Mkataba huo umesainiwa mbele ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mipango wa Iraq, Dkt. Muhammad Ali Tamim, na Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa Msaada kwa Iraq UNAMI, Mohamed Al-Hassan.
Sanamu ya Al-Mutanabbi mmoja wa washairi maarufu katika ulimwengu wa Kiarabu ikiwa kando ya mto Tigris Baghdad
Vipaumbele vinne vya kimkakati wa kitaifa
Mfumo wa UNSDCF umejengwa juu ya vipaumbele vinne vya kimkakati vinavyolingana kwa karibu na Mpango wa Kitaifa wa Maendeleo wa Iraq wa 2024–2028 na Dira ya 2030.
Kipaumbele cha kwanza kinalenga kuboresha upatikanaji wa elimu, huduma za afya na huduma za kijamii, kuhakikisha kuwa WaIraq wote hasa wanawake, watoto na familia zilizofurushwa makwao wanapata huduma bora na mifumo madhubuti ya ulinzi wa kijamii.
Nguzo ya pili inalenga ajira na ukuaji wa uchumi, ikijumuisha kuwezesha vijana na wanawake, kuongeza fursa za ajira, na kuendeleza miradi ya kiuchumi endelevu na rafiki kwa mazingira.
Kulinda mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ni kipaumbele cha tatu, kikilenga usimamizi bora wa rasilimali asilia, kuimarisha uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, na kupunguza hatari za majanga.
Kipaumbele cha nne kinahusu utawala bora na utawala wa sheria, kikilenga kuimarisha taasisi za umma, kukuza haki na usawa, na kuendeleza amani na mshikamano wa kijamii kote nchini Iraq.
Umoja wa Mataid=fa leo umefunga rasmi mpango wake nchini Iraq UNAMI
Mpito kuelekea ushirikiano wa maendeleo endelevu
Akizungumza katika hafla ya kusaini, ushirikiano huo Bwana. Al-Hassan ameelezea mfumo huo kuwa ni hatua muhimu katika mahusiano kati ya Iraq na Umoja wa Mataifa.
“Kutiwa saini kwa mfumo huu ni mpito wa asili na wa heshima katika uhusiano kati ya Umoja wa Mataifa na Jamhuri ya Iraq. Unaakisi kuondoka kwa utaratibu na uwajibikaji kutoka katika msaada wa uthabiti wa kisiasa kuelekea hatua ya kuimarisha ushirikiano wa maendeleo endelevu kati ya Iraq na shirika la Umoja wa Mataifa,” amesema.
Historia: Ushirikiano kati ya Umoja wa Mataifa na Iraq
Umoja wa Mataifa umekuwa ukifanya kazi nchini Iraq kwa miongo kadhaa tangu mwaka 2003, ukitoa msaada wa kibinadamu, kuunga mkono michakato ya kisiasa, na kusaidia kuleta uthabiti baada ya miaka ya migogoro na ukosefu wa usalama. Katika miaka ya hivi karibuni, mchango wa Umoja wa Mataifa umeelekezwa zaidi kwenye maendeleo, sambamba na kuimarika kwa hali ya usalama na kuongezeka kwa umiliki wa kitaifa wa juhudi za mageuzi na ujenzi upya.
Mfumo mpya wa UNSDCF unajengwa juu ya mifumo ya awali ya ushirikiano na unaakisi vipaumbele vinavyobadilika vya Iraq, kutoka katika hatua ya uthabiti baada ya migogoro kuelekea maendeleo ya muda mrefu, mnepo na uimarishaji wa taasisi.
Mkuu wa UN akiwa katika hafla ya kuweka shada la maua kuwakumbuka wafanyakazi wa UN waliouawa katika shambuio la hotel ya Canal Baghdad mwaka 2003 alipozuru Iraq hivi karibuni
Mustakbali wa taifa hilo
Mfumo wa Ushirikiano wa 2025–2029 utakuwa chombo kikuu cha kimkakati kitakachoongoza msaada wa maendeleo wa Umoja wa Mataifa nchini Iraq katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Unalenga kuhakikisha mbinu iliyoratibiwa na inayolenga matokeo miongoni mwa mashirika, wakfu na programu za Umoja wa Mataifa, kwa kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Iraq na wadau wa kitaifa.
