Serikali nchini Uganda imezima mtandao wa intaneti siku chache kuelekea uchaguzi mkuu wa hapo kesho, uchaguzi ambao Rais Yoweri Museveni anataka kuchaguliwa kwa muhula wa saba.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Mamlaka ya mawasiliano katika taifa hilo la Afrika Mashariki inasema imechukua hatua hiyo kuzuia usambazwaji wa habari za kupotosha na kuchochea vurugu.
Licha ya kuthibitisha kuzima intaneti, haikuweka wazi ni lini huduma hiyo itarejeshwa au makataa hayo yatadumu kwa muda gani, jambo ambalo tayari limeibua maswali kuhusu uwazi kuelekea uchaguzi wa hapo kesho.
Mashirika ya kutetea haki za binadamu ya ndani na nje yameonya dhidi ya hatua hii, waliyosema ni wazi ina nia ovu kutaka kuwaweka raia gizani ili wasipate taarifa kwa wakati.
Hatua hii ya mamlaka ya mawasiliano imekuja juma moja kupita tangu mkurugenzi wake akanushe taarifa kuwa serikali ilikuwa na mpango wa kuzima intaneti kabla, wakati na baada ya uchaguzi.
Hatua sawa na hii ilichukuliwa pia katika uchaguzi wa mwaka wa 2021, uchaguzi ambao hata hivyo uligubikwa na udaganyifu pamoja na mamlaka kutumia nguvu dhidi ya wapinzani.
Kilichofanyika Uganda, hakina tofauti na kile kilichofanywa na mamlaka za Tanzania ambazo zilizima Intaneti kwa karibu siku 5 baada ya kutokea machafuko ya wakati na baada ya uchaguzi uliopingwa na upinzani ambapo rais Samia Suluhu Hassan alitangazwa mshindi.
