BAADA ya kufanikiwa kupanda daraja kushiriki Ligi Kuu Zanzibar msimu ujao, Raskazone imeendelea kufanya tathmini ya kikosi chake ili kuboresha maeneo yenye changamoto kuhakikisha timu inakuwa ya ushindani zaidi.

Wakati hayo yakifanyika, nyota wa kikosi hicho, Said Ali Mohammed, alibainisha kuwa, wao kama wachezaji wapo tayari kupokea maelekezo ya benchi la ufundi ili kufikia malengo yao.

Mchezaji huyo ameeleza kuwa, kikosi hicho kimepata uzoefu kupitia michezo mbalimbali iliyocheza, jambo ambalo litawasaidia kufanya vizuri msimu ujao wa Ligi Kuu ya Zanzibar.

Amesema, hiyo ndio sababu ya benchi hilo kufanya maboresho ya kikosi hicho kwa lengo la kuendana na kasi ya ushindani wa ligi baada ya kupanda daraja.

“Mimi pamoja na wachezaji wenzangu tutaendelea kujituma na kupambana kwa nguvu zote ili kuhakikisha tunailetea mafanikio klabu yetu na kuwapa furaha mashabiki wetu,” amesema.

Said amesema baada ya timu hiyo kumaliza ushiriki wake katika mashindano ya FA Unguja, amesisitiza kuwa pamoja na changamoto mbalimbali zilizojitokeza katika soka, mashabiki wanapaswa kuendelea kuiunga mkono timu yao.

Mbali na hilo, aliwashukuru mashabiki wa Raskazone kwa kuendelea kuiunga mkono timu hiyo katika nyakati zote, akieleza kuwa mchango wao ni muhimu katika safari ya maendeleo ya klabu.

Hata hivyo, aliwaomba mashabiki wa klabu hiyo wasikate tamaa kwani mpira una matokeo matatu kushinda, sare au kufungwa hivyo wamewaomba waendelee kuwa pamoja nao.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *