Skip to content
  • Thu. May 28th, 2026

  • CONTACT US
  • TERMS AND CONDITIONS
  • PRIVACY POLICY
  • LIGI KUU TANZANIA LIVE
IDHAA YA DUNIA

“Tulikuwa tunatafuta watoto wetu gizani” – Simanzi baada ya wanafunzi 16 kufa kwenye moto Kenya

Bymjombazecoder

May 28, 2026
“Tulikuwa tunatafuta watoto wetu gizani” – Simanzi baada ya wanafunzi 16 kufa kwenye moto Kenya“Tulikuwa tunatafuta watoto wetu gizani” – Simanzi baada ya wanafunzi 16 kufa kwenye moto Kenya

Iliyochapishwa Dakika 47 zilizopita

Muda wa kusoma: Dakika 5

Nje ya lango la shule ya Utumishi Girls Academy mjini Gilgil, baadhi ya wazazi walikuwa wamepiga magoti wakisali. Wengine walikuwa wakilia kimya kimya huku wakishikilia simu zao mikononi, wakingoja tu simu moja, simu ambayo ingeweza kuwaambia mtoto wao bado yuko hai.

Wanafunzi 16 wamethibitika kufariki baada ya moto mkubwa kuzuka katika bweni la shule hiyo usiku wa kuamkia Alhamisi, Mei 28, 2026, huku wengine wakijeruhiwa walipokuwa wakijaribu kujiokoa kupitia madirishani au kukimbia gizani.

Kwa Fredrick Aloo, taarifa hizo zilianza kwa simu ya ghafla alfajiri.

“Nilipowasha TV na kuona habari zile, moyo wangu ulisimama,” alisema.

Binti yake alikuwa amelala katika bweni lililokuwa likiungua.

“Ni kwa rehema za Mungu tu amepona. Mungu mwenyewe alimwokoa. Amepoteza kila kitu lakini maisha ni muhimu zaidi kuliko vitu. Vitu vinaweza kununuliwa tena, lakini huwezi kununua maisha.”

Moto ulianza wanafunzi wakiwa wamelala

A two-storey dormitory building. Burn marks can be seen coming up on the external walls of the first floor.

Chanzo cha picha, Reuters

Kwa mujibu wa polisi, moto huo ulianza majira ya saa saba usiku kwa saa za Afrika Mashariki na kuteketeza bweni lililokuwa na takribani wanafunzi 220.

Zaidi ya wanafunzi 800 walikuwa katika shule hiyo wakati wa tukio hilo.

Waziri wa Elimu Julius Ogamba alisema moto huo ulianzia katika ghorofa ya kwanza ya bweni hilo, ambalo liliharibiwa kabisa.

“Vikosi vya uokoaji vilifanikiwa kuuzima moto majira ya saa tisa usiku, lakini kufikia muda huo madhara makubwa yalikuwa tayari yametokea,” alisema alipofika eneo la tukio.

Alisema wanafunzi wataanza kukabidhiwa kwa wazazi na walezi wao huku uchunguzi ukiendelea kubaini chanzo cha moto huo.

Kamanda wa polisi Masoud Mwinyi alisema baadhi ya wanafunzi walikimbia kuelekea maeneo ya karibu kutokana na hofu na mshtuko.

“Maafisa wetu bado wanafuatilia maeneo ya karibu kwa sababu baadhi ya wanafunzi walikimbia usiku kutokana na hofu,” alisema.

Mwinyi alieleza tukio hilo kuwa “la kusikitisha na lenye kuumiza sana.”

“Hatukujua watoto wetu wako hai au wamekufa”

Nje ya shule, hali ilikuwa ya sintofahamu huku baadhi ya wazazi wakikimbia kutoka hospitali moja hadi nyingine kutafuta watoto wao.

Roselyn Rakamba alisema alipata taarifa hizo kupitia simu ya rafiki yake mapema asubuhi.

“Rafiki yangu alinipigia akaniuliza, ‘Mtoto yuko salama?’ Nikamuuliza mtoto gani? Ndipo akaniambia kuhusu moto wa shule ya Utumishi,” alisema.

Alisema alijaribu kuwasiliana na shule lakini hakukuwa na taarifa za kutosha.

“Niliambiwa kulikuwa na moto na baadhi ya watoto walikuwa wamejeruhiwa. Rafiki yangu aliyekuwa tayari shuleni alisema bado hawajawaona watoto.”

Dakika za kusubiri zilionekana kama saa nzima.

“Kabla sijafika shuleni, mwanangu alipata njia ya kunipigia simu. Nilikuwa nimechanganyikiwa sana lakini niliposikia sauti yake nilipata nafuu kidogo.”

Hata hivyo alisema furaha yake ilikuwa ya huzuni pia.

“Ninafuraha mwanangu yuko salama… lakini siwezi kusema nina furaha kabisa kwa sababu wazazi wengine wamewapoteza watoto wao. Katika shule hii tulikuwa kama familia moja. Tunaumia pamoja.”

Mama mwingine aliyekuwa akizungumza kwa machozi alisema familia yake ilikuwa imetafuta mtoto wao katika hospitali mbalimbali bila mafanikio.

“Tumekuwa hapa tangu saa kumi na mbili asubuhi. Hawatuambii mtoto wetu yuko wapi,” alisema.

“Tumetafuta hospitali zote za hapa karibu. Walimu hawatuambii chochote.”

A group of relatives stand in a circle in prayer.

Chanzo cha picha, Peter Njoroge / BBC

Wanafunzi waliruka kutoka dirishani kujiokoa

Wambui Nderitu, ambaye binamu yake ni mwanafunzi katika shule hiyo, alisema familia nyingi zilifika shuleni zikiwa katika hali ya hofu kubwa.

“Tulipoingia tuliambiwa tusimame kwenye foleni. Tulikuwa na wasiwasi mkubwa kwa sababu tulikuwa tumesikia baadhi ya wanafunzi wamefariki na wengine wako hospitalini.”

Alisema baadhi ya wanafunzi waliokuwa ghorofa ya juu walilazimika kuruka kutoka dirishani kujiokoa.

“Baadhi ya waliokuwa juu waliruka, ndiyo maana wameumia.”

Binamu yake alinusurika lakini alivunjika mguu.

“Nilimpata… yuko hai… lakini mguu wake umevunjika,” alisema.

Leah Serem, ambaye binti yake ni mwanafunzi wa mwaka wa mwisho katika shule hiyo, alisema alipata taarifa hizo akiwa nyumbani mjini Nakuru.

“Tulikuwa na hofu kwa sababu hatukujua watoto wetu walikuwa hai au wamefariki,” alisema.

Baadaye alimkuta binti yake akiwa salama.

“Nilifurahi sana na nikamshukuru Mungu.”

Binti yake alimweleza kuwa wanafunzi walikuwa wakigongana na kuamshana wakati moto ulipoanza.

“Tunawaombea wazazi ambao bado hawajawaona watoto wao. Tunawaomba Wakenya watuombeee huku chanzo cha moto kikichunguzwa,” alisema.

Satellite map showing the town of Gilgil in Kenya with surrounding roads, buildings, and farmland. A label marks “Utumishi Girls Academy” on the northeastern edge of the town. An inset map in the top left shows Kenya with Nairobi highlighted to indicate location. The main map labels “Gilgil” at the centre. The image is credited to Google with BBC branding.

Historia ya moto mashuleni Kenya

Waziri wa Mambo ya Ndani Kipchumba Murkomen, ambaye pia alifika shuleni humo, alituma salamu za pole kwa familia zilizopoteza watoto wao.

“Ni wakati wa hofu kubwa. Tunapothibitisha vifo vya wanafunzi 16 hadi sasa, naomba Wakenya wote tusimame pamoja na familia hizi kwa maombi na msaada,” alisema.

Aliwataka wananchi kuwa watulivu huku uchunguzi ukiendelea.

“Naomba watu wawe wavumilivu na waepuke kutoa taarifa za kubahatisha.”

Moto katika shule za bweni si jambo geni nchini Kenya.

Mwaka 2001, wanafunzi 67 walifariki katika shule moja eneo la Machakos baada ya bweni kuteketekea kwa moto, tukio ambalo bado linatajwa kuwa baya zaidi katika historia ya shule nchini humo.

Mwaka 2024, watu wasiopungua 21 walifariki katika moto mwingine ulioteketeza bweni katikati mwa Kenya.

Baada ya tukio hilo, tathmini ya Wizara ya Elimu ilibaini kuwa shule nyingi zilikuwa na mabweni yenye madirisha yenye nondo, milango michache ya kutokea na milango iliyokuwa ikifunguka kuelekea ndani, hali iliyokuwa ikihatarisha usalama wa wanafunzi wakati wa dharura.

Msongamano mkubwa wa wanafunzi mabwenini pia ulitajwa kuwa moja ya sababu zinazochangia idadi kubwa ya vifo wakati wa majanga ya moto.

Mwaka 2021, Wizara ya Elimu nchini Kenya ilisema kulikuwa na matukio 126 ya uchomaji moto mashuleni kati ya Januari na Novemba 2020 pekee.

Lakini nje ya lango la Utumishi Girls Academy mjini Gilgil, wazazi wengi hawakuwa wakifikiria kuhusu takwimu wala historia ya majanga ya moto mashuleni.

Walikuwa wakingoja tu kuona watoto wao wakitokea wakiwa hai.

Taarifa hii imechangiwa na waandishi mbalimbali wa BBC akiwemo Akisa Wandera, Basillioh Rukanga na Nairobi Thomas Mukwana

Maelezo zaidi kuhusu taarifa hii

Post navigation

‘Alikua mtu tofauti’: Jinsi kaka yangu mwigizaji wa Hollywood alivyogeuka na kuwa mtu mwenye chuki dhidi ya wanawake mitandaoni

By mjombazecoder

Related Post

IDHAA YA DUNIA

‘Alikua mtu tofauti’: Jinsi kaka yangu mwigizaji wa Hollywood alivyogeuka na kuwa mtu mwenye chuki dhidi ya wanawake mitandaoni

May 28, 2026 mjombazecoder
IDHAA YA DUNIA

Mzozo wa Iran: Kwanini Trump anatishia kuishambulia Oman?

May 28, 2026 mjombazecoder
IDHAA YA DUNIA RFI SWAHILI

Kenya: Wanafunzi 16 wafariki kwenye mkasa wa moto katika bweni lao

May 28, 2026 mjombazecoder

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recent Posts

  • Serikali yazindua mpango mafunzo ya uongozi
  • Utumishi Girls Academy: Mwanafunzi aliyenusurika mkasa wa moto asimulia alivyojiokoa: “Niliruka nje”
  • William Ruto akiri kwa hisia yeye na mkewe Rachel walimpoteza mwanao wa kwanza
  • Kenani kuanza ziara Kaskazini, CCM Kilimanjaro yaeleza sababu ya kurejea baada ya miaka 25
  • Tanzania cherishes digital transport platforms for transforming urban mobility

Recent Comments

  1. DandyHorse on Samia kutunukiwa shahada ya heshima Nigeria
  2. Dydaktyczny on Klabu ya Fountain Gate FC imethibitisha rasmi kumteua Fred Felix Minziro “Majeshi” kuwa Kocha Mkuu mpya, akichukua nafasi ya Moh…

Archives

  • May 2026
  • April 2026
  • March 2026
  • February 2026
  • January 2026
  • December 2025
  • November 2025
  • October 2025
  • September 2025
  • August 2025
  • June 2025
  • August 2024
  • July 2024
  • May 2023
  • June 2016

Categories

  • ASTV TANZANIA
  • CRI SWAHILI
  • DW SWAHILI
  • HABARI ZA KIPEKEE
  • HABARILEO
  • IDHAA YA DUNIA
  • ITVBONGO
  • LTV ENGLISH NEWS
  • MAGAZETI
  • MWANANCHI
  • MWANASPOTI
  • RFI SWAHILI
  • TRT SWAHILI
  • TUKO SWAHILI NEWS
  • TZSPORTS
  • Uncategorized

You missed

HABARILEO

Serikali yazindua mpango mafunzo ya uongozi

May 28, 2026 mjombazecoder
TUKO SWAHILI NEWS

Utumishi Girls Academy: Mwanafunzi aliyenusurika mkasa wa moto asimulia alivyojiokoa: “Niliruka nje”

May 28, 2026 mjombazecoder
TUKO SWAHILI NEWS

William Ruto akiri kwa hisia yeye na mkewe Rachel walimpoteza mwanao wa kwanza

May 28, 2026 mjombazecoder
MWANANCHI

Kenani kuanza ziara Kaskazini, CCM Kilimanjaro yaeleza sababu ya kurejea baada ya miaka 25

May 28, 2026 mjombazecoder

Proudly powered by WordPress | Theme: Newsup by Themeansar.

  • Home
  • CONTACT US
  • LIGI KUU TANZANIA LIVE
  • PRIVACY POLICY
  • TERMS AND CONDITIONS