Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, Mkataba wa Maelewano (MoU) wa kumaliza vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran haukuwa matokeo ya shinikizo au kulazimishwa, bali ni zao la ustahimilivu na nguvu ya taifa shupavu la Iran.

Amesema mapatano hayo, ambayo yanajulikana kama Mapatano ya Islamabad kutokana na upatanishi wa Pakistan, yamedhihirisha kuwa mazungumzo hufanikiwa pale tu upande wa pili unapoachana na tabia ya kulazimisha matakwa yake kwa taifa lenye ustaarabu kama Iran na kukubali haki za taifa hili. Kwa msingi huo, mkataba wa Islamabad umegeuka kuwa tangazo la kushindwa kwa Marekani.

Mohammad Bagher Qalibaf, siku ya Jumatano, tarehe 24 Juni 2026, katika mkutano wa 20 wa Umoja wa Mabunge ya Nchi Wanachama wa Shirika la Ushirikiano wa Kiislamu (PUIC) uliofanyika jijini Baku, Jamhuri ya Azerbaijan. Katika hotuba yake ameishukuru nchi mwenyeji wa kikao hicho na kusema: “Natoa rambirambi kwa mataifa ya Kiislamu kwa siku za kumbukumbu ya kuuawa shahidi kwa mjukuu wa Mtume Muhammad (SAW), Imam Hussein (AS) ambaye ni Bwana wa Mashahidi.” Amesema. Muharram ni mwezi unaotufundisha kuwa heshima na utukufu havipatikani kwa kusalimu amri, bali damu ndiyo inayoshinda upanga. Spika Qalibaf ameongeza kuwa: “Natumai kwa kushikamana na njia ya nuru ya Imam Hussein (AS), mazungumzo yetu ya leo yatakuwa na kheri kwa Umma wa Kiislamu.”

Spika wa Bunge la Iran ameongeza: “”Mkutano huu wa 20 wa Umoja wa Mabunge ya Nchi za Kiislamu unafanyika katika kipindi ambacho Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imepitia uvamizi mkali. Vita vya kulazimishwa vya siku arobaini vya Marekani na utawala wa Kizayuni dhidi ya Iran vilikuwa kitendo cha jinai.”

Ameongeza kkuwa: “Katika jinai hii ya wazi, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, maafisa kadhaa wa ngazi za juu wa kijeshi na kisiasa, na zaidi ya raia 3,000 wa Iran, ambao wengi wao walikuwa wanawake na watoto, waliuawa shahidi. Zaidi ya watu elfu thelathini walijeruhiwa na miundombinu ya viwanda, afya, elimu, nishati, usafirishaji, na maelfu ya vitengo vya huduma na makazi nchini Iran vililengwa na mashambulizi.”

Qalibaf amesisitiza: “Ustahimilivu wa kishujaa wa vikosi vya ulinzi na msimamo wa kishujaa wa wananchi mitaani, uliifanya Iran iweke gharama kubwa kwa Marekani na utawala ghushi wa Israel. Ustahimilivu huu uliotokana na imani, ndio uliokuwa sababu ya adui kukata tamaa ya kufikia malengo yake na kumlazimisha asalimu amri katika medani za mapambano na mazungumzo.”

Alikumbusha: “Vita hivi haikuwa tu mapambano ya kijeshi, bali ilikuwa ni jaribio lililopangwa la kubadilisha mizani ya kimkakati ya eneo na kulazimisha matakwa ya upande mmoja kwa taifa huru. Wasanifu wa uvamizi huu walidhani kuwa kupitia shinikizo la kijeshi, mzingiro, vita vya kisaikolojia, na vitendo vya kigaidi, wangeweza kulilazimisha taifa la Iran kurudi nyuma na kuandika upya milinganyo ya eneo hilo kwa faida yao.”

Spika wa Bunge amesema: “Kilichotokea kilikuwa kinyume kabisa na hesabu za waliopanga vita hivyo. Taifa la Iran lilionyesha kuwa zama za kulazimisha matakwa kwa mataifa huru zimekwisha, na mmeona jinsi dunia ilivyousifu ustahimilivu huu na ushindi huu.”

Qalibaf ameongeza: “Ingawa vita hivi vilisababisha gharama kubwa kwa taifa letu, lakini vilifichua ukweli wa kimsingi kwamba ustahimilivu na msimamo wa wananchi kama nguvu ya kweli, katika hali ngumu zaidi, huvuruga mahesabu ya wavamizi. Amani ya kudumu si zao la kusalimu amri, shinikizo, au udhalilishaji, bali ni zao la nguvu, heshima, na utukufu.”

Ameendelea kwa kusema: “Ushindi wa taifa la Iran unatoa ujumbe huu muhimu kwa Waislamu duniani kuwa, kulinda uhuru na heshima ya kitaifa kunategemea kuamini mafundisho ya Kiislamu yenye kujenga utu. Qur’ani inatufundisha kutokutenda dhuluma wala kukubali kudhulumiwa. Qur’ani inatuambia tuwe na nguvu kadiri tuwezavyo, Qur’ani inatufunza tusiwategemee wasioamini na inatuambia tushikamane na kamba ya Mwenyezi Mungu na tusitawanyike; na hiyo hiyo Qur’ani inatuambia kuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, kundi dogo linaweza kushinda maadui wakubwa, na inatoa dhamana kuwa mkiwa na imani ya kweli kwa Mwenyezi Mungu, mtashinda. Na taifa la Kiislamu la Iran kwa matendo yake ya Kiimani, limetekeleza maagizo haya ya Mwenyezi Mungu.”

Qalibaf amekumbusha kuwa: “Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, licha ya mateso na hasara zote ilizopata katika vita vya hivi karibuni, inasisitiza kanuni moja ya msingi; nayo ni kutanguliza mantiki kuliko nguvu, na kutanguliza ustahimilivu kuliko kusalimu amri.”

Spika wa Bunge amesisitiza: “Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inanyoosha mkono wa undugu na ushirikiano kwa nchi zote za Kiislamu.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *