Togo imefikia hatua ya kihistoria kwa kuwa nchi ya 22 barani Afrika kuanzisha chanjo ya malaria ya R21/Matrix-M, kuanzia Septemba 1, 2025. Nchi hiyo ni ya kwanza barani humo kufanya hivyo moja kwa moja nchini kote, ikijumuisha nchi nzima tangu awali. Kulingana na Shirika la Afya Duniani (WHO), mabadiliko haya ya kimkakati yaliwezekana “kwa dhamira kali ya kisiasa,” na serikali ya Togo ilifadhili dozi hizo.

Imechapishwa:

Dakika 2 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Malaria bado imeenea sana nchini Togo katika mikoa yote ya nchi. Ugonjwa huu huwa mbaya zaidi hasa wakati wa mvua, wakati mbu huongezeka zaidi. Mnamo mwaka 2022, liwakilish 60% ya sababu za mashauriano katika vituo vya afya. Watoto walio chini ya umri wa miaka mitano walifikia 34% ya kesi na karibu 65% ya vifo vinavyohusiana na ugonjwa huo, na kuwafanya kuwa walengwa wakuu wa kampeni hii ya chanjo.

Chanjo ya R21/Matrix-M, iliyoidhinishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), itatolewa kwa dozi nne: katika miezi mitano, miezi sita, miezi saba na miezi kumi na tano. Takriban watoto 269,000 wanalengwa katika awamu ya kwanza, ambayo kwa wakati mmoja itaendeshwa katika wilaya 39 za afya nchini.

Kupunguza maradhi yanayohusiana na malaria

Adidja Amani, anayehusika na kuanzishwa kwa chanjo mpya katika Ofisi ya WHO kanda ya Afrika, anakaribisha uamuzi ambao “unaleta matumaini ya mapambano dhidi ya malaria barani Afrika.” Anasisitiza ufanisi wake: “Kwa sababu chanjo hii, pamoja na afua zingine, inapunguza kwa kiasi kikubwa magonjwa yanayohusiana na malaria.” “Katika nchi za majaribio kama Kenya, Malawi, na Ghana, tumeona kupungua kwa vifo vya watoto kwa asilimia 13,” amemwambia mwandishi wa RFI kitengo cha Afrika Christina Okello.

Lakini anasema kuwa ulinzi unategemea kufuata ratiba ya chanjo. “Huu ni ujumbe wa kuwatia moyo akina mama, kuwataka waje kuchukua dozi zote nne. Moja ya changamoto tunayokabiliana nayo ni dhana kwamba sindano moja inatosha. Hata hivyo, nchini Togo, ratiba inatoa dozi katika miezi mitano, sita, saba na kumi na tano. Ni kwa kuheshimu kampeni hii ambapo watoto watalindwa ipasavyo.”

Chanjo inayokamilisha zana zilizopo

Chanjo ya R21 haichukui nafasi ya mikakati iliyopo—vyandarua vilivyonyunyuziwa dawa, unyunyiziaji wa dawa ndani ya nyumba, uzuiaji wa kemikali kwa wanawake wajawazito na watoto, pamoja na utambuzi wa mapema na matibabu—lakini inaziimarisha kama kizuizi cha ziada.

Kwa utangulizi huu, Togo inaungana na nchi nyingine 21 za Afrika ambazo tayari zimejitolea kwa chanjo hii. Kulingana na WHO, mafanikio haya “yanaonyesha uongozi dhabiti, mipango madhubuti, na dhamira ya wazi ya kusambaza dawa nchi nzima,” amesema Mkurugenzi wake katika kanda ya Afrika Dk. Mohamed Janabi.

Nchi inatarajia kuanzisha enzi mpya katika vita dhidi ya ugonjwa wa malaria, sababu kuu ya vifo vya watoto, na kuokoa maelfu ya maisha ya watu kila mwaka.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *