
Somalia na Rwanda wamethibitisha dhamira yao ya kuimarisha ushirikiano wa kijeshi kama sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama katika kanda ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Ujumbe wa jeshi la Somalia ulioongozwa na Mkuu wa Majeshi, Meja Jenerali Odawa Yusuf Rage, ulianza ziara rasmi ya siku sita nchini Rwanda, wakiangazia ushirikiano zaidi kati ya Jeshi la Somalia (SNAF) na Jeshi la Rwanda (RDF).
Meja Jenerali Odawa, ambaye aliteuliwa tena kuwa mkuu wa majeshi ya Somalia Novemba 2024, ameandamana na maafisa waandamizi wa Somalia, ikiwemo Luteni Kanali Iimaan Elman, Mkuu wa ushirikiano kati ya Raia na Jeshi (CIMIC) katika jeshi la Somalia.
Wakati wa ziara hiyo, ujumbe wa Somalia unatarajiwa kutembelea taasisi muhimu za jeshi nchini Rwanda chini ya Wizara ya Ulinzi, pamoja na Makumbusho ya mauaji ya kimbari, ikiwa sehemu ya mafunzo kuhusu taasisi za elimu na uponyaji baada ya vita.