MBEYA: Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) imewahimiza wawekezaji kutumia fursa zilizopo Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya, ikisema eneo hilo lina uwezo mkubwa wa kuendeleza viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo yanayozalishwa kwa wingi.
Akizungumza wilayani humo, Meneja wa TISEZA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Fidelis Obanga, amesema mamlaka hiyo imeanza kutoa elimu kwa wawekezaji wanaojihusisha na uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa nje ya nchi ili wajisajili rasmi na kunufaika na vivutio vinavyotolewa na Serikali.
Amesema hatua hiyo inalenga kuwawezesha wawekezaji kupata huduma mbalimbali za uwekezaji pamoja na kuchochea ukuaji wa sekta binafsi, ambayo kwa mujibu wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inatarajiwa kuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi.

Obanga amesema Rungwe ni miongoni mwa wilaya zenye fursa nyingi za uwekezaji kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya biashara na chakula, huku akitaja parachichi, kakao, chai, ndizi na tangawizi kuwa mazao yenye uwezo mkubwa wa kuongeza thamani kupitia viwanda vya uchakataji.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Kilimo na Uvuvi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Adam Salumu, alisema pamoja na wilaya hiyo kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa parachichi nchini, bado kuna upungufu wa viwanda vya kuchakata mazao hayo pamoja na mazao mengine ya kilimo.

Amesema Serikali ya Wilaya imetenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji na inaendelea kuwakaribisha wawekezaji watakaowekeza katika viwanda vya uchakataji ili kuongeza thamani ya mazao na kuwainua wakulima kiuchumi.
Naye, Meneja wa Kampuni ya Kuza African Limited, Noel Kabuje, amesema kampuni hiyo imeendelea kutoa soko la uhakika kwa wakulima wa parachichi kwa kununua mazao yao na kuchangia maendeleo ya uchumi wa eneo hilo.

Kabuje amesema mwaka 2025 kampuni ilinunua parachichi kutoka kwa wakulima kwa zaidi ya Sh bilioni 9.8, huku mwaka huu ikitarajia kutumia zaidi ya Sh bilioni 10 kununua mazao hayo