CWT.

Mwita amedai kuwa washtakiwa hao pia walijipatia Sh1.3 bilioni kutoka Kampuni ya Pyrate and Industries Company Limited ili kupitisha zabuni ya ununuzi wa fulana na kofia hizo kinyume cha taratibu za chama.

Aidha, amewataja wakurugenzi wa kampuni hiyo, Wambura Kihengu na Angelina Wambura, kuwa wanakabiliwa na shtaka la kughushi nyaraka mbalimbali ili kuonyesha kampuni hiyo ilikuwa halali, huku wakifahamu kuwa kitendo hicho ni kosa kisheria.

“Watuhumiwa wengine watatu ambao ni Selemani Ikomba, Baraka Mbonalibha na Angelina Wambura bado wanaendelea kutafutwa ili waunganishwe na wenzao kwenye kesi hii,” alisema Mwita.

Kwa upande wa Temesa, waliofikishwa mahakamani mbali na Kilahala, ni Mathias Rutaguza, Sambayeti Magoko, Kennedy Manene, Peter Bongole, Clavery Busunzu, Mbisho Kibuti, Renatha Juma, Vincent Lutembuka, Michael Assey, Caesar Chambo, Nassor Igangule, Deus Matiku pamoja na Kampuni ya Kentra Tanzania Limited.

Washtakiwa hao wanashtakiwa kwa makosa tisa ikiwemo kughushi nyaraka za ununuzi wa vipuri vya magari na kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya Sh1.3 bilioni.

Mwita amesema watuhumiwa wawili, Mathias Rutaguza na Michael Assey, bado wanatafutwa ili waunganishwe katika kesi hiyo.

Aidha, ameeleza kuwa upelelezi wa kesi zote mbili bado unaendelea na kwamba kesi hizo zitaanza kusikilizwa rasmi mara baada ya taratibu za kisheria kukamilika.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mkuu Zabibu Mpangule amewaeleza washtakiwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi na utakatishaji fedha hadi ipokee kibali maalum kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).

“Endapo mahakama hii itapata kibali maalum, kesi hii itaanza kusikilizwa hapa au inaweza kuhamishiwa Mahakama ya Uhujumu Uchumi,” amesema Hakimu Mpangule.

Kesi hiyo iliahirishwa hadi Juni 8, 2026, huku washtakiwa wote wakirudishwa rumande kutokana na kesi hiyo kutokuwa na dhamana.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *