
Hayo yamebainishwa katika ripoti mpya ya UNAIDS iliyotolewa leo ambayo inaonesha kuwa misaada ya maendeleo duniani ilipungua kwa asilimia 23 mwaka 2025, kikwa ni kiwango kikubwa zaidi kuwahi kurekodiwa, na kuathiri vibaya programu za VVU katika nchi maskini zenye mzigo mkubwa wa maambukizi.
Akizungumzia ripoti hiyo kutoka Geneva uswisi Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS, Winnie Byanyima amesema “Hakuna shaka kuwa huu ndio mtikisiko mkubwa zaidi katika mwitikio wa VVU tangu dunia ilipoamua kupambana na ugonjwa hu.”
Katika kipindi cha mwaka 2024 hadi 2025, huduma za upimaji wa VVU zilishuka kwa asilimia 22, huku matumizi ya dawa za kujikinga na maambukizi ya VVU (PrEP) yakipungua kwa asilimia 38 katika nchi 62 zilizowasilisha taarifa kwa UNAIDS.
Aidha, ufadhili wa kondomu umepungua kwa zaidi ya asilimia 90 katika baadhi ya maeneo.
Mafanikio yaliyopatikana yako hatarini
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, vifo vinavyotokana na UKIMWI vimepungua kwa asilimia 56 tangu mwaka 2010, huku maambukizi mapya yakishuka kwa asilimia 43. Hivi sasa watu milioni 32.1 kati ya milioni 40.9 wanaoishi na VVU wanapata matibabu.
Hata hivyo, karibu watu milioni 9 bado hawapati tiba, hali inayoongeza hatari ya kuongezeka kwa vifo na maambukizi mapya, hasa katika maeneo yanayotegemea ufadhili wa nje.
Ripoti hiyo pia inaonesha kuwa kila wiki wasichana 3,000 Barani Afrika Kusini, mwa Jangwa la Sahara wanaambukizwa VVU.
Kubanwa kwa haki za binadamu kunaongeza hatari
UNAIDS imeonya kuwa kuongezeka kwa sheria zinazoyabagua makundi yaliyo pembezoni kunawafanya watu wengi kuogopa kupima VVU au kutafuta matibabu.
“Magonjwa huenea kwa kasi zaidi pale ambapo haki za binadamu zinalindwa kwa kiwango cha chini. Kuporomoka kwa haki za binadamu na nafasi ya kiraia kuna athari kubwa kwa afya ya umma na mapambano dhidi ya VVU,” amesema Byanyima.
Wito wa kuimarisha uwekezaji
Ripoti hiyo inaeleza kuwa bado inawezekana kutokomeza UKIMWI kama tishio la afya ya umma ifikapo mwaka 2030 ikiwa nchi zitaongeza uwekezaji wa ndani na washirika wa maendeleo wataendelea kuunga mkono juhudi hizo.
UNAIDS imeonya kuwa kushindwa kuchukua hatua sasa kunaweza kufuta mafanikio ya miongo kadhaa ya mapambano dhidi ya UKIMWI.