Ratiba ya mechi za nusu fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika AFCON 2025 zimekamilika na zinawakutanisha vigogo wa soka la Afrika: Senegal vs Misri, na Nigeria vs Morocco.
Hizo ndizo timu nne zilizobaki baada ya robo fainali za kusisimua, na zote zitachezwa mnamo siku ya Jumatano nchini Morocco.
Vita ya mabingwa na rekodi nzito
Senegal ilikuwa timu ya kwanza kufuzu nusu fainali baada ya ushindi wao wa 1–0 dhidi ya Mali, katika mchezo uliokuwa na ushindani mkali wa Afrika Magharibi.
Ushindi huo uliwapa nafasi Simba wa Teranga kuendelea kutafuta taji lao la pili la AFCON baada ya kulitwaa kwa mara ya kwanza mwaka 2021.
Misri ambao ni mabingwa mara saba wa Afrika, walipata ushindi wa 3–2 dhidi ya Ivory Coast, wakiizima ndoto ya mabingwa watetezi na kutinga nusu fainali kwa kishindo.
Mchezo huo uliwapa nguvu mpya na kuonyesha uzoefu wao mkubwa katika hatua za mtoano.
Safari ya Nigeria na Morocco
Nigeria Super Eagles wamekuwa miongoni mwa timu zenye kasi, nguvu na ubora mkubwa katika mashindano hayo. Safu yao ya ushambuliaji imekuwa ikifanya kazi kwa ufanisi, na wameonyesha uthabiti kuanzia mechi ya kwanza ya hatua ya makundi. Wamefika nusu fainali baada ya robo fainali yenye ushindani mkali.
Kwa upande wa Morocco ambao ni wenyeji wa mashindano hayo, wamekuwa katika kiwango bora na wanatumia faida ya kucheza nyumbani.
Kikosi chao kimejaa wachezaji wanaocheza Ulaya na kimeonyesha uimara wa kiufundi na kimbinu. Wanakutana na Nigeria katika kile kinachoitwa fainali kabla ya fainali.