Mkutano kati ya Rais wa Urusi Vladimir Putin na mjumbe wa Marekani Steve Witkoff kujadili mpango wa Washington wa kukomesha vita nchini Ukraine ulimalizika baada ya takriban saa tano, Kremlin imetangaza siku ya Jumanne, Desemba 2. Urusi imesema kwamba hakuna maelewano yaliyofikiwa kuhusu maeneo yanayokaliwa nchini Ukraine. Washington, kwa upande wake, imeripoti “maendeleo” katika mazungumzo hayo.

Imechapishwa:

Dakika 2 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Wittkoff aliwasili Moscow mapema siku hiyo akiongozana na mkwe wa Rais wa Marekani Donald Trump, Jared Kushner. Vladimir Putin alionekana pamoja na mshauri wake wa kidiplomasia, Yuri Ushakov, na mjumbe wake wa masuala ya uchumi wa kimataifa, Kirill Dmitriev. Baada ya majadiliano ya saa tano, Witkoff, Kushner, wala Putin hawakuzungumza na waandishi wa habari. Steve Witkoff alikwenda moja kwa moja kwenye Ubalozi wa Marekani, ambapo alitarajiwa kutoa taarifa kuhusu majadiliano yake kwa Donald Trump.

Ni mjumbe wa rais wa Urusi, Kirill Dmitriev, aliyezungumza. Alielezea majadiliano hayo kama “yenye tija,” na mshauri mkuu wa Kremlin, Yuri Ushakov, alisifu mazungumzo “chanya”, ambayo alisema yanapaswa kuendelea. “Hatuko karibu zaidi na kutatua mgogoro nchini Ukraine,” alisema, akiongeza kuwa hakuna maelewano yaliyofikiwa kuhusu suala la Ukraine kukabidhi maeneo yanayokaliwa na kwamba “kazi nyingi bado zinapaswa kufanywa,” kulingana na shirika la habari la Urusi la Interfax.

“Tuliweza kukubaliana kuhusu baadhi ya mambo (…), mengine yalikosolewa, lakini jambo kuu ni kwamba majadiliano yenye kujenga yalifanyika na kwamba pande hizo zilitangaza nia yao ya kuendelea na juhudi zao,” Yuri Ushakov aliongeza. Alifafanua kwamba majadiliano hayo hayakuwa yamezingatia “maneno halisi” ya makubaliano, bali “kiini chake,” na kwamba hati kadhaa zilizowasilishwa Moscow zilijadiliwa, bila kuingia kwa undani.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio aliripoti “baadhi ya maendeleo” katika mazungumzo na Urusi ili kujaribu kufikia makubaliano ya kumaliza vita nchini Ukraine, wakati wa mahojiano yaliyorushwa siku ya Jumanne. “Kwa hivyo kile ambacho tumekuwa tukijaribu kufanya, na nadhani tumepiga hatua fulani, ni kubaini kile kitakachokubalika kwa Waukraine na kuwapa dhamana ya usalama kwa siku zijazo,” Rubio aliambia Fox News.

“Nchi za Ulaya ziko upande wa vita” 

Kabla ya mkutano wake na wajumbe wa Marekani, Vladimir Putin alisema kwamba Urusi haikutaka kwenda vitani na mataifa yenye nguvu ya Ulaya, lakini kwamba itakuwa tayari kupigana ikiwa Ulaya ikitaka mzozo wa moja kwa moja. “Wako upande wa vita,” alisema, akizishutumu nchi za Ulaya kwa kuzuia juhudi za Marekani kwa kuwasilisha mapendekezo wanayojua “hayakubaliki kabisa” kwa Moscow, ili waweze kuishutumu Urusi kwa kutotaka amani.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *