Kansela Friedrich Merz na washirika wake wa muungano walikubaliana pia kuhusu hatua kadhaa mpya Alhamisi usiku zenye lengo la kuisaidia uchumi wa Ujerumani ambao umekuwa ukisuasua. Miongoni mwa hatua hizo ni kupunguza bei ya umeme kwa sekta za viwanda.
“Ujerumani imara inahitaji uchumi imara na ajira salama, zenye malipo mazuri,” alisema Merz akitangaza sera hizo.
Merz ameweka kipaumbele kuufufua uchumi wa nchi hiyo baada ya miaka miwili ya mdororo, akilegeza kanuni kali za ukopaji ili kuruhusu ongezeko la matumizi katika miradi ya miundombinu na ulinzi.
Kwa mujibu wa msemaji wa bajeti wa Chama cha Kijani, Sebastian Schaefer, kamati ya bajeti iliidhinisha rasimu ya mpango wa matumizi wa mwaka ujao ambayo sasa inatarajiwa kupitishwa na bunge mwezi Novemba.
Bajeti mpya inayotarajiwa kupitishwa
Katika bajeti hiyo mpya ambayo inatayarishwa na kutarajiwa kupitishwa na Bunge la Ujerumani mwezi wa Novemba inatarajiwa kuwa kama ifuatavyo.
• Jumla ya matumizi: yuro bilioni 524.5 zinapangwa kutumika
• Ukopaji mpya unatarajiwa kuwa takriban yuro bilioni 98
Hii ni juu ya makadirio ya mwisho wa Julai ambayo yalitabiri ukopaji wa euro 89.9 bilioni. Kwa mwaka 2025, deni linalotarajiwa ni karibu euro 82 bilioni.
Sehemu kubwa ya ukopaji mpya inalenga kuimarisha jeshi la Ujerumani, baada ya miaka ya kuwekezwa kidogo, huku nchi ikijiandaa kukabiliana na tishio lolote kutoka Urusi.
Ukosoaji na mgawanyiko wa kisiasa
Mbinu ya serikali imezua utata katika taifa hilo ambalo kwa muda mrefu limejiona kuwa na viwango vidogo vya deni ikilinganishwa na mataifa mengine yaliyoendelea.
Wakosoaji wanasema serikali inategemea kupanua deni ili kuleta ongezeko la muda mfupi la uchumi bila kushughulikia mageuzi ya kina yanayohitajika.
Schaefer aliukosoa muungano unaoundwa na CDU/CSU na SPD, akisema bajeti hiyo inayotarajiwa kupitishwa na bunge haina mipango ya muda mrefu ya kuendelea kulinda uchumi. “Bajeti ya 2026 inaonyesha kuwa hakuna mpango wa baadaye.” Alisema.
Alituhumu serikali kwa “kutapanya” mfuko maalum ulioundwa kwa ajili ya kuboresha miundombinu na miradi ya kimazingira, akisema sehemu ya fedha hizo zinatumika kugharamia matumizi ya kawaida badala ya uwekezaji wa muda mrefu.
Kupitia mpango mpya wa bei ya umeme, viwanda muhimu kama vile uzalishaji wa kemikali na chuma vitatozwa senti tano tu kwa kilowati kwa saa kuanzia 2026 hadi 2028.
Hatua hii inatarajiwa kuigharimu serikali kati ya yuro bilioni 3 hadi 5, kwa mujibu wa Waziri wa Fedha Lars Klingbeil.
Vilevile, muungano wa serikali umekubaliana kufuta ongezeko la kodi katika sekta ya usafiri wa anga, hatua ambayo inatarajiwa kuipunguzia sekta hiyo gharama ya karibu takriban yuro milioni 350.
