- Mchungaji Victor Kanyari ameanzisha mchakato wa kisheria ili kutatua mzozo wa malezi unaohusisha watoto wake aliowapata na mke wake wa zamani, Betty Bayo
- Kasisi huyo mwenye utata alionyesha hasira kubwa baada ya kudai kuwa baba wa kambo wa watoto wake, Hiram Gitau almaarufu Tash, amekuwa akiwazuia watoto hao kuzungumza naye kupitia simu
- Mchungaji Kanyari pia alidai kuwa hapo awali amekuwa akiisaidia familia hiyo kifedha, lakini sasa yuko tayari kwa “vita” mahakamani ili kuhakikisha watoto wake wanapata akaunti zao binafsi za benki na yeye apate fursa stahiki ya kuwaona na kuwasiliana nao
Mchungaji Victor Kanyari amefunguka kuhusu kwenda mahakamani kutatua masuala yanayohusiana na watoto wake kufuatia mzozo wa malezi na mjane wa aliyekuwa mke wake wa zamani, Betty Bayo.

Source: UGC
Sakata hilo lilianza baada ya rafiki mkubwa wa Betty Bayo, Shiro Stuart, kujitokeza na madai mapya dhidi ya mjane huyo wa mwanamuziki marehemu, Hiram Gitau almaarufu Tash.
Alidai kuwa Tash alikuwa akiwatumia watoto hao na kuwaelekeza kile wanachopaswa kuwaambia watu waliokuwa wakiwasiliana nao ili kujua hali yao.
Baadaye, binti wa Betty Bayo, Sky, alijitokeza kwenye matangazo ya moja kwa moja ya TikTok kumtetea Tash na hata kumtaka Shiro aache kusambaza uvumi kuhusu baba yake wa kambo.
Kwa nini Mchungaji Kanyari anaenda mahakamani?
Kanyari alijiunga katika mjadala huo na kumkosoa Tash kwa namna anavyowashughulikia watoto hao. Pia alithibitisha kuwa watoto hao walikuwa nyumbani kwa wiki tatu kutokana na ada ya shule kutolipwa.
Akizungumza na wanablogu, Kanyari alithibitisha kuwa tayari ameanzisha hatua za kisheria na kudai kuwa watoto wake walionywa wasiongee naye kwa simu.
Pia alijibu maswali kuhusu kwa nini watoto wake hawaishi naye ilhali amenunua nyumba kubwa ya thamani ya KSh 90 milioni huko Runda kwa ajili yao.
“Walikuja kwenye nyumba mpya na wakaishi kwa takriban wiki moja, kisha yule mwanaume akaja akawachukua. Baadaye aliniambia niende kuwachukua, nami nikafanya hivyo kwa sababu, kama mnavyojua, sina uhasama naye. Simchukii. Hata hivyo, nilikasirika baada ya kugundua kuwa alikuwa akiwazuia kuzungumza nami kwa simu, ndiyo maana nimeamua kuwa sasa ni vita. Nilikuwa mpole, lakini sasa ni vita kwa sababu kuna mtu anataka hivyo, na lazima nimpe anachotaka,” alisema.
Kanyari pia alidai kuwa amekuwa akilipa kodi ya nyumba ya Tash pamoja na watoto hao na kudai kuwa binti yake, Sky, hana akaunti yake binafsi ya benki.
“Kulikuwa hata na wakati ambapo mimi ndiye nilikuwa nikimsaidia kulipa kodi ya nyumba wanamoishi. Pia nilikuwa nikilipa bili za umeme. Sina tatizo kufanya mambo kama hayo kwa sababu nimezoea. Hata kanisani kwangu ninasaidia wanaume wengi, na wao si wale wanaowatunza watoto wangu. Kuwaambia watoto wangu kwamba hawawezi kuzungumza nami kwa simu ni kutangaza vita dhidi yangu. Sijui wanachofanya, na hakuna anayejua kwa sababu familia yote ilifukuzwa, hata mama na dada zake Betty,” aliongeza.
Aliahidi kushiriki taarifa zaidi kutoka mahakamani huku akitarajia hatua za kisheria zitakazosaidia kutatua mgogoro huo unaozidi kushika kasi.
“Sasa watoto wangu wanaishi na mwanaume ambaye hata si baba yao. Tayari nimepeleka suala hili mahakamani, lakini sitafichua tarehe kwa sababu ni jambo nyeti. Hivi karibuni tarehe ya kesi itafika. Mimi ninachofanya ni kutekeleza wajibu wangu kama baba. Nitakapohitaji kuwa mkali nitakuwa mkali, na nitakapohitaji kuwa mpole nitakuwa mpole,” alisema zaidi.
Kanyari sasa anataka watoto wake wawe na akaunti zao binafsi za benki.
Pia alieleza sababu iliyomfanya kukataa kupokea fedha kutoka kwa Naibu Rais, Kithure Kindiki.
“Yule mwanaume hawezi kuwaonya wanapokosea kwa sababu si baba yao. Binti yangu hana akaunti yake binafsi ya benki, maana yake kila anachopata kinaenda kwa yule mwanaume. Ndiyo maana nilikataa fedha ambazo Kindiki alitoa. Nilisema akaunti mbili zifunguliwe, moja ya Dany na nyingine ya Sky, na fedha zote ziwekwe humo,” alisema.
Je, Tash alijibu tuhuma hizo?
Siku moja iliyopita, video iliyosambaa sana kwenye TikTok ilimuonyesha Tash akiwa hana wasiwasi wowote kuhusu drama ya kifamilia na lawama za umma zinazomkabili.

Source: TikTok
Mjane huyo amekuwa akichagua kukaa kimya hata wakati watu waliomzunguka walikuwa wakimshutumu na kutoa vitisho dhidi yake.
Badala ya kujibu ukosoaji unaoendelea, Tash aliendelea na maisha yake kawaida na alionekana akifurahia kula githeri pamoja na rafiki yake aliyekuwa akimuunga mkono.
Read ENGLISH VERSION
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.
Chanzo: TUKO.co.ke


