Aliyekuwa mfuasi wa kundi la Red Army Faction (RAF) la Ujerumani amehukumiwa kifungo cha miaka 13 gerezani kwa kutekeleza vitendo vya ujambazi wa kutumia silaha kati ya mwaka 1999 na 2016.
Daniela Klette, mwenye umri wa miaka 67, alikamatwa hatimaye katika nyumba moja mjini Berlin mwaka 2024 baada ya zaidi ya miaka 30 akiwa mafichoni.Kesi yake ilianza kusikilizwa mwaka uliopita.
Wakili wake wa utetezi aliomba aachiliwe huru, lakini mahakama ya Verden, Lower Saxony, ilimkuta na hatia siku ya Jumatano kwa makosa ya ujambazi uliokithiri, kukiuka sheria za silaha, na makosa mengine yaliyotendeka katika kipindi cha miaka 17.
Kundi la RAF, ambalo pia lilijulikana kama “Baader-Meinhof Gang,” hatimaye lilivunjika baada ya kampeni ya mauaji, utekaji nyara na mashambulizi ya mabomu kuanzia miaka ya 1970 hadi mapema miaka ya 1990.
Mahakama ilielezwa kuwa Daniela Klette alihusika katika uporaji wa maduka makubwa na magari ya kubeba fedha pamoja na wafuasi wengine wawili wa zamani wa RAF, Burkhard Garweg na Ernst-Volker Staub, ambao bado hawajakamatwa.
Kesi hiyo ililenga matukio manane yawizi yaliyotokea kaskazini na magharibi mwa Ujerumani, yaliyoanza katika mji wa Duisburg mwezi Julai 1999, ambapo washambuliaji waliovaa barakoa walifika kwenye ATM kwa gari na kuwatishia walinzi kwa silaha na mabomu ya mkono, kisha wakatoroka na kiasi kikubwa cha fedha.
Shambulio la mwisho zaidi lilitokea Juni 2016, likihusisha gari la kubeba fedha lililokuwa karibu na mji wa Braunschweig. Wahalifu hao walitoroka na takriban euro milioni 1.4 (paundi milioni 1.2).
Daniela Klette alikamatwa Februari 2024, akiwa amejificha kwa kutumia jina la bandia na pasipoti ya nchi ya kigeni, na akiishi katika mtaa tulivu eneo la Kreuzberg.

(Feed generated with FetchRSS)
