Takriban muongo mmoja uliopita, Amina Abdalla, kipindi hicho akiwa mmiliki wa kampuni ya utalii ya Tours and Safaris Limited, iliyokuwa na mafanikio mjini Mombasa, pwani ya Kenya, aliacha biashara hiyo, na yote yaliyompa fahari.

Kila kitu kilibadilika siku alipokutana na msichana mwenye umri wa takribani miaka ishirini, akitembea uchi mitaani huku watu wakimcheka. “Kama mzazi, sikuweza kupita tu,” Amina anakumbuka. Alimpeleka msichana huyo hospitalini na kugharamia matibabu yake ya afya ya akili kwa sababu, anavyosema, “Niliamini maisha yake yanaweza kuwa na matumaini.”

Kwa miezi sita, Amina alikuwa akimfuatilia msichana huyo ili aweze kupona. Alipomrudisha nyumbani, alimkuta baba yake ni kipofu, na maskini, na hakuwa na uwezo wa kumtunza. Miezi kadhaa baadaye, Amina alimpata msichana huyo akifanya biashara ya kuuza chapati na maharagwe, sasa akiwa ametulia kiakili na akimsaidia baba yake. “Kama ningemwacha vile nilivyompata, angeweza kudhulumiwa kingono, kupachikwa mimba au hata kupotea kabisa,” anasema Amina.

Tukio hilo lilibadilisha maisha yake. Aliuza magari yake ya biashara ya utalii, akijitolea kuwaokoa watu wanaoishi na matatizo ya afya ya akili mitaani. “Sikuona sababu ya kukaa ofisini nikisafirisha watalii. Niliamini ni wito wangu wa kufanya jambo ambalo Mungu angefurahia zaidi.”

Kabla kazi yake katika masuala ya afya ya akili haijafahamika kikamilifu, Amina tayari alikuwa ameanzisha shirika lisilokuwa la kiserikali la ‘‘Mombasa Women Empowerment Network’’ kama shirika la kijamii la kusaidia wanawake na watoto.

Lakini mahitaji makubwa aliyoyaona mitaani yalimfanya kupanua wigo wake. Alinunua ardhi, hata kabla ya kununua nyumba yake binafsi ya kuishi, na akajenga kituo cha kusaidia wenye matatizo ya afya ya akili. “Idadi ya wagonjwa ilikuwa kubwa mno, na gharama za matibabu zilikuwa juu. Nilijua nilihitaji kituo changu binafsi na daktari ili kupunguza gharama,” anaeleza.

Kila siku, Amina na wenzake huendesha gari wakipita mitaa ya Mombasa kuwaokoa watu. “Mara chache sana tunafika mjini kabla gari langu halijajaa,” anaiambia TRT Afrika. “Ukiwa pamoja na mimi, katika umbali wa chini ya kilomita moja naweza kuwakuta takriban watu kumi wagonjwa.” Huwa tunapokea simu hutoka viungani vya mji wa Mombasa na kaunti jirani.

Kilichoanza kama uokoaji wa muda sasa imekuwa kituo muhimu nchini Kenya kinachowaokoa watu wenye matatizo ya afya ya akili ambao hawajapata matibabu, kuwahudumia, kuwapa chakula, makazi, na elimu.

Kwa Amina, mitaa imekuwa wito wake kwa sababu ameona kwa macho yake unyama wanaopitia wagonjwa wa akili. Wengi hutengwa, kudharauliwa, au huitwa majina ya kejeli kama “wendawazimu,” “wamerogwa,” au “wamekabiliwa na mapepo.” “Hawatendewi haki kama binadamu wengine,” anaeleza. “Na unapomtendea mtu hivyo, anaanza kuamini kuwa yeye si wa dunia hii.”

Imani za kitamaduni husababisha kuwepo kwa changamoto kubwa zaidi. “Afya ya akili sio kile watu wanachofikiria,” Amina anasema. “Familia nyingi hushindwa kwa sababu wanaamini ni uchawi au laana.” Mtu anapojizungumzisha peke yake, familia hudhani ni mapepo. Katika familia nyingi, tabia zisizo za kawaida huhusishwa na adhabu kutoka kwa Mungu au laana.

Kufikiria hivyo hufanya familia kukataa kabisa matibabu ya kitaalamu. “Kwa miaka mingi, watu waliamini huwezi kupona,” anasema. “Waliwaita walioathirika waliolaaniwa, wamerogwa, au kuwatenga.”

Lakini unyanyapaa unazidi utamaduni. Kenya inakabiliwa na uhaba mkubwa wa wataalamu wa afya ya akili. Mombasa, jiji lenye zaidi ya watu milioni moja, lina chini ya matabibu wa magonjwa ya akili kumi pekee.

Kwa kuwa matatizo ya akili yanaathiri mtu mmoja kati ya wanne, mfumo hauwezi kukabiliana. “Wagonjwa wengi hawatibiwi, hawaonekani, hawasikiki,” Amina anasema.

Msaada wa serikali ni mdogo, na upatikanaji wa vifaa vya kufanya vipimo vya kama ubongo vinavyotumika nchi nyingine bado haupatikani. Matibabu yanategemea vipimo vya kitaalamu na dawa pekee, na kuifanya Kenya kubaki nyuma ikilinganisha na viwango vya kimataifa.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *