Simba imeendeleza ubabe katika Ligi Kuu ya NBC baada ya leo Jumatano, Juni 17, 2026 kuichapa Mbeya City kwa bao 1-0 katika Uwanja wa Sokoine Mbeya.

Ushindi huo umeifanya Simba ipande kileleni mwa msimamon wa Lig ikifikisha pointi 64 na hivyo kuendelea kuweka hai matumaini yake ya kutwaa ubingwa.

Kwa upande mwingine matokeo hayo, yanazidi kuiweka Mbeya City katika hali ngumu zaidi kwenye ushindani wa kukwepa kushuka daraja ikibakiza mechi tatu za hukumu ikiwa ni dhidi ya Dodoma Jiji, Pamba Jiji na TRA United.

Shujaa wa Simba katika mechi ya leo ni Elie Mpanzu ambaye amefunga bao hilo pekee katika dakika ya 44 akimalizia pasi nzuri ya Clatous Chama.

Kwa kufunga bao hilo, Mpanzu anakuwa amefumania nyavu za wapinzani katika mechi tatu mfululizo, ambapo kabla alifunga dhidi ya Dodoma Jiji na Pamba Jiji.

Huo ni ushindi wa saba mfululizo kwa Simba kwenye Ligi Kuu tangu ilipotoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya Yanga, Mei 3 mwaka huu.

Baada ya kuingia kwa bao hilo, timu hizo zilionekana kushambuliana kwa zamu lakini ubao wa matokeo haukubadilika hadi filimbi ya kumaliza mchezo ilipopulizwa na refa Ahmada Simba kutoka Kagera, Simba ilifanikiwa kulinda bao lake.

Baada ya mchezo wa leo, kibarua kinachofuata kwa Simba ni mechi ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha, Jumamosi, Juni 20.

Mbeya City yenyewe ina kibarua cha mechi ya Ligi Kuu dhidi ya Pamba Jiji, Juni 24, katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *