Mamlaka za waasi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC zinasema watu zaidi ya 200 wameuawa katika mgodi ulioporomoka huko Rubaya mashariki mwa nchi hiyo Januari 28.
Shirika la habari la Reuters liliripoti idadi hiyo ya vifo, likinukuu mamlaka kutoka kundi la waasi la M23, ambalo linadhibiti eneo hilo.
Mgodi huo unazalisha coltan, madini yenye metali ambayo yana nyenzo muhimu ya tantalum, inayotumika kutengenezea vifaa vya kielektroniki kwa ajili ya simu za smartphone na bidhaa zingine.
Shirika la Habari la Associated Press linasema asilimia zaidi ya 15 ya usambazaji wa tantalum duniani hutoka kwenye migodi huko Rubaya.
Kulikuwa na wasiwasi kuhusu uwezekano wa kuporomoka, kwani handaki huchimbwa kwa mikono na hatua za usalama hazitoshi.
Umoja wa Mataifa unasema kwamba migodi hiyo imekuwa chanzo cha ufadhili wa mashambulizi ya M23 huko mashariki mwa nchi hiyo.
Kundi hilo la waasi, linaloungwa mkono na nchi jirani ya Rwanda, limekuwa likipambana mara kwa mara na vikosi vya serikali ya DRC.
Ukichochewa na shauku kubwa katika madini muhimu, utawala wa Rais wa Marekani Donald Trump umeingilia kati ili kuleta amani.